Tuesday, February 19, 2013

Balozi wa Tanzania Ubelgiji awa kiongozi wa mabalozi nchini humo.



Balozi Joel M Nheleko wa Swaziland nchini Ubeligiji, ambaye alikuwa Rais wa Mabalozi wa Afrika nchini Ubeligiji aliyemaliza muda wake, akimkabidhi Balozi wa Tanzania Dk. Diodorus Kamala mfuko wenye vitendea kazi kama ishara ya kumkabidhi Urais wa Mabalozi wa Afrika Ubeligiji jijini Brussels juzi. (Na Mpiga Picha Wetu)



BRUSSELS, Ubeligiji 

Balozi wa Tanzania nchini Ubeligiji, Dk. Diodorus Kamala ameteuliwa na mabalozi wa nchi za Africa wanaoziwakilisha nchi zao nchini humo kuwa Mwenyekiti wao.

Balozi Kamala amepokea uenyekiti huo kutoka kwa Balozi wa Swaziland nchini Ubeligiji, Joel Nheleko aliyemaliza muda wake. Tanzania itashikilia kiti hicho kwa muda wa miezi sita hadi Julai 1, 2013.

“Nimefurahi kupewa heshima hii, na naamini nitaitumia fursa hii kufahamiana vizuri na mabalozi wenzangu na kuvutia fursa za kiuchumi kwa nchi yetu,” alisema Balozi Kamala.

Wakati huo huo, juzi mabalozi wa nchi tano zinazozunguka Bonde la Ziwa Tanganyika, walimchagua Balozi Kamala kuwa mwenyekiti wao.

Nchi wanachama wa Bonde la Ziwa Tanganyika ni Burundi, Rwanda, Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Zambia.

Nchi hizi zimeunganisha nguvu kutafuta wafadhili kwa ajili ya maendeleo ya Bonde la Ziwa Tanganyika, ambapo eneo la bonde hili lenye wakazi wastani wa milioni 40 wanalenga kuliendeleza kwa ajili ya kujenga miundombinu, kurahisisha usafiri na usafirishaji, kujenga reli mpya na kuendeleza utalii.

Chini ya mpango huu wanalenga pia kuboresha viwanja vya ndege vya nchi wanachama vya Mbala, Kalemie, Bujumbura, Kigoma na Kasanga kwa nia ya kurahisisha usafiri wa anga katika ukanda huu.

Dk. Kamala amekabidhiwa jukumu la kuratibu mpango huu na kwa pamoja watatafuta fedha kutoka kwa wafadhili kwa ajili ya mradi huu.
Chnazo: Habari mseto blog. 



No comments:

Post a Comment