Tuesday, November 6, 2012

Msimu wa korosho umeanza....

 Makamu mwenyekiti bodi ya korosho na mbunge wa zamani wa jimbo la mchinga Mudhihiri Mudhihiri akizungumza na wanahabari katika ofisi za bodi hiyo leo asubuhi.



 Wanahabari wakisikiliza kwa makini maelezo ya Mudhihiri katika ofisi za bodi ya korosho nchini.



Hafidh Kido

Bodi ya korosho Tanzania imeamua kuzima maandamano ya wakulima wa korosho yaliyopangwa kufanyika leo baada ya wakulima hao kulalamika kukaa na mazao hayo bila ya serikali kuyanunua na hata walipojaribu kuyauza kwa njia wanazozijua wao walikamatwa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo asubuhi makamu mwenyekiti wa bodi hiyo mbunge wa zamani wa jimbo la Mchinga Mudhihiri Mudhihiri, amesema ingawa msimu wa ununuzi wa korosho ulifunguliwa mwezi wa tisa mwaka huu lakini vyama vinavyohusika na ununuzi wa zao hilo vilikosa mkopo kutoka katika mabenki hivyo kushindwa kukamilisha zoezi hilo.

“Msimu wa ununuzi wa korosho ulifunguliwa rasmi 20/09/2012 kwa vyama vya msingi kuanza kukusanya korosho kwa wakulima, kwa kawaida vyama hivi hupata mkopo kutoka katika mabenki ili kuwalipa malipo ya awali na baada ya kuziuza huwalipa malipo ya pili.

“lakini mwaka huu vyama vimechelewa kupata mikopo hivyo kuchelewa kukusanya korosho za wakulima kwa wakati muafaka, kuchelewa kuanza ununuzi wa korosho kumewaathiri sana wakulima hata sisi tunafahamu,” alisema Mudhihiri.

Aidha mnamo mwezi wa kumi na moja mwaka huu waziri wa kilimo, chakula na ushirika Christopher Chiza, aliitisha kikao maalum mjini Dodoma ili kujadili suala hili. Ambapo watu waliohudhuria kikao hicho ni bodi ya korosho, bodi ya leseni ya maghala, wizara ya viwanda na biashara, benki kuu na benki za CRDB, NMB, TIB pamoja na chama cha ushirika.

“Kikao kile kilijadili mambo kadha ikiwemo mkanganyiko wa bei dira, madeni ya msimu wa 2011/2012 na kutafuta suluhisho la matatizo yote, kulikuwa na mafanikio makubwa maana kikao kilifikia maazimio yafuatayo:- bei dira ibaki Tsh 1,200 kwa kilo ya korosho daraja la kwanza, na Tsh 960 kwa daraja la pili.

Ili kumpunguzia mkulima mzigo wa riba ya deni mabenki yatakopesha vyama vya msingi malipo ya awali kwa riba ya asilimia 50 badala ya asilimia 70 msimu uliopita. Tafsiri ya badiliko hili ni kuwa bei ya awali ya malipo kwa kilo ya korosho daraja la kwanza itashuka kutoka Tsh 800 mpaka Tsh 600. manufaa yake ni kuwa hakutakuwa na riba kwa malipo ya pili na  yale ya majaliwa,” aliainisha Mudhihiri.

Makamu mwenyekiti huyo wa bodi ya korosho nchini alieleza kwa mwaka huu wanatarajia kununua tani 160 za korosho kutoka kwa wakulima na kusisitiza kuwa zile korosho zilizokamatwa siku kadhaa zilizopita zilikuwa zinakwenda kuuzwa bila ya utaratibu hivyo serikali haiwezi kukubali kuendelea kupata hasara kama waliyoipata msimu uliopita ambapo walipoteza kodi zaidi ya bilioni 100.

Wiki kadhaa zilizopita wauzaji wa korosho kutoka wilaya ya Tandahimba mkoa wa Mtwara, baada ya kuona korosho zao hazinunuliwi waliamua kujikusanya na kuzisafirisha kutoka mashambani na kuenda kuzibangua Kibaha mkoa wa Pwani ambapo magari yao yalikamatwa maeneo ya Vikindu nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam yakiwa na tani 15 za korosho.

Akizungmzia sakata hilo mudhihiri alisema “Zile korosho tumeamua kuzikamata kwasababu zinatakiwa kuuzwa kwa mfumo wa mnada na si kwa njia ya kiholela kama walivyotaka wao. Zikiuzwa kiholela tutakosa kodi, na kutokana na kutofahamu tumezipima tumeona zimechanganywa daraja la kwanza na la pili.

“Hata unyevu ni 12, hivyo bado ni za hivi karibuni lakin tumeamua tutaziachia ikiwa tu watakubali kufuata taratibu za kuziuza kwa kutumia mnada. Tuna mpango wa kuanzisha viwanda vya ndani vya ubanguaji korosho ili tuache kupeleka korosho zetu India zikiwa ghafi.” 

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
kidojembe@gmail.com




No comments:

Post a Comment