Monday, October 22, 2012

Nilichojifunza vurugu za Waislamu Tanzania bara na visiwani....




Kwanza naomba ‘ku-declare interest’ kwa Kiswahili wanasema kukubali kuwa na maslahi katika Uislamu. Maana nami ni muislamu tena safi. Hivyo katika makala haya ikiwa nitateleza na kuutetea Uislamu katika namna ambayo itakujengea maswali naomba mnisamehe wasomaji, si kupenda kwangu.

Wiki mbili zilizopita kulitokea matukio mawili yaliyoongozana utadhani yalipangwa, moja lilitokea mjini Dar es Salaam maeneo ya Mbagala kwa kijana wa miaka 14 kuinajisi Quran. Tukio la pili lilitokea mjini Zanzibar baada ya kiongozi wa Uamsho Sheikh Farid kudaiwa kupotea katika mazingira ya kutatanisha.

Matukio haya mawili ukiyapima kwa umakini hayakupasa kutokea ikiwa Serikali yetu ingeyachukulia kwa uzito wake na kuyaamua kwa kutumia hekima kitu ambacho hata jamii ya waislamu walishindwa kukifanya.

Upungufu wa hekima ndicho kilema kilichosababisha machafuko yote Zanzibar na Bara. Pia kutumika kisiasa na mataifa ya nje hasa ya kiarabu limeonekana kwa asilimia kubwa kuwa ni chanzo kingine. Na hili ni kwa mujibu wangu wala sijasikia kwa mtu yeyote. Bali ni namna matukio yalivyotokea.

Tuanze na sheikh Ponda Issa Ponda, huyu ni katibu wa jumuiya na taasisi za Kiislamu Tanzania. Yeye alikamatwa kwa tuhuma za kuchochea vurugu na uvunjifu wa amani nchini.

Sababu kuu mbali ya vurugu za mbagala zilizosababisha makanisa matatu kuchomwa na kuharibiwa vibaya baada ya kijana mmoja kukojolea kitabu cha Quran ikiwa ni ubishani wa kitoto na mwenzie ambae inadaiwa alikuwa muislamu. Alimwambia kijana huyo wa kikristo kuwa mtu yeyote akikojolea kitabu hicho kitukufu atageuka panya au maelezo mengine yanasema atageuka nyoka.

Sababu nyingine ya kukamatwa kwa Sheikh Ponda ni uvamizi wa kiwanja namba 311/3/4 kilichopo Chang’ombe karibu na uwanja wa taifa mali ya kampuni ya Agritanza.

Nilitangulia kusema hekima ingetumika balaa hili lisingetokea ni kuwa mtoto yule (alieidharau Quran) tayari alikuwa mikononi mwa polisi. Kisheria ni mhalifu, maana kwa mujibu wa katiba yetu mtu hatakiwi kudharau dini ya mwenzie kwasababu kila mtu anao uhuru na mipaka ya kuabudu ingawa serikali haina dini. Kundi la watu kuenda kumtoa mhalifu katika kituo cha polisi ni kosa kisheria hata huko Makka na Madina dini ya kiislamu ilipoanza tendo hili lisingeweza kukubalika.

Simaanishi tendo la kunajisi Quran, bali kitendo cha wananchi kuvamia kituo cha polisi na kutaka kumtoa mhalifu mkamuhukumu mnavyojua nyinyi.

Kitu cha pili maandamano ama vurugu zinavutia watu wengi, waislamu na wasio waislamu. Wezi na wastaarabu, wenye akili timamu na wendawazimu. Hivyo inawezekana kabisa walioharibu makanisa  si waislamu bali ni wahuni tu ambao wametumia mgongo wa maandamano kutimiza dhamira zao chafu.

Mafundisho ya dini ya kiislamu hayakubali wizi (kitu ambacho kilifanyika). Mafundisho hayakubali uharibufu wa mazingira katika vita (kitu ambacho kilifanyika) hapa nitafafanua.

Dini ya kiislamu imefaradhisha (kukubali) vita na wasio waislamu ikiwa watawanyanyasa na kuwatoa katika majumba yao. Lakini katika vita hivyo Mungu na Mtume wake wamesema haitakiwi kwa Muislamu kukata miti, kuchoma nyumba za ibada. (Tena hili hata Sheikh Basaleh imamu wa msikiti wa Mtoro ambae sikumsikia kushiriki vurugu zile, aliwahi kulizungumza kuwa Uislamu unaheshimu nyumba za ibada na haifai kuharibiwa hasa ikiwa wao hawajaharibu za kwenu). Sasa elimu hii ya kuchoma makanisa imetoka wapi?

Kitu cha pili katika kunajisiwa kitabu cha Mungu wa kweli (Quran), sikusikia kiongozi hata mmoja wa kanisa kutoa tamko la kudharau ama kuafiki kitendo kile. Sasa kuchoma makanisa ni kudhihirisha hasira kwa yule kijana mdogo ambae alishawishiwa na kijana mwenzie wa kiislamu ama ni hasira kwa ukristo?

Kitu kingine yule kijana alietoka na msahafu nyumbani kwao na kumuamuru rafiki yake aukojolee ambapo atageuka mnyama yeye yupo wapi? Maana kama ni makosa wametenda pamoja kutokana na utoto wao.

Hapa naomba nieleweke, siafiki hata kidogo kitendo kile, hata kingefanywa na motto mchanga basi ningekuwa upande wa wailsamu na si vinginevyo. Ila hatua zilizochukuliwa kutokana na kitendo kile ndizo zinazonitatiza.

Kuhusu tukio la pili la kuvamia kiwanja makosa ni ya BAKWATA, baraza la Waislamu Tanzania ambao kisheria wanatambulika na Serikali. Wao waliuza kiwanja kile ambacho kisheria kilikuwa Waqfu (Waqfu, ni mali yoyote ambayo inawachwa kuwa urithi kwa waislamu wa eneo ama nchi. Wapo Waislamu matajiri ambao wanakufa hawana ndugu, wanaamua mali zao wanazitoa kwa waislamu, hiyo ndiyo waqfu).

Ikiwa bakwata ndiwo waliouza kiwanja kile na mikataba ilishawekwa kisheria, haikutakiwa mtu msomi na mwenye uelewa wa mambo kama Sheikh Ponda kutenda mambo yale.

Ilitakiwa vurugu hizo akazifanyie bakwata ambae ndie alieuza, kwa maana tayari mali ile imeshakuwa ya mnunuaji, kumvamia ni kuingilia uhuru wa mtu. Anaweza kukuita jambazi ama mwizi na mahakama ikakuhukumu bila mwanasheria yoyote aliekubuhu kuweza kushinda kesi hiyo.

Kwasababu mnunuzji tayari alikuwa na hati na mikataba yote ya kuimiliki mali ile kisheria na kitaratibu tayari ni yak wake. Kumvamia ni uchokozi na kukosa busara.

Kosa la tatu ni pale Sheikh Ponda alipokamatwa halafu waislamu wakaanza kuishinikiza Serikali kumwachia kinguvu. Ni upuuzi kuingilia uhuru wa mahakama. Na huu ni ujanja mpya wa Serikali ya Tanzania. Wanapogundua wameteleza mahala haraka wanakimbilia mahakamani, hivyo kimsingi waislamu walishachelewa kuitaka serikali kumuachia sheikh wao, maana mtu amabe ameshasimama mahakamani hawezi kutolewa tena. Maana hata hiyo serikali haina uwezo kwani mahakama ni mhimili wa dola unaojitegemea.

Kosa la nne lililofanywa na waislamu ni pale waliposhindwa kuitumia nafasi pekee waliyokuwa nayo kuiduwaza serikali na vyombo vyake likiwemo jeshi la polisi.

Kamanda Suleiman Kova, mkuu wa jeshi la polisi kanda maalum Dar es Salaam, alitamka siku ya jumatano iliyopita kuwa mtu yeyote ambae anaona yupo chini ya Sheikh Ponda basi ajisalimishe haraka kwa jeshi la polisi. Misikiti yote jijini Dar es Salaam ilitangaza baada ya sala ya ijumaa kuwa watakwenda kujisalimisha kwa Kova.

Lakini cha ajabu asubuhi ya siku hiyo mambo yakabadilishwa na kusema wanakwenda ikulu kuonana na rais ilhali wengi walikuwa wakijua rais hayupo nchini alikuwa ziarani nchini Oman.Maana waliona wakienda kujisalimisha serikali haitawaandama kwa mabomu kwani mtu anaejisalimisha hatakiwi kupigwa. Na hapa ndipo ninapoamini waislamu wa Tanzania wanatumiwa na watu walio nje ya nchi kwa maslahi yao. Kwani watu wakiuwawa na jeshi la polisi ama kuumizwa kwao hiona ndiyo njia sahihi ya kuionyesha jamii kuwa wanaonewa.

Ningekuwa mshauri wa waislamu nchini ningewataka kusimamia msimamo wao uleule wa kuenda kujislaimisha kwa Kova. Jiulize Tanzania ina waislamu wangapi, sote tuamue Tanzania nzima tunakwenda kujisalimisha kwa kamanda Kova kwa amani bila vurugu. Unadhani Dar es Salaam itakalika? Wote wavae kanzu zao nyeupe huku wanataja jina la Mungu na Mtume wake kiutulivu bila ghasia. Hilo vipi?

Wakiulizwa mnataka nini, wajibu sisi ni wafuasi wa sheikh Ponda tumekuja kujisalimisha tunataka kupelekwa mahakamani. Nikitaja idadi ndogo tu ya waislamu Tanzania ambao wataunga mkono wazo hilo mathalan waislamu milioni kumi wajisalimishe, sidhani serikali itaweza kuwahudumia mahabusu milioni kumi wakati wakiendelea kusikiliza kesi yao. Lazima Sheikh Ponda angeachiwa huru tu hata kwa kupindisha sheria.

Tukiachana na hapa bara tuhamie Zanzibar, sheikh wa uamsho ana lake jambo. Maana sikubaliani na ukweli kuwa alitekwa maana jambo hili limefanyika kimaajabu sana hata wenye akili wameshaanza kubaini baadhi ya makosa ya kimkakati yaliyofanywa na kikundi hicho cha wanauamsho kwa uongo walioufanya kuwa ni kweli.

Haiwezekani mtu aliekamatwa kwa ajili ya mahojiano mazito kama hayo ya kuhujumu nchi halafu asirudi na alama hata ya kufinywa. Mimi si mwana usalama lakini wanausalama nawajua, hasa wanapokuwa na mtu mkaidi kama Sheikh Farid.

Sheikh huyo anasema siku ya tukio alipigiwa simu na mtu aliejitambulisha ni mwanafunzi wake, hakuwa akimjua wala kuwahi kuonanan na huyo mtu aliempigia simu. Kwa Sheikh wa kikundi kama uamsho kuenda sehemu aliyoitwa na mtu asiemfahamu tena bila ulinzi kwa kipindi hiki ambacho Tanzania alishatekwa kiongozi wa madaktari na kuteswa vibaya si jambo la kuingia akilini.

Na hata maelezo ya kutekwa kwake hayaingii akilini kwabisa. Maana anasema alipofika katika eneo la Mbweni karibu na msikitimdogousiotumika na watu wengi aliamua kushuka na kumwamuru dereva wake akanunue umeme, nae alikwenda msikitini kwa ajili ya haja ndogo.

Yaani ni kitu cha ajabu sana unamruhusu mtu wako wa karibu kuondoka eneo ambalo unakwenda kukutana na mtu ambae humjui, tena kwa dharura ndogo kama ya kununua umeme kitu ambacho ungekifanya hata wakati unarudi nyumbani.

Halafu kitu cha pili taarifa za kupotea Sheikh huyo zilisambaa haraka zikiambatana na vurugu za kuchoma na kuharibu maskani za CCM. Kwanini CCM?

CCM ni chama tu kama vyama vingine, CCM si serikali, kama hasira zao zilikuwa ni dhidi ya serikali kwanini hawakuchoma moto na kuharibu majumba ya chama cha wananchi CUF? Maana Zanzibar sasa inaongozwa na vyama viwili CCM na CUF ambapo inaitwa Serikali ya umoja wa kitaifa.

Halafu kupotea kwake kwanini kunasibishwe na kutekwa? Kwanini wasingefanya subira japo baada ya siku mbili ama tatu ndipo wakaanza kuonyesha hasira zao? Jibu ni rahisi, tayari wanauamsho walishakuwa na hofu ya kutekwa kiongozi wao siku yoyote, sasa kwanini Sheikh wao huyo hakuchukua hadhari mapema?

Hapa pana kitu kilitakiwa kifanyike, vurugu zilipangwa na hata kutekwa kwa sheikh huyo pia kulipangwa na ndiyo maana amerudi nyumbani bila mchubuko. Usifanye mchezo na chombo cha dola, wasingekubali kumshikilia mtu kwa siku nne halafu wamuachie akatoe siri za maswali aliyoulizwa.

Kamakweli wanataka kuitia ila serikali ya Dk Shein rais wa Zanzibar basi wasome historia za ukatili wa rais wa kwanza wan chi hiyo ambae alikuwa akimkamata mtu kinachopatikana ni mwili wake tena ukiwa mfu ama una kilema cha kudumu.
Naomba leo niishie hapa, lakini kichwa changu kina mambo mengi sana ya kuzungumza ambayo nimejifunza kutokana na wiki mbili hizi za vurugu. Waislam tumeingia do asana kwa kuonekana ni wakorofi na hatuna simile.

Mathalan, wapo waislamu amabao walitaka kuandamana mpaka ikulu ili kumsemarais kwanini amewapa pole wakristo na kuenda kutembelea makanisa yaliyoharibiwa huko mbagala.

Sijui kama hao waislamu wanajua walichokuwa wakikidai, jeshi la polisi lipo chini ya rais ambae ni muislamu pia. Tayari kijana alieidharau Quran alishafika mikononi mwake rais, hamkumpa muda afanye maamuzi mkaandamana mpaka kituo cha polisi kutaka kumpora kijana huyo ili mumuadhibu mnavyojua nyinyi, matokeo yake badala ya kutoa adhabu kwa muhalifu mkaamua kufanya uhalifu kwa kuharibu mali.

Ni rais wa aina gani atakaesimama mbele ya umma ambao yeye ni kiongozi abariki uhalifu na kukiukwa sheria za nchi? Sitaki kuamini kama wapo waislamu walitegemea baada ya wao kuvuruga amani na kuharibu mali asubuhi yake rais Kikwete angesimama na kusema ‘sawa sawa mmefanya kazi nzuri sana waislamu kwa kuharibu makanisa hawa wakristo ni washenzi sana’. Sijui labda akili yangu haijui kufikiri lakini laiti Kikwete angezungumza maneno hayo…..

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894   
22/10/2012

      

No comments:

Post a Comment