Thursday, January 10, 2013

Ujasiriliamali ni mambo manne mtaji, ubunifu, fursa na mawasiliano

                         Tunalazimisha furaha ili tuendelee kuishi.


Na Hafidh Kido

Kuna siku nilikuwa nikitembelea mijadala katika mitandao ya kijamii, nikakuta mada kuhusu ujasiriamali. Mchangiaji mmoja aliuliza swali juu ya ujasiriamali unataka vigezo gani. Alitaka kujua ujasiriamali ni pesa au nia ya dhati ndipo mtu apate mafanikio.

Baada ya kutafakari kwa muda mrefu nimeona ujasiriamali unahitaji mambo manne katika mengi ambayo watu wengi wanayatumia kupata mafanikio. Mtaji, ubunifu, fursa na mawasiliano.

Kwa nchi zinazoendelea tatizo kubwa ni ukosefu wa rasilimali za kutosha, kwa Tanzania si rasilimazi za kutosha tu bali ni matumizi mabaya ya rasilimali tulizonazo ima kwa kuwapa wageni ama kushindwa kuzizalisha kwa faida ya wote.

Hili hushusha pato la taifa na kufanya ajira kuwa chache kwani mashirika ya umma na binafsi yanashindwa kuajiri kwa kasi kinachotakiwa kutokana na pato dogo wanalopata katika huduma wanazotoa ama bidhaa wanazouza.

Baada ya kuona hilo Serikali iliamua kuanzisha mpango wa kupunguza na kuondoa umsikini Tanzania (MKUKUTA) na Visiwani wakaanzisha (MKUZA).

Lakini mpaka sasa imepita miaka mingi bado mipango hiyo haijazaa matunda wala kuonyesha mafanikio yoyote zaidi ya uongeza vitambi kwa wakuu wa miradi.

Miaka ya hivi karibuni kumeingia dhana mpya ya maendeleo katika jamii kwa kuzuka neno ‘ujasiriamali’ lakini watu wengi ima hawaifahamu dhana hii ama wanaielewa vibaya.

Kwa mtu anaetaka kuwa mjasiriamali kitu pekee anachotakiwa kuwa nacho ni maarifa ya biashara; baada ya hapo ndipo yanapokuja masuala ya mazingira ya biashara, mwelekeo wa uchumi katika nchi, sheria na masuala ya fedha za kigeni.

Aidha katika mambo manne niliyoyataja hapo juu yaani Mtaji, Ubunifu, Fursa na Mawasiliano kuwa ndiyo uhai wa mjasiriamali katika shuguli za kila siku, ufafanuzi wake ni huu.

Mtaji
Tukianza na mtaji katika ujasiriamali hiki ndicho kitu cha kwanza mtu anaetaka kuwa mjasiriamali kupasa kuwa nacho. Unaweza kuwa mtaji wa fedha, fikra ama matarajio makubwa katika shughuli zako.

Maana bila mtaji huwezi kuanza kitu chochote, lazima uwe na kitu kitakachoweka uhai. Fedha ni kitu cha pili baada ya nia na umadhubuti wa kusimamia kile utakachokianzisha.

Watu wengi wanashindwa kuendeleza shughuli za kijasiriamali kwa kuamini fedha ndiyo mtaji pekee kwa biashara ama huduma ya kijasiriamali.

Mawasiliano
Hapa mjasiriamali anapasa kuwa na mawasiliano mengi kadiri awezavyo, na mawasiliano yenyewe ni kwa wateja wapya na wa zamani, wapinzani na washirika katika biashara na serikali.

Mjasiriamali ambae anatumia muda mwingi kuwasiliana na watu anakuwa na nafasi kubwa ya kujiweka sawa ama kukabiliana na changamoto anazokutana nazo katika shughuli zake.

Lazima ujue kuhusu mabadiliko ya bei za bidhaa katika mataifa makubwa, ujue kuhusu sera za Serikali kuhusiana na biashara unazofanya ama mawasiliano na wateja wako wa kila siku na wale wapya kujua wanataka nini na hawataki nini katika biashara mnayofanya, maana biashara ni maelewano.

Ubunifu
Katika vitu vinavyowashinda watu wengi katika biashara ni kuwa wabunifu, wajasiriamali huamini baada ya biashara kusimama basi kila kitu kinakwenda sawa.

Lakini hakuna kitu hatari kama kumchosha mteja wako kwa kuona kitu kilekile kwako. Ni vema kubadilikabadilika ili kuendelea kumpa hamu mteja wako na hata kumvutia mteja ambae alikuwa hapendezwi na mfumo ama mwonekano wa zamani katika eneo lako la bishara.

Unaweza kushusha bei katika msimu wa sikukuu, ama kubadili nembo ya biashara yako kila baada ya mwaka mmoja ama wakati maalum hasa nyakati ambazo zinawagusa wateja wako wa imani fulani ama kundi maalum la watu.

Fursa
Hiki ni kitu ambacho watu wengi wanakikosa katika harakati za ujasiriamali, na sababu kubwa ni rushwa na kujuana.

Wapo watu ambao wanapewa kandarasi ambazo hawaziwezi ama wanashinda zabuni ambazo hawana uwezo nazo. Lakini zote hizi ni fursa ambazo mjasiriamali anahitaji kuwa nazo ili aweze kufika mbali katika shuguli zake.

Lakini hakuna kilichoharibika ikiwa utakosa fursa kwasababu hutoi rushwa ama hujulikani. Maana waswahili husema chema kinajiuza na kibaya kinajitembeza, onyesha juhudi katika kazi zako watu watakufuata ili kutaka huduma zako, maana mbali ya mambo kuendeshwa kwa kujuana lakini watu wanapenda ufanisi katika kazi na si kubebana.

Hivyo ni vema mtu anapopata nafasi ya kufanya kazi basi afanye hivyo kwa kiwango cha juu ili walio pembeni yake ama washindani wake waone tofauti kati yao na yako.

Faida na hasara za kuajiriwa

Kwa sasa watu wengi wanafikiria kuacha kazi ili kujiajiri, ama utakuta asilimia kubwa ya watu walioajiriwa serikalini na sekta binafsi pembeni utakuta wana biashara ndogondogo wanazofanya ili kuwakimu. Kwa maana mishahara haitoshi kwa kila mtu.

Wataalam wa uchumi duniani walipiga hesabu ndogo inayoonyesha ni namna gani mwajiriwa hawezi kutimiza malengo yake ikiwa hatakuwa na biashara pembeni.

Taarifa zinasema zaidi ya asilimia 90 ya wafanyakazi duniani hawajui njia nzuri ya kutafuta pesa, watu wengi wanatumia kiasi kikubwa cha pesa kutafuta faida tofauti na kiasi wanachorudisha.
 Tuanatumia nguvu nyingi sana kubuni miradi lakini hatufanyi utafiti ni namna gani miradi hiyo itaweza kudumu.


Wajasiriamali wengi hufanya biashara za kupata kula ya siku moja tu. Elimu inahitajika sana.


Matokeo yake wanatumia maisha yao yote kutafuta pesa ambazo hawafanikiwi kuzipata ila wanawazalishia waajiri wao bila kujijua. Mbaya zaidi waajiri hao hawajali masilahi ya wafanyakazi waliowazalishia zaidi ya kuwalipa mishahara ambayo kimsingi haiwafai chochote.

Kwa mfano, ikiwa umeajiriwa na unafanya kazi kwa saa nane kwa siku, siku tano katika wiki na wiki 50 katika mwaka; maana yake utakuwa unafanya kazi saa 2,000 kwa mwaka.

Kwa mshahara wa kitanzania mtu anaelipwa mshahara wa juu ni milioni moja, maana yake kwa mwaka atakuwa anaingiza milioni 12, ambayo ameisotea kwa saa 2,000.

Sasa tujiulize kwa pamoja, ikiwa utaamua kuwa mjasiriamali unafanya shughuli zako mwenyewe kwa mikono yako kwa saa hizo 2,000 kwa mwaka ambazo ni sehemu ya saa 9125 kwa mwaka. Tumepiga hesabu ndogo ya saa 24 kwa siku zidisha siku 365 za mwaka.

Utakuwa unaingiza kiasi gani kwa jasho lako mwenyewe kwa saa zote hizo, na utakuwa na uhakika wa kupumzika muda unaotaka na kufanya kazi kwa muda unaotaka kikubwa ni nidhamu ya kazi. Tofauti na waajiri ambao hawajali umefiwa, unaumwa ama umechoka.

Hivyo tunakubaliana kwa pamoja kuwa suluhisho la umaskini katika nchi zinazoendelea ni ujasiriamali uliotukuka.

HAFIDH KIDO
kidojembe@gmail.com
0713 593894
10/1/2013
Dar es Salaam, Tanzania

No comments:

Post a Comment