Tuesday, March 5, 2013

Shehe Ponda Issa Ponda ana kesi ya kujibu.


HAKIMU Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam, Victoria Nongwa amesema Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda na wenzake 49 wana kesi ya kujibu kwa mashtaka yote matano yanayowakabili.
Sheikh Ponda na wenzake hao wanakabiliwa na mashtaka matano, likiwamo la kula njama, wizi wa mali yenye thamani ya Sh59.6 milioni, uchochezi na kuingia  katika ardhi inayomilikiwa na Kampuni ya Agritanza Limited kwa nia ya kujimilikisha visivyo halali.
Akitangaza uamuzi huo, Hakimu Nongwa alisema: “Mahakama imepitia ushahidi uliotolewa na mashahidi 17 wa upande wa mashtaka... inaonekana wazi shauri hili linatokana na kipande cha ardhi.”
Kiongozi huyo na wenzake wanatarajiwa kuanza kujitetea Jumatano na Alhamisi.
Hakimu Nongwa alieleza kuwa baada ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), kubadilisha ardhi ya ekari nne zilizopo Chang’ombe Markazi na 40 za Kampuni ya Agritanza Ltd zilizopo Kisarawe, kuna baadhi ya Waislamu hawakuridhika.
Alisema Mahakama haitaujadili kwa undani ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka, bali itawapa nafasi upande wa utetezi kujitetea... “Kila mshtakiwa anatakiwa aseme alikuwa anatafuta nini katika maeneo yale ya Chang’ombe Markazi.,”
Alisema kabla ya Sheikh Ponda na wenzake kuanza  kujitetea, Wakili wao Juma Nassor anatakiwa apeleke vielelezo watakavyovitumia na kueleza watatoa utetezi kwa njia ya kiapo ama la.
Katika kesi hiyo, Sheikh Ponda, Saleh Mukadam na wenzao 48, wanakabiliwa na mashtaka manne, likiwamo la wizi wa mali yenye thamani ya Sh59.6 milioni.
Mbali na mashtaka hayo, pia Ponda na Mukadam wanakabiliwa na shtaka la uchochezi ikidaiwa kuwa kati ya Oktoba 12 na 16, mwaka huu katika eneo la Chang’ombe  Markazi, wakiwa viongozi wa Taasisi na Jumuiya za Kiislamu Tanzania, waliwashawishi wafuasi wao kutenda makosa hayo.
Akisoma hati ya mashtaka, Wakili Mwandamizi wa Serikali, Tumaini Kweka alisema Oktoba 12, mwaka huu katika eneo hilo lililopo Wilaya ya Temeke, kwa jinai na pasipo sababu za msingi walivamia ardhi inayomilikiwa na Kampuni ya Agritanza Ltd kwa nia ya kujimilikisha isivyo halali.
Kweka alidai kuwa washtakiwa hao walitenda kosa hilo la kuingia kwa nguvu kwa nia ya kutenda kosa, kinyume na Kifungu cha 85 na 35 cha Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Alidai kuwa kati ya Oktoba 21 na 16, mwaka huu katika eneo hilohilo, washtakiwa hao pasipo uhalali wowote na hali iliyosababisha uvunjifu wa amani, walijimilikisha ardhi hiyo mali ya Agritanza Limited.
Aidha Hakimu Nongwa alisema washtakiwa hao wanadaiwa kuiba vifaa na malighafi mbalimbali za ujenzi, yakiwamo matofali 1500, tani 36 za kokoto na nondo vyote vikiwa na thamani ya Sh 59,650,000, mali ya Kampuni ya Agritanza Ltd, kati ya Oktoba 12 na 16.
Awali, baada ya washtakiwa hao kusomewa mashtaka  yanayowakabili kwa nyakati tofauti, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) aliwasilisha hati za kuzuia dhamana zao chini ya Kifungu cha 148 (4) cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai (CPA).
Mara ya kwanza kesi hiyo ilifika Mahakama ya Kisutu Oktoba 18 na tangu wakati huo ilikuwa ikisikiliza mashahidi upande wa utetezi na kabla ya kufikia uamuzi huo.
Chanzo: Mwananchi.

No comments:

Post a Comment