Friday, March 1, 2013

CAG agundua madudu Tanesco.


                                Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za Serikali Ludovick Utouh.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh amesema uchunguzi alioufanya dhidi ya vigogo watatu wa Shirika la Ugavi wa Umeme (Tanesco), unaonyesha kuwa kuna madudu ya kutisha.

Utouh alisema hivi karibuni kuwa alijikita zaidi katika mikataba yenye thamani ya zaidi ya Sh500 milioni iliyoingiwa na shirika hilo.

Awali, Ofisi ya CAG ilitoa ripoti ambayo ilisababisha aliyekuwa Mkurugenzi wa Tanesco, William Mhando kusimamishwa na baadaye kufukuzwa.

Vigogo wengine waliotajwa katika ripoti hiyo, Robert Shemhilu, Ofisa Mkuu wa Fedha, Lusekelo Kassanga na Meneja Mwandamizi Ununuzi, Harun Mattambo walisimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazowakabili ikiwa ni pamoja na kuingia mikataba mibovu wakati wa ununuzi wa mali za shirika.

Utouh alisema ripoti hiyo imejaa madudu, jambo ambalo lilisababisha kutumia nguvu kubwa wakati wa ukusanyaji wa taarifa zake.

Alisema baada ya kugundua madudu hayo, walilazimika kuzunguka kwenye ofisi za shirika hilo zilizoko mikoani ili waweze kuhoji baadhi ya wafanyakazi na kukagua mikataba hiyo.
Alisema kutokana na hali hiyo, walitumia nguvu kubwa wakati wa ukusanyaji wa taarifa zake, jambo ambao lilisababisha kuchukua muda wa miezi mitatu ili kukamilisha.

“Tumefanya kazi kubwa sana katika ripoti hii ya awamu ya pili. Hii inatokana na kutakiwa kukagua mikataba iliyoingiwa na Tanesco ya miradi mikubwa, jambo ambalo lilisababisha kwenda hadi kwenye ofisi za mikoa ili kuhoji na kuchunguza mikataba hiyo,” alisema Utouh.

Alisema baada ya kubaini madudu hayo walitoa mapendekezo yao ambayo Serikali inapaswa kuyafanyia kazi ili waweze kutenda haki pindi wanapotoa uamuzi kuhusu tuhuma zinazowakabili viongozi hao.

Alisema kutokana na hali hiyo wamekabidhi ripoti hiyo tangu Januari mwaka huu kwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Jenerali Robert Mboma ili aipitie na kuiwasilisha kwenye mamlaka nyingine husika.
Mboma alikiri kupokea ripoti hiyo na kudai kuwa wanaanza kuwahoji watuhumiwa hao wiki jayo.
 Chanzo: Mwananchi.

No comments:

Post a Comment