Wednesday, September 5, 2012

Uchaguzi CCM NEC waduwaza wakongwe...



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji) Dk Mary Nagu
Waandishi Wetu
MBIO za uchaguzi ndani ya CCM zimefikia patamu, baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji) Dk Mary Nagu kuenguliwa kugombea nafasi ya Ujumbe wa Nec kupitia Wilaya ya Hanang', huku Mke wa Rais, Salma Kikwete akiwa mgombea pekee wa nafasi hiyo Lindi Mjini.

Mkoani Dar es Salaam, mbio hizo zimeonekana kuwaweka pabaya Mwenyekiti wa UWT wa mkoa huo Zarina Madabida na Katibu wake, Tatu Maliaga baada ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa, John Guninita kueleza kuwa viongozi hao watafikishwa kwenye kamati ya maadili kueleza kwa nini wamesitisha uchaguzi wilayani Kinondoni.

Habari kutoka Hanang' zimeeleza kuwa Kamati ya Siasa ya CCM ya Wilaya hiyo imemwengua Dk Nagu na kuwabakiza wagombe wawili, Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye na Leonsi Marmo.

Taarifa kutoka kwenye kikao hicho kilichofanyika juzi katika Ofisi ya CCM ya wilaya hiyo na kuhudhuriwa na wajumbe 12 zimeeleza kuwa Dk Nagu ameenguliwa kutokana na maelezo kuwa kanuni hazimruhusu kugombea.
Chanzo cha habari kimeeleza kuwa kanuni iliyomwondoa Dk Nagu kwenye kinyang’anyiro hicho ni ile inayowataka viongozi wenye kazi za kila siku; ubunge na uwaziri kutogombea.

Imeelezwa kuwa jitihada za wajumbe watano waliojipambanua katika kikao hicho kumtetea Dk Nagu ziligonga mwamba, baada ya wenzao saba kuunga mkono uamuzi huo.

“Kikao kilikuwa kizito, lakini tulitazama zaidi kanuni, sifa za wagombea na uwezo wa wagombea hasa katika nafasi hii nyeti ya Nec kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015,” alisema mmoja wa wajumbe wa kikao hicho.
Alisema mapendekezo ya kikao hicho, tayari yamefikishwa ngazi ya CCM mkoa kwa uamuzi zaidi na baadaye yatafikishwa Kamati Kuu (CC) ya CCM.

“Sisi tumemaliza kazi yetu, tunaamini kuwa tumetenda haki kwa manufaa ya chama chetu Wilaya ya Hanang’,” alisema kiongozi huyo.

Hata hivyo, mjumbe mwingine wa kikao hicho alisema, mgawo wa mkopo wa matrekta ambao umekuwa ukiendelea Hanang’ umechangia kumwengua waziri huyo.

“Hapa kuna mambo mengi, nadhani hao waliokuwa na taarifa hizi, wameshindwa kueleza zaidi. Kuna mambo ya chinichini hasa baada ya baadhi ya viongozi kutounga mkono uamuzi wa Waziri Nagu kusaidia baadhi ya wanaCCM wakiwamo viongozi kukopeshwa matrekta,” alisema mjumbe huyo.

Kiongozi mmoja wa CCM Wilaya ya Hanang’ ambaye hakutaka jina lake litajwe, alikiri kufanyika kwa kikao hicho na kueleza kuwa tatizo la Dk Nagu ni kutoombewa kibali na kamati ya siasa wilaya au mkoa kama kanuni zinavyotaka.
Alieleza kuwa kanuni za CCM zinataka viongozi wenye majukumu ya kila siku kuombewa kibali kwanza na Kamati ya Siasa ya Wilaya au Mkoa kabla ya kugombea jambo ambalo halikufanyika kwa Dk Nagu.

“Hadi kikao hicho kinafanyika, Dk Nagu alikuwa hajaombewa kibali hicho na hili limetokana na migogoro ya kisiasa iliyoko wilayani Hanang’,” alisema.

Alipoulizwa kuhusu hilo, Katibu wa CCM Wilaya ya Hanang’, Allan Kingazi alisema: “Ni kweli kikao kilifanyika, lakini mapendekezo yetu ni siri na hao waliokuambia wamekiuka kanuni. Sisi baada ya kumaliza kikao chetu, mapendekezo yetu tumeyapeleka ngazi ya mkoa ambako pia yataendelea kuwa siri hadi majina yatakapotangazwa rasmi,” alisema.

Uamuzi wa Dk Nagu kuamua kugombea NEC kupambana na Sumaye ambaye ndiye alimwachia jimbo hilo, ulitabiriwa kuibua mgawanyiko mkubwa ndani ya wana CCM wa Hanang’.
Jitihada za gazeti hili kumpata Dk Nagu kuzungumzia uamuzi huo zilishindikana baada ya simu yake ya mkononi kuita muda mrefu bila kupokewa.

Kuenguliwa kwa Dk Nagu kunatokana na sababu za kuwa na kazi za muda wote kumeibua hofu kuhusu hatima ya viongozi wengine waliochukua fomu ambao kwa mujibu wa kanuni iliyomwondoa Dk Nagu nao hawakupaswa kugombea.
Hao ni pamoja na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika na Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk Abdallah Kigoda, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk Emmanuel Nchimbi.

Wengine ni Wabunge Deo Filikunjombe (Ludewa), Mussa Azzan Zungu (Ilala), Dk Hamis Kigwangalla (Nzega) na Andrew Chenge (Bariadi Magharibi).

Salma akosa mpinzani Lindi
Katika hatua nyingine Mke wa Rais, Salma Kikwete amerudisha fomu ya kuwania ujumbe wa Nec Taifa kupitia Wilaya ya Lindi Mjini.

Katibu wa CCM Wilaya ya Lindi Mjini Mohamed Kateva, alisema jana kwamba Salma ni mgombea pekee aliyejitokeza kuwania nafasi hiyo katika wilaya yake.

Kateva alisema mwisho wa kurudisha fomu ilikuwa Agosti 28, mwaka huu na mpaka tarehe hiyo hakukuwa na mtu mwingine aliyekuwa amejitokeza kuwania nafasi hiyo....
www.mwananchi.co.tz 

No comments:

Post a Comment