Wednesday, November 14, 2012

Serikali: Hakuna tiba ya Ukimwi



Na Mwandishi Wetu
Serikali imetangaza vita na waganga wa kienyeji waliobandika mabango sehemu mbalimbali za nchi na watu wengine kuwa wanatibu ugonjwa wa Ukimwi.
Akizumgumza katika mkutano wa Tacaids uliofanyika jijini Dar es Salaam jana na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa mashirika ya dini, taasisi binafsi na watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu,  Paniel Lyimo, alisema mpaka sasa hakuna dawa ya ugonjwa huo.
Alisema dawa ikipatikana itatangazwa na serikali na kwamba wanajitangazia kufanya kazi hiyo ni kinyume cha taratibu na wanastahili kushughulikiwa.
Alisema sehemu kubwa ya Watanzania hawajaathirika na kushauri wajikinge na maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi (VVU).
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi (Nacopha), Vitalisi Makayula, alisema tatizo la dawa feki za Ukimwi ni njama ya watu wanaotaka kujipatia fedha lakini kisayansi tiba ya ugonjwa huo haijapatikana.
Alisema zaidi ya aina 60 ya dawa zilizopo ni za kupunguza makali ya Ukimwi na wataalamu wanaendelea na utafiti.
Aliongeza kuwa dawa hizo feki zinapotosha jamii na pia serikali hupata hasara kwani hutumia gharama kubwa kwa ajili ya kununua dawa  lakini watumiaji hukiuka kwa madai kuwa dawa ya Ukimwi imepatikana.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Tacaids, Dk. Fatma Mrisho alisema yapo makundi yanayopata maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi kwa kasi na kushauri kujikinga zaidi.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment