Wednesday, March 13, 2013

Wanawake hawakuruhusiwa kuimba Taarab Zanzibar


Mama Sitti Bint Saad akipiga tari, ala aliyoipenda sana na kumudu kuipiga kiustadi wakati wa uhai wake.


 Na Hafidh Kido

WANAUME wengi wanaojishughulisha na Muziki wa Taarab maarufu ‘Mipasho’ huonekana wamepotea kwa kuchagua burudani inayopendwa na kinamama.

Muziki wa Taarab umechangia kuongezeka kwa misamiati mingi katika miji ya pwani hasa Dar es Salaam, Tanga na Zanzibar ambapo kinadada huitumia kunogesha mazungumzo wenyewe huita ‘kupashana.’

Lakini wengi hawafahamu kuwa Muziki wa Taarab ulipofika pwani ya Afrika Mashariki katika karne ya 19 mjini Unguja wanawake hawakuruhusiwa kuimba, kupiga vyombo wala kucheza muziki huo.

Alieleta burudani hii katika Afrika Mashariki ni Sultan Seyyid Baraghash Bin Said ambae alitawala Zanzibar (1870-1888).

Alikuwa akipenda sana Muziki huu akawa anaagiza vikundi kutoka Misri ambapo wanaume tu ndiwo walikuwa wakiimba na kupiga ala zote katika jumba la burudani Beit El-Ajaib.

Mzanzibari wa kwanza kuonyesha uwezo wa kuimba Taarab alikuwa ni Mohammed Ibrahim, ambapo Sultani aliagiza apelekwe Misri ili akajifunze kupiga ala na uimbaji ili akiweza awafundishe wengine na kupunguza gharama za kuagiza vikundi kutoka nje.

Ibrahim, alipokuwa Misri alijifunza kupiga chombo cha Kanuni ama ‘Ganuni’ ambacho ni chombo kigumu kuliko vyote kwenye Muziki wa Taarab, ni mfano wa kinanda chenye nyuzi za chuma, mpaka sasa ni watu wachache sana wanaojua kucheza chobo hicho.

Baadae Mohammed Ibrahim alipowafunza Wazanzibari wengine kuimba na kupiga vyombo vya Taarab wakaamua kuanzisha kikundi cha kwanza cha Taarab Afrika Mashariki kilichitwa ‘Zanzibar Taarab Orchestra’ baadae kikaitwa (Cultural Musical Club) mpaka sasa kipo na kinatumika kama chuo cha Taarab mjini Unguja.

Baadae mwaka 1905 kikundi cha pili cha Nadi Ikhwani Swafaa kikaanzishwa. Ikawa ukoo wa kisultani haupati gharama tena ya kuagiza vikundi kutoka Misri, kumbuka wakati wote huo wanaume ndiwo waliokuwa na ruhusa ya kuimba na kupiga vyombo vya Taarab.

Miaka ya 1920 mwanamke wa kwanza Afrika Mashariki kakata minyororo ya utumwa na kupaza sauti kwa uimbaji Taarab alikuwa ni Bi Mtumwa Saad maarufu Sitti Bint Saad. Na wakati huo Taarab ilikuwa ikiimbwa kwa lugha ya kiarabu, ila Kiswahili kilitumika kwa kiasi kidogo.

Hata hivyo, mashairi yaliandikwa kwa hati za kiarabu ingawa yalisomeka kwa Kiswahili. Hii ilikuwa kasumba ya waarabu kwani iliaminika asili ya Muziki huo ni lugha ya kiarabu hivyo kutumia lugha nyingine ilikuwa ni kama kuupunguzia ladha.

Zingatia, wakati wote huo Taarab ilikuwa ikitumika kuwaburudisha mabwanyenye wa kiarabu ‘ukoo wa kisultani’. Ulitumbuizwa katika kasri la Sultani tu haukuruhusiwa kupigwa mitaani, yaani haukutumika kwa kupata kipato kama inavyofanyika sasa.

Sitti Bint Saad huyohuyo ndie mtu wa kwanza kutoka Afrika Mashariki kurekodi sauti yake akiimba Taarab nchini India katika Studio maarufu kwa wakati huo ‘His Master’s voice’, ingawa vipo vitabu vingine vinaandika ilikuwa ni kampuni ya ‘Columbia Records’.

Mpaka sasa jina la Sitti Bint Saad aliefariki June 1950 halisahauliki midomoni mwa  wapenzi wa Taarab kwani ndie aliewakomboa wanawake mpaka sasa Taarab ikiimbwa na wanaume inaonekana ajabu.

HAFIDH KIDO
13 March, 2013
Dar es Salaam, Tanzania


No comments:

Post a Comment