Thursday, May 30, 2013

NAMNA MIKOA YA MTWARA NA LINDI INAVYONUFAIKA NA UTAFUTAJI NA UENDELEZAJI WA GESI ASILIA

SHIRIKA LA MAENDELEO YA PETROLI TANZANIA



1.0 UTANGULIZI
Gesi asilia iligunduliwa kwa mara ya kwanza hapa nchini Mwaka 1974 kwenye Kisiwa cha Songo Songo, Mkoani Lindi. Ugunduzi mwingine umefanyiaka katika maeneo ya Mtwara Vijijini (Mnazi Bay-1982 na Ntorya-2012), Mkuranga (Pwani, 2007) na Kiliwani (Lindi, 2008). Kiasi cha gesi asilia iliyogunduliwa katika maeneo haya inakadiriwa kuwa futi za ujazo trilioni 8. Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kumekuwa na kasi kubwa ya utafutaji mafuta na gesi asilia uliojikita zaidi kwenye maji ya kina kirefu cha bahari. Kiasi cha gesi asilia iliyogunduliwa katika kina kirefu cha maji ni takribani futi za ujazo trilioni 33.7. Jumla ya gesi asilia iliyogunduliwa nchi kavu na baharini inafikia takribani futi za ujazo trilioni 41.7.
Rasilimali hii ya gesi asilia inaweza kutumika katika maeneo mbalimbali yakiwemo; kuzalisha umeme, malighali ya kuzalishia mbolea na kemikali, nishati viwandani, majumbuni na kwenye taasisi mbali mbali. Pia gesi asilia inatumika kama nishati ya kuendeshea magari.



FAIDA YA GESI ASILIA MKOA WA LINDI
1. Mradi wa gesi asilia wa Songo Songo- LINDI
(i) Kodi ya Huduma (Service Levy):
Songo Songo huzalisha gesi asilia takribani futi za ujazo milioni 102 kwa siku na kuletwa Dar es Salaam kwa ajili ya kufua umeme na kutumika viwandani. Kufuatana na kodi ya huduma (Service levy) Halmashauri ya Lindi inapata asilimia 0.3 ya mauzo ya gesi hiyo. Toka mwaka 2004 wakati mradi wa Songo Songo Songo ulipoanza kuzalisha gesi hadi kufikia mwisho wa 2012, Halmashauri imepata jumla ya Shs. 885 milioni. Wastani wa mapato kwa kila miezi mitatu ni Shillingi 110 millioni.

(ii) Umeme:
§ Wananchi wa Kisiwa cha Songo Songo hupata umeme wa uhakika na bure.
§ Mara tu Bomba la Gesi litokalo Songo Songo likifika nchi kavu sehemu ya Somanga Fungu, Serikali imefunga mitambo ya kufua umeme. Umeme unaofuliwa Somanga Fungu ni MW 7.5 unaotumika ni takribani MW 2.5. Umeme huu wa ziada unatoa fursa kwa viwanda kujengwa katika mkoa wa Lindi.

(iii) Maji Safi:
§ Mradi unatoa maji safi kwa wakazi wa Songo Songo kwa kuhudumia kisima cha Kijiji.

(iv) Huduma za jamii:
§ Kila mwaka wanafunzi kumi bora waliofaulu wanafadhiliwa na mradi kwenda shule ya Sekondari ya Makongo. Wanafunzi hawa wanaofaulu vizuri watafadhiliwa hadi vyuo vikuu.
§ PanAfrican (PAT) wamejenga Shule ya chekechea Songo Songo na watoto wanahudumiwa na kampuni hiyo.
§ PAT wamepeleka waalimu wawili wa chekechea katika mafunzo ya muda mrefu.
§ Zahanati ya Songo Songo imekarabatiwa na kuongeza baadhi ya vifaa.
§ Bweni la wasichana limejengwa na kuikarabati Shule ya Sekondari ya Songo Songo.
§ Ajira hutolewa kwa wakazi wa kijiji cha Songo Songo.
Huduma hizi za jamii zimegahrimiwa kwa kiasi cha Shilingi milioni 730 ($455,000) kwa kipindi cha 2004 hadi Desemba 2012.

2. Manufa kutokana Kampuni ya Maurel and Prom.
Katika shughuli za utafutaji mafuta Kampuni hii imejenga barabara ya kudumu ya kilometa 15 kutoka Somangafungu hadi Kinjumbi. Aidha Kampuni pia imejenga zahanati kwa ajili ya Kijiji cha Kinjumbi.

3. Manufaa kutokana na Kampuni ya Statoil
Wamepeleka wawakilishi wa wananchi wa Mkoa wa Lindi kwenye ziara ya mafunzo ya Mitambo ya Kusindika Gesi Asilia (LNG) nchini Norway.

4. Wizara ya Nishati na Madini.
Mwaka huu wa Fedha Wizara ya Nishati na Madini imefadhili wanafunzi 55 katika Chuo cha VETA Lindi kwenye fani mbali mbali za ufundi.

5. Kiwanda cha Mbolea Mkoani Lindi.
Serikali inafanya majadiliano na Kampuni kadhaa zilizoonyesha nia kutaka kujenga Kiwanda cha Mbolea Mkoani Lindi. Mazungumzo yatakamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu.

FAIDA KWA MKOA WA MTWARA
1. Kodi ya Huduma na Umeme.
Gesi asilia iliyopo Mnazi Bay ilianza kutumika mwishoni mwa mwaka 2006 kwa kuzalisha umeme wa uhakika unaotumika mjini Mtwara. Uwezo wa mitambo iliyofungwa mjini Mtwara ni MW 18 lakini uzalishaji wake kutokana na mahitaji ni MW 12. Halmashauri ya Mtwara Vijiji hupata kodi ya Huduma (Service Levy) ya asilimia 0.3 ya mauzo gesi hiyo. Kwa wastani Halmashauri hupata Shilingi milioni 16 kwa mwaka. Kiasi hiki ni kidogo kutokana na uzalishaji na uuzaji mdogo wa gesi ingawa uwezo wa kuzalisha gesi kwenye visima vyote vinne vilivyopo Mnazi Bay kufikia futi za ujazo milioni 130 kwa siku upo. Kuanzia mwaka 2006, Mkoa wa Mtwara wanapata umeme wa uhakika unaozalishwa kutokana na gesi asilia ya Mnazi Bay.

1. Mafunzo
Mwaka 2010, Kampuni ya Petrobrass wametumia $350,000 (sawa na Shilingi 560 milioni) kufundisha na kuleta vifaa VETA Mtwara. Wanafunzi 50 (wakufunzi 2) walifundishwa kwenye fani ya umeme na makanika. Aidha, Kampuni ya BG wameendesha pia mafunzo na VETA – Mtwara mwaka 2012 kwenye fani za English language, food preparation, plumbing, welding, carpentry, motor vehicle, electrical installation and maintenance.

Katika Mwaka wa Fedha 2012/13, Wizara ya Nishati na Madini imetoa ufadhili wa wanafunzi 50 kusoma Chuo cha VETA – Mtwara.

2. Huduma za Jamii:
Kampuni ya BG imetumia jumla ya Dola za Marekani 557,028 sawa na Shilingi 891 milioni katika yafuatayo:
§ Kukarabati majengo ya shule za sekondari Mkoani Lindi
§ Madawati 600 yalisambazwa kwa shule za msingi Wilayani Mtwara Mjini.
§ Mafunzo ya Usalama Barabarani kwa shule za msingi katika Mkoa wa Mtwara – wanafunzi 14,611 wamefaidika
§ Usalama Barabarani katika Mkoa wa Mtwara – kwa wapanda Pikipiki
§ Kukarabati Maktaba ya Shule ya Sekondari ya Wasichana Mtwara
§ Hifadhi ya fukwe za bahari na (marine park) na Aga Khan Msimbati.
§ kukarabati shule za sekondari, kutoa elimu ya usalama barabarani kwa shule za msingi na mafunzo kwa madereva wa boda boda.
Kampuni ya Wentworth Resources inayofanya utafiti na uendelezaji wa Mnazi Bay nayo imetumia Dola za Marekani 551,333 sawa na Shilingi milioni 882 katika huduma zifuatazo:
§ kusambaza maji kwa shule za Mnolela na Msimbati, Mtwara Vijijini.
§ wamesambaza umeme kwenye shule ya Mnolela,
§ Wamejenga jengo la utawala, mabweni, madarasa matano, nyumba za waalimu, jiko, jengo la kulia chakula na vyoo kwenye shule ya Mnolela Kijiji cha Ruhokwe.
§ Wametoa vitanda na magodoro kwa shule hii.
§ wamejenga mabweni ya wasichana,
§ kujenga, ufadhili wa masomo na michezo na kukarabati shule mbalimbali.
§ Uchimbaji visima vya maji kwa ajili ya Kijiji cha Mnete, ukarabati barabara za vijiji, ujenzi wa darasa moja kwa ajili ya Shule ya Msingi Msimbati na uwanja wa mpira wa miguu kwa Shule ya msingi Msimbati.
§ Ajira kwa wanavijiji 10 kutoka kijiji cha Msimbati kwa ajili ya kutengeneza boti na kwa Mwaka 2013 kukarabati majengo ya shule ya Sekondari ya Msimbati.
§ Januari 2013 mchango kwa ajili Mafuriko.

Kampuni ya Dominion kwenye huduma za jamii imechangia Dola za Marekani 82,000 sawa Shilingi milioni 131 kama ifuatavyo:
§ Kuanzia 2007 hadi 2010, vijiji kumi vya Mandawa na Kisangire, vilipewa kila kimoja Shs. 5 milioni kwa ajili ya ukarabati majengo ya utawala, mabweni ya shule na kliniki. Jumla Shs. 50 milioni zilitumika.
§ Mwaka 2010 na 2011 Kampuni ilitumia shs. 10 milioni kwa ajili ya kutoa elimu kuhusu hifadhi ya viumbe bahari kwa wanavijiji wa vijiji vya mwambao.
§ Mwaka 2011 na 2012 Kampuni ilitoa msaada wa $ 22,000 (sawa na Tsh. 35 milioni) kwa Chuo cha mambo ya Bahari kwa ajili ya masomo ya shahada za uzamivu kwa wanafunzi wawili kutoka Mtwara.

Kampuni ya Ophir East Africa Ventures Ltd - Tsh 34,000,000
§ Mwaka 2011 Kampuni ilisaidia Watawa wa Benedictine kwa ajili ya Dispensary/Clinic ya Shangani.
§ Mwaka 2012 Kampuni ilisaidia Shs. 16,000,000 kwa Watawa wa Benedictine kwa ajili ya Dispensary/Clinic ya Shangani.

3. Utafutaji wa Mafuta na Gesi kwenye Kina Kirefu Cha Bahari
Shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia katika kina kirefu cha bahari zinaendelea na zimeleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Mikoa ya kusini. Kati ya manufaa hayo ni:
• Ajira
Uanzishwaji wa eneo la kupokelea vifaa vya utafutaji wa mafuta na gesi asilia, Mtwara Supply Base kwenye Bandari ya Mtwara na uchimbaji wa gesi baharini umeajiri wafanyakazi wengi katika kada mbalimbali kama vile udereva, uboharia, waendesha mitambo na ufundi mbalimbali;
• Eneo la huduma za utafutaji wa mafuta na gesi asilia (Oil Field Supply Hub) lilianzishwa Mwaka 2010 ndani ya Bandari ya Mtwara, mahususi kwa ajili ya kuhifadhi vifaa vya utafutaji na uchorongaji wa visima vya mafuta na gesi katika kina kirefu cha bahari. Katika kutekeleza hili faida zifuatazo zimepatikana:
§ Bandari ya Mtwara imekarabatiwa;
§ Shughuli za Bandari zimeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka kuhudumia usafirishaji wa korosho tu na kuwa kitovu cha ugunduzi wa gesi yote kwenye kina kirefu cha maji baharini;
§ Bandari ya Mtwara sasa imekuwa chimbuko kubwa la ajira kwa watu wa Mtwara;
§ Bandari ya Mtwara imekuwa yenye ufanisi wa hali ya juu, yenye gharama nafuu na ya kisasa.

3. Kiwanda cha Saruji cha Dangote.
Kiwanda kitakuwa kinazalisha saruji kwa kutumia nishati ya gesi asilia ya Mnazi Bay. Kiwanda kimekwishaanza kujengwa na kinategemewa kukamilika ndani ya miaka miwili. Kiwanda kitakuwa kikubwa kuliko chochote Kusini mwa Sahara, ambacho kitazalisha tani 3,000 kwa siku. Kiwanda kitakapokamilika kitatoa faida zifuatazo:

• Ajira rasmi kwa wananchi takribani 500 na zile zisizo rasmi takribani watu 800;
• Kitakuza uchumi wa wananchi wa Mikoa ya Kusini pamoja na Watanzania kwa ujumla; na
• Saruji itakayozalishwa itasafirishwa kwa kutumia meli na barabara, hivyo kuongeza shughuli za Bandari ya Mtwara.

4. Karakana ya Kifundi ya Schlumberger.
Kampuni ya Schlumberger ambayo hutoa huduma kwa kampuni za utafutaji mafuta na gesi imejenga karakana kubwa na ya kisasa mjini Mtwara kwa ajili ya kuhudumia utafutaji wa mafuta na gesi nchini, Msumbiji, Kenya, Uganda na Afrika kusini. Karakana hii imekamilika na inategemewa kuajiri wafanyaka takriban 100.

5. Mitambo ya kusafishia gesi asilia
Ili kuhakikisha ajira na faida nyinginezo zinabaki maeneo ambayo gesi inazalishwa, Serikali imeamua mitambo ya kusafisha gesi ijengwe maeneo yanayozalishwa gesi hiyo.

Kwa hivi sasa, Serikali kwa kupitia TPDC inajenga mitambo ya kusafisha gesi katika Kijiji cha Madimba Wilaya ya Mtwara Vijijini yenye uwezo wa wa kusafisha futi za ujazo milioni 210 kwa siku. Vilevile inajenga mitambo mingine katika kijiji cha Songo Songo mkoani Lindi yenye uwezo wa kusafisha futi za ujazo milioni 140 kwa siku. Mitambo itakapo kamilika itatoa fursa zifuatazo:

• Fursa ya ajira kwa wastani wa wafanyakazi sitini (60) kwa Mtwara na sitini (60) kwa ule wa Songo Songo (Lindi);
• Pia itatoa ajira zisizo rasmi kwa wananchi watakao toa huduma kwa wataalam kama vile chakula, afya, elimu, maji, usafiri pamoja na huduma nyingine za kijamii zitakazo hitajika;
• Kutajengwa mitambo ya kusafishia maji ambapo vijiji vilivyo maeneo ya jirani vitapatiwa maji safi. Hadi sasa tayari Mkandarasi ameshakamilisha uchimbaji wa visima vya maji eneo la Madimba vyenye uwezo wa kuzalisha mita za ujazo mia moja na hamsini (150) kwa saa (150m3/hr). Sehemu ya maji hayo yatatumika katika mtambo wa kusafishia gesi na sehemu nyingine itahudumia wana kijiji.

6. Ujenzi wa Mitambo ya Liquefied Natural Gas (LNG)

Ugunduzi wa gesi asilia katika kina kirefu cha bahari kimepelekea Serikali pamoja na Makampuni ya utafutaji kuamua kuwekeza katika uzalishaji wa LNG. Mitambo ya LNG itajengwa nchi kavu kwenye Mikoa ya Lindi na Mtwara.

7. Ujenzi wa Kiwanda cha Mbolea (Urea)

Kwa kuzingatia sera ya kilimo kwanza, Serikali inatarajia kujenga kiwanda cha Mbolea kwa kutumia gesi asilia katika Ukanda wa Mikoa ya Kusini. Hadi sasa Serikali inafanya mazungumzo na Makampuni mbalimbali ambayo yameonesha nia ya kuwekeza katika mradi huu. Kampuni nyingi zimeonesha nia ya kujenga kiwanda cha mbolea Mtwara kwa kutumia gesi asilia ya Mnazi Bay. Kiasi cha mtaji unaohitajika kwa ujenzi wa mtambo wenye uwezo wa kuzalisha tani 3,800 za mbolea (Urea) ni takribani Dola za Marekani bilioni 1.7. Kiwanda hiki kitatumia kiasi cha gesi ipatayo futi za ujazo milioni 60 kwa siku.
Eneo la Mnazi Bay lina kiasi kikubwa cha gesi asilia ya kutumika katika viwanda mbali mbali vikiwemo vya mbolea. Kiwanda cha Mbolea kitakapokamilika kitatoa faida zifuatazo:

• Ajira kwa wananchi. Kwa kiwanda kitachotumia chenye uwezo wa kuzalisha tani 3200 kwa siku kitaajiri wastani ya watu 400 kwa ajira rasmi na ajira 1,600 zisizo rasmi;
• Kitakuza uchumi wa wananchi wa mikoa ya kusini pamoja na Watanzania kwa ujumla;
• Kutokana na mbolea kuzalishwa hapa nchini, ni wazi kuwa pembejeo hii itapatikana kwa bei nafuu na hivyo kuongeza kipato kitokanacho na kilimo; na
• Mbolea itakayozalishwa itasafirishwa kwa kutumia meli na barabara, hivyo kuongeza shughuli za bandari ya Mtwara.

8. Ujenzi wa Kiwanda cha Amonia

Wawekezajiwengi wameonesha nia ya kujenga kiwanda cha kuzalisha Amonia kwa kutumia gesi asilia ya Mnazi Bay. Kiwanda kinakadiriwa kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 3,000 za Amonia kwa siku na kitagharimu takribani Bilioni 1.6 dola za marekani na kitatumia gesi asilia kiasi cha fut iza ujazo milioni 160 kwa siku.Kiwanda hiki kitakapo jengwa kitatoa ajira kwa watu wapatao 400 kwa ajira rasmi na zaidi ya watu 1,500 kwa ajira zisizo rasmi.

9. Mitambo ya kuzalisha umeme

Mradi wa kuzalisha umeme upatao Megawati 400 utatekelezwa kama sehemu ya upanuzi wa mitambo iliyopo sasa huko Mtwara. Katika kutekeleza wa mradi huu, Serikali kwa kupitia Tanesco, imeingia ubia na Kampuni ya Symbion kuweka mitambo ya kuzalisha umeme mjini Mtwara kutokana na gesi asilia ya Mnazi Bay.

Pamoja na Mikoa ya Mtwara na Lindi umeme utakaozalishwa unatazamiwa kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa na pia utasambazwa katika Wilaya za Newala, Namtumbo, Mbinga, Songea pamoja na sehemu nyinginezo.

10. Ujenzi wa Kiwanda cha Methanol

Wawekezaji mbali mbali wa viwanda vya Kemikali wanataka kujenga Kdiwanda cha kuzalisha Methanol kwa kutumia gesi asilia. Kiwanda hiki kinatarajiwa kiwe na uwezo wa kuzalisha tani 5,000 za methanol kwa siku na kitagharimu Bilioni 1.7 Dola za Marekani na kitatumia gesi asilia kiasi cha futi za ujazo milioni 180 kwa siku. Kiwanda kitakapo jengwa kitatoa ajira kwa watu wapatao 400 kwa ajira rasmi na zaidi ya watu 1,500 kwa ajira zisizo rasmi.

11. Uanzishwaji wa Ukanda huru wa Bandari (Free Port Zone)

Ili kuhakikisha sekta ya uchimbaji wa mafuta inafanikiwa ni muhimu kwa serikali kuandaa mazingira yatakayovutia makampuni yanayotoa huduma na yanayouza malighafi na vitendea kazi kwenye sekta hiyo. Aidha, ili kutengeneza hayo mazingira kuwa mazuri kwa makampuni ya huduma, malighafi na vitendea kazi, serikali imetenga eneo maalum ndani ya Bandari ya Mtwara ambalo litawekewa miundombinu ya msingi na kutoa vivutio mbali mbali kwa makampuni hayo. Eneo hilo litapewa hadhi ya Ukanda Huru wa Bandari (Freeport Zone). Huduma za shughuli za utafutaji na uzalishaji wa gesi na mafuta nchini zitapatikana Mtwara badala ya kwenda nje ya nchi kutafuta huduma hizo. Hii itaongeza ajira kwa wakazi wa maeneo ya Kusini na kukuza uchumi.

Faida za Ukanda Huru wa Bandari (Freeport Zone) ni kama zifuatazo:
• Kuvutia uwekezaji wa kigeni;
• Kukuza makusanyo ya mapato ya serikali kupitia kodi ya mapato (Corporate Tax), ushuru wa forodha na VAT pale ambapo bidhaa zitaingizwa ndani ya nchi, PAYE na tozo za bandarini (Port Charges);
• Kukuza makusanyo ya mapato ya fedha za kigeni kupitia bidhaa zitakazouzwa nje ya nchi kwa kuwa eneo hili litakuwa kama kiunganishi (hub) cha Afrika Mashariki na Kati;
• Kukuza ajira;
• Kukuza biashara za kimataifa;
• Kukuza uchumi wa nchi; na
• Kukuza na Kuboresha uwezo wa kiteknolojia.

Kwa taarifa zaidi na ufafanuzi wasiliana na:
Mkurugenzi Mtendaji
Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania
S.L.P 2774
Simu: 2200103/4 & 2200112
Fax: 2200113
Dar es Salaam
Email: tpdcmd@tpdc-tz.com
Website: http://www.tpdc-tz.com

No comments:

Post a Comment