Friday, March 8, 2013

Hali tete uchaguzi Kenya, Raila agomea matokeo ya baadhi ya majimb


HALI imeanza kuwa tete nchini Kenya baada ya Chama cha Muungano wa Cord kinachoongozwa na Raila Odinga kutaka shughuli ya kuhesabu kura za urais kusitishwa mara moja na kimetishia kwenda mahakamani kusitisha mpango huo.

Wakati hali ikiwa hivyo, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), imeendelea kutoa matokeo ya mwisho ya kura hizo kwa majimbo huku ikipanga kutangaza matokeo kamili ya uchaguzi wa rais leo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mgombea Mwenza wa Raila, Kalonzo Musyoka alisema Cord ina wasiwasi kwamba kumekuwa na ukiukwaji wa taratibu na amesema kuna hisia za hujuma katika mchakato wa kuhesabu kura unaoendelea.

Musyoka alisema Cord inataka shughuli hiyo ya kuhesabu kura za urais isitishwe mara moja na kuanzishwa upya kwa kutumia stakabadhi kutoka kwa makarani wa kura jambo ambalo imeelezwa kwamba ndilo linalofanyika kwa sasa.

Alisema pia kuwa muungano huo una tashwishi kuhusu baadhi ya matokeo akisema si ya kweli kwa kuwa hayawiani na yale ambayo mawakala wao waliyowasilisha.
Alisema baadhi ya matokeo yako juu kuliko idadi ya wapiga kura katika baadhi ya maeneo ambako kura zilipigwa.

Alisisitiza kuwa tatizo hilo limetokana na kugoma kwa mitambo ya kupiga kura na pia kuanza upya kwa shughuli ya kuhesabu kura kwa kutumia mfumo wa zamani.

Musyoka alisema Tume ya Uchaguzi inastahili kutumia mitambo ya elektroniki kuhesabu kura kama inavyoagiza katiba ya nchi, huku akisisitiza kuwa muungano huo ungali unatafakari hatua za kuchukua ikiwamo kufuata sheria.
Hali ya taharuki imeanza kutanda katika maeneo mbalimbali ya Kenya baada ya IEBC kuendelea kuyakalia matokeo ya urais ikiwa ni zaidi ya saa 48 tangu Wakenya walipopiga kura.

Shughuli hiyo imekumbwa na utata hasa baada ya mitambo ya kuhesabia kura ya Tume ya Uchaguzi kukumbwa na hitilafu.

Hatua hiyo imeilazimu tume hiyo kuanza kuhesabu kura upya katika kituo cha kupokea matokeo ya kura za urais kwenye Ukumbi wa Bomas, Nairobi.

Uhuru aendelea kuongoza
Mgombea wa urais kupitia Muungano Jubilee, Uhuru Kenyatta hadi kufikia saa 11:00 jioni jana, alikuwa anaongoza kwa kura 2,660,379 huku mpinzani wake, Raila akimfuatiwa kwa kura 1,996, 181.

IEBC ilisitisha utumiaji wa mitambo ya kielektroniki kuhesabu kura kutokana na hitilafu na kusababisha zoezi hilo kubadilika na kura kuhesabiwa kwa njia ya kawaida.
Ingawa utaratibu wa kuhesabu ulikuwa unakwenda kwa mwendo wa kinyonga, bado Kenyatta alikuwa mbele.

Katika hatua nyingine, wanasiasa wa vyama vya Jubilee na Cord, walifukuzwa katika kituo cha kutangaza matokeo cha Bomas baada ya kutaka kuingilia kazi ya Tume ya Uchaguzi.
 Wanasiasa hao walianza kupiga kelele wakitaka matokeo ya jumla yatangazwe jambo lililowafanya viongozi wa IEBC, kuwafukuza katika eneo hilo.
Chanzo: Gazeti Mwananchi

No comments:

Post a Comment