Sunday, April 14, 2013

Asprini inasababisha kuvuja damu tumboni...



Siyo watu wengi wanapendelea kutumia Aspirin kwa ajili ya kutuliza maumivu kama ilivyo kwa Panadol na Diclopar au diclofenac.Pamoja na mazingira hayo, kuna wanaoitumia bila kujua, kupitia dawa nyingine zilizochanganywa na paracetamol pamoja na caffeine.
Dawa hizo ni kama vile Headex, Mifupen, Action ama dakika tatu. Zote hizo ni mchanganyiko wa dawa kadhaa, asprini ikiwa ni miongoni.
Dawa hizi kwa sasa zinapatikana hadi kwenye maduka ya vyakula na hazina udhibiti wowote kwani hata machinga anaweza kuzijumuisha kwenye bidhaa anazouza.
Kama nilivyoeleza awali, matumizi holela ya dawa hizi za kutuliza maumivu yamekithiri, hivyo baadhi hutembea nazo mifukoni au kwenye pochi.
Watu wa namna hii huwa hawatibu chanzo cha matatizo yao, bali wanatumia dawa hizo ili kujipa ahueni ya maumivu ambayo ni dalili tu ya yale yanayowasumbua.
Leo katika kuzungumzia Aspirin nimezungumza na Mtaalamu wa Dawa nchini, Mfamasia Mildred Kinyawa.
Kinyawa ambaye ni Msajili wa Baraza la Wafamasia Tanzania anaanza kwa kueleza:
“Kwa jumla, kitu chochote kikishaitwa dawa ni muhimu kutumiwa kwa uangalifu. Hakuna dawa isiyo na kiwango fulani cha madhara kwa mtumiaji. Pia hiyo ni mbaya zaidi kwa wale wanaotumia kiholela.”
Anasema kuwa kitaalamu Aspirin ni dawa nzuri kuliko dawa nyingine za kutuliza maumivu kwa sababu huweza kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja.
Anabainisha kuwa kama ilivyo paracetamol, Aspirin inaweza kutuliza maumivu madogomadogo kama vile kuumwa kichwa, mafua na kushusha homa.
Kinyawa anafafanua kwamba, tofauti na Paracetamol, Aspirin inaweza kutuliza maumivu makali kama vile ya mifupa, meno na hata kutibu uvimbe.
Faida nyingine za Aspirin ni kwamba huweza kumsaidia mtu asipate matatizo ya moyo au kiharusi kutokana na damu kuganda na kuziba mishipa ya damu.
Anaeleza kuwa Aspirin huweza kuyeyusha vipande vidogovidogo vya damu iliyoganda na kujikuta ikiendelea kusafirishwa kwenye mfumo wa damu.
Kinyawa anaielezea damu iliyoiganda kuwa inaweza kuziba mirija kwenye moyo au ubongo na kusababisha madhara makubwa ikiwamo kifo cha ghafla.
Athari za Aspirin
Mfamasia huyo anasema kwamba kwa namna ilivyotengenezwa, Asprin ina asili ya aside, hivyo inapotumiwa wakati tumbo likiwa wazi hukwangua tumbo na kumsababishia vidonda tumboni.
Kwa watu wenye matatizo ya vidonda vya tumbo, hushauriwa kutokutumia kabisa asprini kwa sababu huchangia kuongeza tatizo.
Tafiti nyingine ambazo zimewahi kufanywa na kuandikwa kwenye majarida mbalimbali ya afya duniani zinaonyesha kuwa mtu akitumia aspirin na pombe anaweza kusababisha damu kuvuja tumboni kiasi cha kuhatarisha maisha yake.
Utafiti uliofanywa mwaka 2009, ulibaini kwamba matumizi mabaya ya Aspirin kutibu mafua makali kwenye kipindi cha mwaka 1918-19 ilisababisha athari mbalimbali zikiwamo za mapafu kujaa maji, vifo na udhaifu wa mwili kushambuliwa na bakteria pamoja na virusi.
Utafiti huo ulisababisha matumizi ya Aspirin kupungua na hata kupendekezwa isitumike kwa watoto chini ya miaka 16.
Inafanyaje kazi?
Aspirin inafanya kazi kwa kupunguza uzalishaji wa kemikali inayojulikana kama prostaglandin ambayo kwa kawaida husababisha maumivu.
Mara nyingi Aspirin inapendekezwa kutumiwa na watu wazima na mtumiaji awe ameshakula au kutumia wakati anakula.
Wiki ijayo nitamalizia mada hii kwa kuelezea juu ya Diclopar na Diclofenac.
Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment