Thursday, November 8, 2012

Vipi miaka miine hii obama ataikumbuka Afrika?


Kuna baadhi ya wenyeji wa bara hili waliotegemea mengi zaidi kutoka kwa mwanawe mtu aliyekuwa akichunga mbuzi huko Magharibi mwa Kenya
Lakini Rais Barack Obama, katika muhula wake wa kwanza, alizuru Afrika mara moja tu, tena kama mpita njia, na kusema wazi kwamba hangekuwa anajihusisha kupita kiasi na maswala ya Afrika.
“Hatima ya Afrika iko mikononi mwa Waafrika wenyewe,” alisema huko Ghana, katika hotuba iliyodhihirisha wazi kwamba ushawishi wa Marekani unapungua katika bara ambalo sasa linafanya biashara zaidi na Uchina kuliko Marekani.
Kwa hivyo, ni mabadiliko yapi yatakayokuwepo katika muhula wa pili?
“Kama Kenya itafanya uchaguzi huru, basi Obama ataitembelea nchi hiyo.''
Swala hili la yeye kutokuwa na muda na Afrika, kwa sababu ya matukio mengine, halikutiwa mkazo katika uchaguzi ulioangazia maswala nyeti nchini Marekani na harakati za mapinduzi katika nchi za Kiarabu.
Akitoa hotuba yake baada ya kushinda, Bwana Obama aligusia tu “,muongo wa vita” na “watu walioko katika nchi za mbali… wanaoweka maisha yao hatarini ili tu kujadili masuala muhimu, na kupata nafasi, kama sisi, kupiga kura kama sisi tulivyopiga leo”
Hakuna “Kanuni za Obama”
Katika muhula wa kwanza, maswala yalilenga mizozo mikubwa iliyokuwa Ivory Coast, Somalia, Sudan and Sudan Kusini, na hata uchaguzi uliofanywa Zambia.
Kuna uwezekano kwamba mwanzo wa muhula wa pili atajishughulisha na masuala kama hayo: mikakati ya kimataifa kuwaondoa waasi wenye uhusiano na Al-Qaeda kutoka Mali kaskazini – kwa kutumia nguvu au mazungumzo, au yote mawili – na juhudi kuhakikisha kuwa Zimbabwe na Kenya hawatakuwa tena na michafuko baada ya uchaguzi, iliyoharibu chaguzi zao zilizopita.
Hadi sasa, hakujawa na ishara yoyote ya kuwepo kwa “Sera Kabambe ya Obama” kwa ajili ya Afrika. Labda hilo siyo jambo baya ukitilia maanani tofauti na masuala mengine kuhusu Afrika.


Bwana Obama kawaachia wengine watoe tahadhari kuhusu Uchina, nchi ambayo haijitoshelezi kirasilimali.
Lakini kuna uwezekano kwamba muhula wake wa pili utampa nafasi ya kujiondoa kutoka kwa mkakati wake wa “vita dhidi ya ugaidi” huko Mali na Somalia, na kuangazia maswala mapana zaidi – hususan biashara – jambo aliloligusia miaka mitatu iliyopita nchini Ghana.
Chanzo:BBC Swahili.

No comments:

Post a Comment