Tuesday, October 16, 2012

Msome mama Joyce Mbwette kutoka Foot Loose Tanzania LTD.....

 Hapa akielezea hadithi yake mbele ya maafisa wa unalozi wa Marekani walipomtembelea ofisini kwake leo alasiri maeneo ya Mwenge Dar es Salaam.

                                                         Hizi ni moja ya bidhaa zake.

 Maafisa ubalozi wakiwa makini kuandika kila walichoona ni muhimu kutoka katika hadithi tamu ya mama huyu.


 Hapa akionyesha baadhi ya bidhaa zinazotengenezwa kwa kutumia mikono kutoka katika kampuni yake.

 Balozi Demetrios Marantis akimuuliza swali mama Joyce wakati alipokuwa akijieleza mbele yake.

                                                               Bidhaa nyingine hizi.


Hapa Balozi Demetrios akizungumza na mama Joyce wakati walipoingia katika banda la uchoraji na utengenezaji mabatiki.

 Akiondoka huku akiwa ana uso wa furaha kutokana na saa moja iliyokuwa nzuri kwake na Foot Loose.

Hapa wafanyakazi wa Foot Loose wakimpa zawadi balozi huyo baada ya kufurahishwa na maneno yake.


Leo kidojembe nilihudhuria kibanda cha mjasiriamali mama Joyce Mbwette, kulikuwa na ziara ya mtu mkubwa kutoka serikali ya marekani ambae alitaka kujua kuhusu wafanyabiashara wa kitanzania na namna ambavyo wanaweza kuuza bidhaa zao nchini Marekani.

Kibanda hicho cha mjasiriamali mama Joyce kinaitwa Foot Loose Tanzania Limited, anajihusisa na uchongaji vinyago, uchoraji picha za tingatinga, mabatiki na vikapu. Zipo bidhaa nyingi ambazo nikianza kuzitaja mojamoja sitoweza kuzimaliza; ila ibakie tu kuwa anafanya biashara ya kuuza mapambo ya kiafrika.

Naibu mwakilishi wa biashara kutoka nchini Marekani au kwa kizungu cheo chake unaweza kukiita ‘US Deputy Trade Representative’ Balozi Demetrios Marantis, anafanya ziara nchini Tanzania na inadaiwa atatembelea baadhi ya wafanyabiashara ndogondogo za kijasiriamali jijini Dar es Salaam na mjini Unguja kwa lengo la kuongeza nguvu mahusiano ya kibiashara baina ya Tanzania na Marekani.

Ikumbukwe nchi ya Marekani ipo katika kuhangaika kutafuta namna ya kushindana kibiashana na nchi ya China, kwa maana China wameshatangaza sera yao ya mambo ya nje ni tunakwenda Africa ‘We are going to africa’. Sasa wameamua kutengeneza bidhaa rahisi ili ziweze kununuliwa kwa wingi na waafrika maskini.

Hivyo Marekani kwakuwa hawawezi kutengeneza bidhaa rahisi wameamua kuja wenyewe ili kungalia namna ya kuwainua wajasiriamali wa kiafrika na kuona ni namna gani wataweza kufanya nao biashara bila kupoteza lengo na sera zao za mahusiano kwa mataifa ya nje.

Nimefarijika sana na maelezo ya mama Joyce mbele ya mgeni wake, alijieleza vizuri sana kwa lugha ya kikoloni ‘english’ mpaka ndugu balozi alionekana kuvutiwa na hadithi yake ya mafanikio katika biashara.

Mama Joyce anaeleza kuwa alianza biashara hiyo mwaka 1999, mpaka kufikia sasa ameweza kutengeneza kampuni yeye na mume wake. Ametembea mataifa mengi yakiwemo Marekani, Ujerumani, Japan, Sweden na Uingereza kuhudhuria matamasha na mikutano mbalimbali inayohusu wajasiriamali.

“Nilianza biashara hii mwaka 1999 baada ya kuacha kazi katika benki ya bishara ya taifa NBC. Mafao yangu niliongeza na baadhi ya vijisenti nilivyohifadhi na kuamua kufungua kampuni hii kipindi hicho ikiwa changa sana,” anaeleza mama Joyce kwa furaha.

Yeye na mume wake wamepata bahati kubwa sana ya kusaidiwa na serikali ya Tanzania kwa kuingizwa katika baadhi ya misafara ya Rais nchi za ulaya na Marekani hivyo kupata nafasi ya kujitangaza na kutengeneza marafiki na wateja wapya kila siku.

Anasema kampuni yake inachangia kutoa ajira zipatazo 700, ingawa si moja kwa moja. Maana akipokea maombi ya bidhaa nyingi kutoka ulaya ama Amerika huita watu mbalimbali wenye utaalamu wa masuala ya uchoraji, ufinyanzi, uchongaji na ususi kisha huwapa oda ya vitu anavyotaka na tarehe ya mwisho kuleta bidhaa hizo. Hivyo kwa mtindo huo idadi kubwa ya vijana na kinamama hupata ajira ingawa si ya kudumu.

“Mara nyingine naweza kupokea oda ya makontena mawili ya bidhaa mbalimbali kama vikapu na picha za tingatinga ninachofanya ni kuita watu na kuwapa kazi hiyo halafu mimi ninanunua kutoka kwao. Ila mara nyingi nikipokea oda kubwa kama hiyo nawaomba wateja wangu watume wawakilishi watakaosimamia viwango vya bidhaa hizo ili isijekutokea baada ya kutuma mzigo kwa gharama kubwa matokeo yake unakuwa chini ya kiwango na kurudishwa,” alimuleza balozi Demetrios.

Kwa upande wake balozi Demetrios alimsifia mama Joyce kwa kumwambia hachoki kumsikiliza kwani anazungumza vitu ambavyo binaadamu yeyote mpenda maendeleo atatamani kusikiliza zaidi na zaidi.

“Siwezi kuacha kusikiliza hadithi yako ya kuvutia kuhusu biashara hii. Inaonekana wewe ni kiigizo chema ‘role model’ kwa wanamama wa kitanzania, ninapenda kupitia kwako wanamama wa kitanzania waone namna nchi ya Marekani inavyoweza kutoa nafasi za kufanya biashara na Tanzania hivyo ni vema kuzichangamkia nafasi hizo,” alieleza balozi huyo.

Kama kawaida yangu kidojembe nilipopata nafasi nilimtwanga swali balozi Demetrios ambapo nilitaka kujua ni kitu gani kimemshangaza ama hakukitegemea kukiona ama kukisikia kutoka kwa mama huyo.

Haya ndiyo yalikuwa majibu yake, “leo nimeonana na mwanamke wa shoka kitu kilichonishitua kutoka kwake na sikutegemea kukisikia ni namna alivyoweza kuwasaidia watanzania wenzie kupata ajira. Kampuni ndogo kama hii kuzalisha ajira 700 ni kitu cha kuvutia na kushangaza sana, hakika nimeshangazwa hii ni hadithi ambayo nitaikumbuka mpaka nikirudi nyumbani.”   

Waswahili wanasema ‘halifai lakini lapumbaza’ yaani nchi ya Marekani inasemwa inanyonya nchi changa lakini mbali ya kuwa ni mbaya lakini inasaidia kwa upande mwengine waafrika tunapumbazika kwa misaada yake na ‘vita ya panzi furaha ya kunguru’ yaani vita ya kibiashara baina ya China na Marekani inatusaidia hata sisi wachanga tunakumbukwa. Tazama mtu mzito kama huyu ambae ameteuliwa na Rais Obama na kupitishwa na maseneta ameikumbuka nchi kama Tanzania na kuona ni watu ambao anaweza kushirikiana nao katika biashara.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
16/10/2012

No comments:

Post a Comment