Friday, April 19, 2013

Mwamuzi pambano la Cheka na Mashali apatikana.


NA: ONESMO NGOWI
Shirikishoi la Ngumi la Kimataifa (IBF) limeteua mwamuzi na majaji wa pambano la kutetea ubingwa wa Afrika kati ya anayeushukilia ubingwa huo Francis Cheka wa Tanzania na mpinzani wake Thomas Mashali ambaye ni bingwa wa uzito wa Middle ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (ECAPBA).

Mwamuzi  wa mpambano huo wa kukata na shoka atakuwa ni John Shipanuka kutoka nchini Zambia mbaye alilisimamia pambano kati ya Francis Cheka na Mada Maugo mwaka jana kwa ustadi mkubwa. Shipanuka ni Afisa Ugavi katika jeshi la Jamhuri ya Watu wa Zambia na ana ujuzi mkubwa wa kusimamia mapambano ya ngumi ya kimataifa.

Aidha, majaji wa mpambano huo ni Daudi Chikwanje kutoka Malawi ambaye ndiye Katibu Mkuu wa Chama Cha Ngumi Cha Malawi na ambaye anakuwa jaji namba moja. Steve Okumu wa Kenya ambaye anakuwa jaji namba mbili na Ismail Sekisambu wa Uganda ambaye anakuwa jaji namba tatu. Msimamizi mkuu wa mpambano huo ni Rais wa IBF katika bara la Afrika, Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati Mtanzania Onesmo Ngowi.

 Hata hivyo Ngowi amemwagiza Mwenyekiti wa Kamati ya Viwango  na Ushindi wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Nchini (TPBC) Boniface Wambura amshikie nafasi hiyo ili Ngowi apate nafasi nzuri ya kusimamia mapambano matatu ambayo ni (la ubingwa wa Dunia kwa vijana,, lingine la ubingwa wa mabara kwa wanawake na lingine ubingwa wa Afrika) yatakayofanyika nchini Ghana tarehe 3 mwezi Mei.

 Nayo Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa nchini TPBC imeshateua maofisa watakaosimamia mapambano ya awali pamoja na kutoa kibali kwa kampuni ya Mumask Investment and Gebby ili iendeshe mpambano huo!

 Hii ni mara ya pili kwa bondia Francis Cheka kutetea ubingwa wake tangu amsambaratishe kwa TKO bondia machachari Mada Maugo katika mpambano uliofanyika mwaka jana mwezi wa Aprili katika ukumbi wa PTA jijini Dar Es Salaam.
<

No comments:

Post a Comment