Wednesday, March 13, 2013

Kadinali Jorge Mario Bergoglio wa Argentina amechaguliwa kuwa Papa mpya wa Kanisa Katoliki.



Kadinali Bergoglio anakuwa mtu wa kwanza kutoka Amerika kusini kuchaguliwa kuwa Papa.
Mara tu baada ya kuchaguliwa alichagua jina la Papa Francis I.
Awali moshi mweupe ulishuhudiwa ukifuka kutoka bomba la kutolea moshi katika kanisa la Sistine Chapel na kufuatiwa na kengele kupigwa. Hii ilikuwa ni ishara kwa walimwengu kuwa makadinali ambao walianza mchakato wa kumchagua Papa mpya hatimae walikuwa wamefaulu katika kazi yao.
Kadinali Bergoglio anachukuwa mahali pa Papa Benedict XVI, ambaye alijiuzulu mwezi uliopita akisema hana nguvu na uwezo wa kuendelea kuliongoza Kanisa Katoliki.
Makadinali 115 wamekuwa faraghani tangu siku ya Jumanne alasiri na wakaanza mchakato wao kwa kupiga kura mara nne kwa siku.
Ilikuwa inahitajika kuwa angalau Makadinali 77 yaani theluthi-mbili wangeliweza kumpigia kura mmoja wao ili aweze kutangazwa kuwa Papa mpya.
Na kabla ya mchakato huo kuanza kulikuwa hakuna dalili za kuonyesha nani angelichaguliwa.

Maelfu ya watu kutoka sehemu mbali mbali duniani walikwa wamekusanyika katika ukumbi wa Kanisa la St Peter tangu siku ya Jumanne.
Muda mfupi kabla ya Kadinali Bergoglio kujitokeza , maelfu ya watu walionekana wakikimbia kuelekea ukumbi wa St Peters ili kuweza kumshuhudia Papa mpya akitangazwa .

Papa Francis I ni nani?

Alizaliwa Mjini Buenos Aires huko Argentina mwaka1936.
Papa Francis 1 ni mtu wa kwanza katika kipindi cha miaka elfu moja (1,000) kwa mtu kutoka nje ya bara la Ulaya kutawazwa kuwa papa wa Kanisa Katoliki.
Papa Francis 1 ni mwana wa Mtaliano aliyekuwa akifanya kazi katika shirika la gari Moshi kabla ya kuhamia nchini Argentina miaka ya zamani.
Kama kadinali wa Jimbo la Buenos Aires ,Kadinali Bergoglio amekuwa mkosoaji mkubwa wa serikali ya Argentina.
Hata hivyo Kadinali Bergoglio anapendwa sana na wafuasi wa kanisa hilo huko Argentina na hasa watu maskini.
adinali Jorge Bergoglio, mwenye umri wa mwaka 76, kwa karibu miaka yake yote kama Kasisi amehudumu nyumbani kwao Argentina.
Kadinali huyo wa Jimbo la Buenos Aires inasemekana aliibuka nambari mbili wakati Papa Benedict alipochaguliwa mwaka 2005
Anaaminika kuwa na ujuzi mkubwa ambao wengi wanasema utamsaidia sana katika uongozi wake.
Katika maisha yake ya huduma kwa Kanisa Katoliki huko Amerika Kusini ambapo Kanisa Katoliki lina waumini wengi zaidi duniani, Kadinali Bergoglio ameibuka kuwa mtu anayependa sana udhabiti wa kisiasa katika nchi zilizo katika bara la Amerika Kusini.
Bergoglio anasifiwa kwa kuleta mageuzi makubwa katika Kanisa la Argentina huku katika eneo hilo la Amerika Kusini Kanisa bado linashikilia itikadi za kale.
Chanzo: BBC Swahili.

No comments:

Post a Comment