Sunday, March 17, 2013

Coastal Union waendelea kuwa ving'ang'anizi nafasi ya nne ligi kuu Tanzania bara.

 Kocha mkuu wa Mtibwa Sugar Mecky Mexime wa kwanza kulia akitabasamu wakati timu yake ikipambana na Coastal Union ya Tanga jana jumamosi ambapo walitoka suluhu 1-1 uwanja wa Manungu Turiani.

 Wachezaji wa coastal Union wakipiga jaramba kabla ya kuanza mechi yao dhidi ya Mtibwa Sugar jana.

Mchezo unaopokolea halafu jua linakunyima utamu inabidi utumie akili ya ziada kufaidi soka.


Jana kigoma cha wagosi wa kaya kimerejea mjini Tanga kutoka Manungu Turiani Mkoa wa Morogoro kikiwa na shangwe baada ya kupata suluhu ya 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar katika mechi ya ligi kuu ya vodacom Tanzania Bara.

Coastal Union ilikuwa ya kwanza kuliona lango la Mtibwa Sugar dakika nne tu baada ya mwamuzi kupuliza kipyenga cha kuashiria mchezo huo wa jana uliojaa kukamiana kuwa umeanza katika uwanja wa Manungu ndani ya mashamba ya miwa na kiwanda cha sukari.

Ibrahim Twaha ‘Messi’ jana alifunga goli la kwanza tangu aanze kucheza ligi kuu, ambapo aliunganisha krosi nzuri iliyochongwa kiustadi na Joseph Mahundi na kumlazimisha golikipa wa timu ya Taifa Hussein Sharrif ‘Cassilas’ kushindwa kudhibiti shuti hafifu lililopigwa na ‘Messi’ na kuishia kuumalizia kwa mkono wa kushoto mpira ule ukaingia wavuni.

Baadae Mtibwa walibadilika wakaanza kushambulia kwa kasi kiasi Kocha wa Coastal Union Hemed Morroco akawa hakai kitini kila mara anainuka kuwafokea wachezaji wake. Ingawa mpaka timu zinakwenda mapumziko matokeo ilikuwa ni 1-0.

Hata hivyo kipindi cha pili kilipoanza Mtibwa waliingia kwa ari kubwa kiasi kufika dakika ya 67 ya mchezo Vicent Barnabas alivuruga furaha ya wapenzi wa Coastal Union walioandamana na timu mpaka Manungu baada ya kusawazisha bao kiubwete kwani mpira ulimgonga mguuni na kutinga wavuni wakati mabeki wa Coastal Union walipokuwa katika harakati za kuokoa hatari iliyodumu langoni mwao kwa dakika moja na nusu, hivyo kubadilisha matokeo na kusomeka 1-1.

Baada ya hapo Mtibwa walishambulia kwa kasi mpaka mwamuzi anapuliza kipyenga cha mwisho dakika ya 90 matokeo yalibaki 1-1 lakini wagosi wa kaya walikuwa katika hali mbaya sana.

Kudhihirisha hilo wakati wagosi wa kaya wana kona tatu Mtibwa Sugar walikuwa na kona 12 mpaka mpira unaisha. Na zote zilikuwa kona hatari kama si umahiri wa Shaaban Kado golikipa namba moja wa Coastal Union alietokea hapohapo Mtibwa Sugar leo habari zingekuwa nyingine.

Kikosi cha kwanza kilichoanza jana Coastal Union ni: Shaaban Kado, Ismail suma, Othman Tamim, Philip Mugenzi, Mbwana Kibacha, Razak Khalfan, Castro Mumbala, Danny Lyanga, Joseph Mahundi, Gabriel Barbosa na Ibwahim Twaha.

Baadae kocha akafanya mabadiliko akaingia Nzara Ndaro akatoka Castro Mumbala, akaingia Abdi Banda akatoka Razak Khalfan halafu akaingia Mohammed Miraji akatoka Gabriel Barbosa.

Mtibwa Sugar walikuwa ni: Hussein Sharrif, Said Mkopi, Isasa Issa, Rajab Mohammed, Ally Lundenga, Babu Seif, Jamal Mnyate, Rashid Kombo, Hussein Javu, Ayub Isiko na Vicent Barnabas.

Kwa matokeo hayo Coastal Union wataendelea kubaki nafasi ya nne kwa pont 32 wakati Mtibwa watabaki nafasi ya tano kwa point hizohizo 32 huku Kagera Sugar wakishika nafasi ya sita wakiwa na point 31.

Ili wagosi wa kaya wawe na amani katika nafasi hiyo ni lazima waombe mabaya kwa Kagera Sugar kwenye mechi yao tarehe 27 March, uwanja wa nyumbani Kaitaba mjini Bukoba ambapo wanashuka na Simba SC.

Mechi nyingine ya Coastal Union itachezwa jumamosi ijayo jijini Dar es Salaam dhidi ya African Lyon inayotishia kushuka daraja.

HAFIDH KIDO
kidojembe@gmail.com
Turiani, Morogoro
17 March, 2013 

No comments:

Post a Comment