Tuesday, July 30, 2013

Anyimwa Viza ya New Zealand kwasababu ya ubonge.


Maafisa wa utawala nchini New Zealand , wamemwambia mwanamume mmoja raia wa Afrika Kusini ambaye pia ni mpishi kuwa ni mnene kupita kiasi kuweza kuruhusiwa kuishi nchini humo.
Maafisa wa uhamiaji walisema kuwa Albert Buitenhuis, mwenye uzani wa kilo 130 hana afya nzuri.
Sasa anakabiliwa na tisho la kufukuzwa kutoka nchini humo licha ya kupunguza uzani wake kwa kilo 30 tangu kuhamia mjini Christchurch miaka sita iliyopita.
New Zealand ni mojawapo ya nchi zenye idadi kubwa ya watu wenye unene kupita kiasi huku takriban asilimia 30 ya watu wake wakiwa waathiriwa.
Bwana Buitenhuis na mkewe walihamia nchini New Zealand, mwaka 2007. Wakati huo mwanamume huyo alikuwa na uzani wa kilo 160.
Hadi sasa wamekuwa wakipokea Viza zao zinazowaruhusu kufanya kazi nchini humo bila matatizo mengi kulingana na mkewe.
''Tumekuwa tukiomba viza hizo kila mwaka na hapajawahi kuwa na matatizo yoyote, '' alisema mkewe Albert
"hawajawahi kuzungumzia uzito wa Albert wala afya yake wakati hata alipokuwa mnene kushinda sasa.''
Lakini mapema mwezi Mei, wanandoa hao waliambiwa kuwa hawatapokea visa mpya kwa sababu ya unene wa bwana Buitenhuis.
"nimeshangazwa sana kwa sababu kwa sasa ameweza kupoteza kilo 30 tangu tuje hapa New Zealand, '' alisema mkewe Buitenhuis.
Wawili hao wamemuomba waziri wa uhamiaji wa nchi hiyo kuwaruhusu waendelee kuishi nchini humo kwani bwana Buitenhuis ameweza kupoteza kilo.
Msemaji wa uhamiaji alisema kuwa bwana Buitenhuis alinyimwa visa mpya kwa sababu ya tisho kwa afya yake kutokana na uzani wake, kuwa anaweza kupatwa na kisiukari, shinikizo la damu na maradhi ya moyo.
BBC SWAHILI

Tuesday, July 23, 2013

Familia ya kifalme Uingereza yapata mtoto.

 Kate na Prince William siku ya ndoa yao wakipungia mikono wananchi wa Uingereza waliohudhuria.

Tangazo la kuzaliwa mwana mfalme likitolewa katika kasri la Birmingham.

Ujumbe wa heri njema umeendelea kutolewa kutoka kote duniani baada ya Kate na Prince William ambaye atakuwa wa tatu kwenye foleni katika kurithi ufalme wa Uingereza.
Mwanamfalme William na mkewe Kate ,wameamkia hospitalini asubuhi ya leo mjini London baada ya kupata mtoto wao wa kwanzaJumatatu jioni.

Mtoto huyo aliyezaliwa akiwa na takriban kilo tatu na nusu atafahamika kama mwanamfalme wa Cambridge, lakini hajapewa jina.
Katika taarifa fupi William,amesema wana furaha isiyo na kifani.
Baadaye leo jeshi la Uingereza linatarajiwa kutoa heshima kwa kuzaliwa mwanamfalme huyo kwa kurusha mizinga 40 hewani huko London na kengele la kanisa la Westminster Abbey zitalia.
Kawaida saluti ambayo hutolewa kwa mwanamfalme huwa ni mizinga ishirini na moja lakini huongezeka hadi arobaini na moja ikiwa itarushwa kutoka katika makao ya kifalme
Taarifa kutoka katika Kasri la Buckingham, zinasema kuwa Malkia Elizabeth na mumewe walifurahishwa sana na habari za kuzaliwa kwa mtoto huyo. Naye babake William
Prince Charles, alisema ana furaha isiyo kifani na ana raha sana kuwa babu kwa mara ya kwanza.
Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron, alisifu sana kuzaliwa kwa mtoto huyo na kuitaja kuwa hatua muhimu sana kwa Uingereza.
Naye wawiri mkuu wa Australia, Kevin Rudd, alitaja sherehe za jana kama muhimu sana kwa nchi za juimuiya ya madola, huku akiongeza kuwa watu wa Australia wanampenda sana Prince William baada ya kuzuru nchi hiyo akiwa mtoto mwenyewe.
BBC SWAHILI

Timu za soka zinawatumia vipi wafadhili?


 
Rais wa Simba Aden Rage (kushoto) akipeana mkono na mwakilishi wa Azam huku mwanasheria wa Azam akishuhudia mara baada ya kusaini mkataba wa mil 331 wiki iliyopita.
Wiki iliyopita timu kongwe ya soka nchini Simba SC iliingia mkataba mnono wa mil 331 na Azam Media Group ili kuweza kuitumia Simba TV kurusha matukio mbalimbali ya timu hiyo wakati huohuo  watapata faida ya kutangaza biashara zao.
Siku zote waswahili husema penye fungu ndipo huenda nyongeza lakini watu husahau kuwa anayehangaika ndiye anayepata.
Wapinzani wakubwa wa Simba yaani Yanga nawo walipata kuingia kwenye mazungumzo na Azam Media Group ili kupata mkataba aina hiyo ila haijulikani mazungumzo yao yameishia vipi. Ila kikubwa ni dalili za wazi kuwa vilabu vya soka Tanzania  vinaanza kuendeshwa kwa faida.
Hili ni somo kwa timu nyingine zinazoshiriki ligi kuu ya Tanzania bara kutafuta wadhamini watakaowapa kipato kikubwa kitakachowawezesha kujenga majengo ama kuanzisha miradi  itakayowasaidia kupata fedha za kuendesha timu kwa mwaka mzima, bila kutegemea fedha za mlangoni ambazo hazina uhakika.
Fedha inayopatikana lazima itumike kutengeneza fedha, Simba na Yanga wamejaaliwa kupata busara hiyo ya kuwekeza kwenye soka kwa kuendeleza vyanzo vya mapato. Kingine ni kuwa na uongozi uliokamilika ambapo kunakuwa na ofisi zilizo hai zenye kushughulikia masuala ya fedha, miradi, usajili, kuuza taswira ya timu ndani na nje ya nchi na kamati maalum inayokutana na wafadhili kujadili thamani ya timu.
Hapa ndipo timu nyingine zinaposhindwa, mfadhili lazima aangaliwe kiwango anachonufaika kwa kutangaza biashara yake kwenye vifua ama migongo ya wachezaji, timu nayo inanufaika kwa kiwango hichohicho?
Huu si wakati wa kun’gan’gania wafadhili bali timu zinahitaji kupata wadhamini watakaoingia mikataba na timu ili iwepo ‘win win situation’ timu inufaike na mdhamini anufaike.
Kwa kipindi kirefu nembo ya Yanga ilitumika vibaya, wajanja waliuza bendera, fulana na vifaa vingine vyenye nembo ya Yanga. Mpaka miezi michache ilipopita baada ya watu wenye akili kukaa na kujadili uhalali wa watu kuitumia vibaya nembo ya timu, ndipo ikapitishwa hoja kuwa nembo lazima iiletee faida timu.
Yanga sasa wanazungumza kuhusu kujenga uwanja utakaoingiza watazamaji 40,000 hicho ni kitega uchumi kikubwa kitakachowaingizia mapato mengi kwa mwaka mzima.
Viongozi wa timu zinazoshiriki ligi kuu wafunguke macho katika hili, ligi ya Tanzania muda si mrefu itaingia kwenye orodha ya ligi zinazorushwa kwenye kituo maarufu cha luninga Supersport. Wadhamini lazima watambue gharama ya kutangaza biashara zao kwenye luninga inayorusha matangazo dunia nzima.
HAFIDH KIDO
23 JULAI, 2013

Monday, July 22, 2013

Jacob Zuma amwambia balozi wake Zimbabwe asijibizane na Rais Mugabe.


Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amemtaka balozi wake nchini Zimbabwe kukoma kutoa matamshi hadharani baada ya kukosolewa na rais Robert Mugabe.
Zuma, aliyekuwa mpatanishi mkuu katika mgogoro wa kisiasa mwaka 2008-2009 nchini Zimbabwe, alisema ni yeye pekee anayeruhusiwa kutoa matamshi yoyote kabla ya uchaguzi mkuu kufanyika Julai tarehe 31.
Balozi wake Lindiwe Zulu, wiki jana alisema kuwa maandalizi ya uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe hayaonekani kuridhisha.
Rais wa Zimbabwe ndiye alimtaka Zuma kumkomesha balozi wake dhidi ya kutoa matamshi kama hayo hadharani.
Rais Mugabe ananuia kuendelea kuongoza nchi hiyo hata baada ya kuitawala kwa miaka 33 na atamenyana na waziri mkuu wake Morgan Tsvangirai.
Mahasimu hao wa jadi wamekuwa wakigawana mamlaka tangu mwaka 2009, chini ya mkataba ulioafikiwa kwa usaidizi wa rais Zuma.
BBC SWAHILI