Monday, March 4, 2013

Siku si nyingi moshi mweupe utatoka Vatican na Papa mpya atatangazwa....


MAKARDINALI wa Kanisa Katoliki kutoka sehemu mbalimbali duniani, leo wanaanza maandalizi ya kumchagua mrithi wa Papa Benedict XVI, aliyeachia ngazi wiki kiliyopita.
Kwa mujibu wa tovuti ya Vatican City, ilieleza kuwa mkutano mkuu wa Makardinali utaanza leo saa 3.00 asubuhi kwa saa za Vatican (Saa 6.00 mchana kwa saa za Tanzania) kwenye Ukumbi wa New Synod Hall.
Mkutano huo ndio utafungua mchakato wa uchaguzi wa Papa mpya na unatarajiwa kuandaa ratiba ya uteuzi wa papa mpya.
Makardinali hao ndio watapanga siku ya kufanyika mkusanyiko wao unaoitwa `Papal Conclave' kwa ajili kufanya uchaguzi huo.
Papa anavyochaguliwa
Kwa kawaida uchaguzi wa Papa hutakiwa kufanyika siku 15 hadi 20 wakati nafasi hiyo itakapokuwa wazi na Uchaguzi kwa kawaida hufanyika katika Kanisa la Sistine Chapel.
Uchaguzi wa Papa unatarajiwa kuhusisha makardinali 115 kutoka nchi mbalimbali duniani. Kati ya hao, makardinali 67 waliteuliwa na Papa Benedict, ambaye jina lake kamili ni Joseph Aloisius Ratzinger.
Wakati mkutano unaendelea utakuwa unatoka moshi mweusi ndani ya mkutano huo kuashiria papa hajapatikana.
Siku utakapoonekana moshi mweupe ukitoka kwenye kanisa basi ndio itakuwa ishara kuwa papa mpya amechaguliwa.
Papa Benedict aburudika na kinandaMkurugenzi wa Habari wa Vatican, Padri Federico Lombardi, alisema Papa Benedict, ambaye ni mzaliwa wa Ujerumani, amekuwa akijiburudisha kwa kupiga kinanda.
“Tumezungumza wasaidizi wa Papa na wametuleleza Papa amekuwa na mapumziko mazuri na amekuwa akitumia muda mwingi kuimba nyimbo za dini huku akipiga kinanda,” aliongeza.
Pia Papa, ambaye ni mzaliwa wa Ujerumani amekuwa akitumia muda mwingine kusoma vitabu na meseji za kumtakia kila la heri kutoka sehemu mbalimbali duniani.
Ni nadra kwa Papa kujiuzulu na mara ya mwisho kabla ya Benedict kuachia ngazi ilitokea miaka 600 iliyopita.

No comments:

Post a Comment