Sunday, January 6, 2013

John Mnyika mbunge wa Ubungo 'Chadema' ameshawasilisha mswada bungeni wa kuunda barasa la vijana..



SATURDAY, JANUARY 5, 2013

Nimewasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana


Jana tarehe 4 Januari 2012 niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge  taarifa ya muswada  binafsi wa Sheria ya kuunda Baraza la Taifa la Vijana (The National Youth Council Bill, 2013) kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (1) na Taarifa ya Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).

Nimechukua hatua hiyo kwa kuwa kwa miaka zaidi ya kumi Serikali imekuwa ikiahidi karibu kila mwaka bungeni kuwa itawasilisha muswada wa kuunda baraza la vijana la taifa lakini haijawahi kutekeleza ahadi hiyo; nimeamua kuitekeleza ahadi hiyo kwa kupeleka bungeni muswada binafsi wa kuunda baraza la vijana la taifa.

Katika taarifa hiyo ya muswada nimewasilisha madhumuni, sababu pamoja na nakala ya muswada wenyewe wa sheria  ya kuanzisha Baraza la Vijana la Taifa kwa madhumuni ya kuanzisha chombo cha kuwaratibu vijana  wa Tanzania katika kutekeleza shughuli zao kijamii, kuuchumi, kiutamaduni na kimichezo, na kuchagiza hali ya utambulisho wa Kitaifa wa pamoja na uzalendo.

Baraza litawawezesha vijana kukutana na kushughulikia masuala ya kisera na kisheria yanayogusa maslahi ya vijana kupitia njia mbalimbali kama zinavyopendekezwa katika muswada huo katika ngazi na maeneo mbalimbali nchini ikiwemo katika kitaifa, kiwilaya, kikata na kivijiji/kimitaa.

Muswada pia utawezesha vijana kuwa na mfuko wa fedha ambazo kwazo vijana wataweza kutekeleza shughuli hili kufikia malengo ya Baraza ikiwemo ya kuwezesha utekelezaji wa sera ya taifa ya maendeleo ya vijana.

Muswada huo umegawanyika katika sehemu nane kama ifuatavyo: Sehemu ya Kwanza ya muswada huu inatoa utangulizi kwa kutamka jina la sheria na mipaka ya sheria na tafsiri za maneno yanayotumika kwenye muswada.

Sehemu ya Pili ya muswada huo inapendekeza kuundwa kwa Baraza la Vijana, kazi na majukumu yake, na zaidi kuanzisha nafasi ya mwenyekiti wa Baraza.

Sehemu ya Tatu ya muswada huo inapendekeza kuundwa kwa Bunge la Baraza, Bodi ya Baraza na Bodi ya Washauri wa chama kama sehemu Baraza pamoja na vyombo vingine.

Sehemu ya Nne ya muswada huo inapendekeza kuazishwa mfuko wa fedha wa Baraza kwa madhumuni ya kuwezesha utekelezaji wa kazi za Baraza kama zilivyoainishwa kwenye muswada.

Sehemu ya Tano, ya muswada huo inapendekeza kuundwa kwa sekretarieti kwa madhumuni ya kuwa watekelezaji wa shughuli za siku kwa siku za Baraza.

Sehemu ya Sita, ya muswada huo inapendekeza kuanzishwa kwa Majukwaa ya Vijana katika ngazi ya Halmashauri, na Kamati za Vijana za Kata, Vijiji na Mitaa kwa madhumuni ya kuzishusha chini shughuli za vijana kwenye ngazi ya chini kabisa.

Sehemu ya Saba, ya muswada inapendekeza kusajili asasi na taasisi shiriki za Baraza zinazoongozwa na vijana na vigezo vitakavyotumika kusajili asasi na taasisi hizo.

Sehemu ya Nane, ya muswada inapendekeza kuanzishwa kwa siku na juma la vijana, na zaidi inampa nguvu waziri kutunga kanuni kwa uendeshaji bora wa shughuli za Baraza.

Itakumbukwa hata kabla kuwa mbunge kwa nyakati mbalimbali nimeungana na vijana wengine kwa zaidi ya miaka kumi kutaka kuundwe Baraza la Taifa la Maendeleo ya Vijana kwa lengo la kuwaunganisha vijana bila kujali tofauti zao zingine katika kushughulikia vipaumbele mbalimbali vya vijana ikiwemo katika masuala ya elimu, ajira, afya, michezo na maisha ya vijana kwa ujumla.
Baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge niliungana na wabunge wengine kuhoji bungeni na serikali iliahidi kwamba mchakato wa kuundwa kwa baraza hilo ungekamilika katika mwaka wa fedha 2011/2012, hata hivyo mpaka kipindi hicho kinamalizika mwezi Juni 2012 na kuanza kwa mwaka mwingine wa fedha 2012/2013 ahadi hiyo haijatekelezwa.

Wenu katika uwakilishi wa wananchi,

John Mnyika
Mbunge wa Jimbo la Ubungo
05 Januari 2012

No comments:

Post a Comment