Friday, July 19, 2013

Hizi ndizo kamati mpya za TFF.



 
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemteua Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bernard Luanda kuongoza Kamati ya Rufani ya Uchaguzi kufuatia mabadiliko ya Katiba yaliyofanywa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) na kuingiza kamati nyingine mpya.

Rais wa TFF, Leodegar Tenga ametangaza wajumbe wa kamati hizo leo (Julai 18 mwaka huu) mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema uteuzi wa wajumbe hao umezingatia maoni ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, lakini vilevile amewashukuru wajumbe walioteuliwa kwa kukubali kutoa mchango wao katika maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

Mbali ya Jaji Luanda ambaye ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, wajumbe ni Francis Kiwanga (Makamu Mwenyekiti), Anney Semu, Yohane Masalla na Allen Kasamala. Kamati ya Uchaguzi inaongozwa na Hamidu Mbwezeleni, Moses Kaluwa (Makamu Mwenyekiti), Mustafa Siyani, Hassan Dyamwale na Kitwana Manara.

Mwenyekiti Kamati ya Rufani ya Maadili ni Jaji Steven Ihema, Bi. Victoria Makani (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Mohamed Missanga, Henry Tandau na Mheshimiwa Murtaza Mangungu. Kamati ya Maadili inaundwa na Bi. Jesse Mguto (Mwenyekiti), Francis Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Profesa Mtambo Madundo, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Mohamed Mpinga na Evod Mmanda.

Profesa Mgongo Fimbo anaongoza Kamati ya Rufani ya Nidhamu wakati Makamu wake ni Ong’wanuhama Kibuta na wajumbe ni Kanali Mstaafu Idd Kipingu, Dk. Mshindo Msolla na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Mstaafu Jamal Rwambow. Kamati ya Nidhamu inaongozwa na Kamishna wa Polisi (CP) Mstaafu Alfred Tibaigana, Mustafa Kambona (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Azzan Zungu, Yusuf Nzowa na Mohamed Msomali.
Pia Kamati ya Utendaji imefanya mabadiliko katika Kamati ya Waamuzi ambapo Said Nassoro na Charles Ndagala kutoka Chama cha Waamuzi wanachukua nafasi za Joan Minja na Riziki Majala. Kamati hiyo inaendelea kuongozwa na Kapteni Mstaafu Stanley Lugenge, Omar Kasinde (Makamu Mwenyekiti) wakati mjumbe mwingine ni Mohamed Nyama.

Kamati ya Tiba inaongozwa na Dk. Paul Marealle wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti itajazwa baadaye na Rais Tenga. Wajumbe ni Mwanandi Mwankemwa, Anthony Ngome, Frank Mhonda, Kapteni Joakim Mshanga na Helen Semu.

Rais Tenga alisema mabadiliko mengine yamefanyika kutokana na waliokuwa wajumbe kuomba kupumzika. Wajumbe walioomba kupumzika ni Dk. Sylvester Faya, Idd Mtiginjola na Deo Lyatto

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Julai 18, 2013

No comments:

Post a Comment