Tuesday, September 4, 2012

 Waziri nchimbi hapa akisisitiza kitu katika mkutano huo uliofanyika leo mchana katika makao makuu ya jeshi la polisi.

 Hapa Waziri Nchimbi aliwataka watu wote kusimama dakika moja kuomboleza kifo cha Mwandishi Daud.

 Waziri wa mambo ya ndani Dk Emmanuel Nchimbi akijinasibu kuwa yeye ni muumini wa haki hapendi dhulma.

Maafisa wa jeshi la Polisi wakimsikiliza kwa makini bosi wao Waziri Dk Emmanuel Nchimbi.


NA Hafidh Kido

Waziri wa mambo ya ndani Dk Emmanuel Nchimbi ameshangazwa na ukimya wa mkuu wa jeshi la polisi nchini IGP Said Mwema juu ya mauaji ya mwandishi yaliyotokea Mkoani Iringa wiki iliyopita.

Akizungumza na waandishi wa habari katika makao makuu ya jeshi la polisi nchini wakati akitaja majina matano ya watu watakaokuwa katika tume aliyoiunda kuchunguza mauaji hayo.

Dk Nchimbi alisema haamini kama IGP Mwema anastahiki nafasi hiyo maana amekuwa mpole sana kabla na baada ya tukio la Iringa mbali ya kupokea ujumbe wa simu kutoka kwa Dk Slaa uliomtaka kuandaa silaha za kutosha kukabiliana na mauaji yatakayotokea.

“Mimi nilishangaa sana namna IGP alivyomnyenyekea katibu mkuu wa CHADEMA Dk Wilbord Slaa tarehe 28 mwezi uliopita juu ya kusitisha maandamano na mikutano ya chama hicho ili kupisha sensa. Maana alimnyenyekea na kumbembeleza utadhani anamuomba nini sijui, mpaka nikajiuliza huyu ni IGP kweli.

Kama hiyo haitoshi tarehe moja mwezi huu siku moja kabla ya mauaji ya Iringa IGP alipokea ujumbe wa simu kutoka kwa DK Slaa kumtaka kuandaa silaha za kutosha kukabiliana na karamu ya mauaji siku ya pili. Lakini alipuuza na kweli mauaji yalitokea,” alisema Nchimbi.

Ujumbe huo wa simu uliotumwa kwa IGP Mwema kutoka kwa DK Slaa ulisomeka hivi “IGP nasubiri simu yako. Wajulishe Polisi wako waandae risasi za kutosha, mabomu ya kutosha. Mtakuwa na karamu ya mauaji na kisha kusherehekea, mjiandae kwa kwenda mahakama ya The Hegue. Ni afadhali kufa kuliko manyanyaso haya.”

Mbali na hayo Dk Nchimbi aliwaasa wanahabari kutoshabikia mambo haya yanayoendelea nchini na kuhoji ikiwa chadema wanafurahia mambo yanayotokea ama nao wanahuzunika.

“Hebu tujiulize kwa pamoja ndugu zangu, hawa chadema hawajui umuhimu wa sensa ama wanafanya kusudi. Na walishawahi kujiuliza ndani ya miezi mitatu mikutano yao mitatu imeua watu watatu familia za marehemu hawa zinakuwa katika hali gani. Mbona wapo wanaharakati kabla yao walifanya harakati bila mauaji,” alihoji Dk Nchimbi.

Aidha katika mkutano huo Waziri Dk Nchimbi alitaja majina ya wajumbe watano watakaokuwa katika tume huru ya kuchunguza mauaji hayo na kuwapa siku thalathini kumletea majibu ya kueleweka.

“Nimeunda tume ya watu watano itakayokuwa chini ya uenyekiti wa jaji mstaafu Time Ihemba, nikawaambia jukwaa lawahariri wanipe jina moja wakanipa jina la Teoful Makunga, pia nikawaomba MCT wanipe jina moja wakanipa Pili Mtambalike. Wakati jeshi la wananchi Tanzania wamenipa mtaalamu wa milipuko kanali Wema W.Wapo, na upande wa jeshi la polisi tunae kamishna Esaya Mkulu.

Tume hii itakuwa huru na ya haki hakuna kupendelewa wala kushindwa kwa jambo lolote lile, na nimeshawaambia ikiwa watakuwa na tatizo lolote la kitaalamu wasisite kuwasiliana na wizara ili tuombe msaada kutoka nje” Dk nchimbi.

Akifafanua masuala ya msingi ambayo yataangaziwa katika tume hiyo Dk Nchimbi alisema, yapo mambo sita ambayo mpaka sasa ndiyo yanayotajwatajwa na watu katika mitandao ya kijamii na hata jukwaa la wahariri walitaja baadhi.

“Yapo mambo sita ambayo yatakuwa kama muongozo kwa kamati hii, Kwanza nini chanzo cha mauaji, bomu, risasi ama nini. Pili ni kweli upo uhasama baina ya jeshi la polisi na waandishi wa mkoa wa Iringa. Tatu, ni kweli wapo waandishi watatu ambao inadaiwa jeshi la polisi mkoani humo wamewaweka katika orosha ya kuwashughulikia.

“Nne, ukubwa wa nguvu iliyotumika kumkamata Marehemu Daud Mwangosi na wafuasi wa chadema ilikuwa na uhalali wowote. Tano, Vyama vya siasa ni kweli wamepanga kukata rufaa mara wasiporisdhishwa na tume ya polisi iliyoundwa kuchunguza tukio hilo. Na mwisho ni kutaka kujua kuwa ni kweli mkoani Iringa upo mvutano wa muda mrefu baina ya jeshi la polisi na vyama vya siasa,” alieleza Dk Nchimbi.

Katika hatua nyingine jembe lenu lilimuuliza Waziri Dk Nchimbi ikiwa atakuwa tayari kuwajibika mara baada ya ripoti ya tume hiyo kutolewa na kubainika jeshi la polisi lilihusika moja kwa moja na mauaji hayo.

Majibu yake yalikuwa haya “Mbona unaharakisha majibu ya tume namna hiyo, labda niwaambie kitu mimi ni muumini wa haki na ikiwa itabainika kuna kuchezewachezewa haki kila aliehusika atawajibishwa kwa mujibu wa sheria.”

Lakini baada ya jembe kusisitiza kutoridhishwa na majibu yake kwani swali la msingi lilikuwa ni yeye akiwa waziri ambae jeshi la polisi lipo chini yake atakubali kuwajibika.

Alijibu kwa hamaki “mbona hamunielewi na mnasisitiza vitu kama hivyo, mimi jamani nikiondoka mtanikumbuka shenziii,” alihamaki Dk Nchimbi.
HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
04/09/2012



No comments:

Post a Comment