Wednesday, July 3, 2013

Obama aacha gumzo Tanzania..

 Hakika ni kipenzi cha watu, kila mmoja alitamani kumshika mkono ili aje kuwasifia wajukuu zake baadaye.

 Alikutana na Rais wa zamani wa Marekani George W. Bush ambaye alikuja kwa shughuli za kimaendeleo.

 Kitu ambacho watanzania wengi kiliwafurahisha ni namna alivyoonyesha mahaba ya hali ya juu kwa mkewe.

 Kikafuata kikao cha kujadili miradi watakayotiliana saini ili kila nchi inufaike. Mwenyewe aliita win win situation.

Akatuachia mipira inayozalisha gesi, yaani unawapa watu wanaichezea weee halafu unatumia kuwashia taa au kuzalisha umeme .


Dar es Salaam. Rais Barack Obama wa Marekani ameitaka Serikali ya Tanzania kuhakikisha miradi iliyopangwa kutekelezwa chini ya ufadhili wa nchi hiyo haicheleweshwi bila ya sababu za msingi.
Alisema hayo jana katika mitambo ya kufua umeme ya Symbion na kubainisha kuwa Marekani imetenga kiasi cha Dola 7 bilioni zitakazotolewa kwa nchi sita za Afrika katika kipindi cha miaka mitano kugharimia miradi ya umeme.
Akizungumza mbele ya mwenyeji wake, Rais Jakaya Kikwete, Rais Obama alisema utamaduni wa kuchelewesha utekelezaji wa miradi haufai kufumbiwa macho kwani unakawiza maendeleo kwa wananchi wenye shida.
“Utakuta mradi unakaa kwa miaka saba au minane bila ya kutekelezwa, jambo hilo hatutaki litokee. Mara mradi unapopangwa na mipango kukamilika, basi utekelezwe haraka iwezekanavyo ili wananchi waone faida zake,” alisisitiza Rais Obama.
Rais Obama alikuwa akizungumzia mradi mkubwa wa umeme unaofadhiliwa na nchi yake ujulikanao kama ‘Power Afrika’ ambao pamoja na fedha hizo za Serikali yake, taasisi mbalimbali binafsi nazo zimetoa Dola 9 bilioni kwa ajili ya utekelezaji wake.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya hotuba hiyo ya Rais Obama, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema tatizo la ucheleweshaji wa miradi halipo kwa Tanzania kwa kuwa Serikali imejipanga vyema kuhakikisha kuwa mambo yanakwenda kwa kasi chini ya utaratibu mpya wa ‘Matokeo Makubwa Sasa’ (Big Results Now) inayosimamiwa na Kitengo cha Ofisi ya Rais kinachoitwa President’s Delivery Unit.
Hata hivyo, Profesa Muhongo alisema tayari Tanzania imeshaorodhesha miradi ambayo ingependa itekelezwe chini ya mpango huo na tayari miradi hiyo imeshawasilishwa katika ofisi za Ubalozi wa Marekani nchini.
Waziri Muhongo alisema miradi mingi ni ya umeme vijijini ambayo inatekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (Rea).
Katika hotuba yake fupi, Rais Obama alibainisha kuwa lengo la Marekani ni kuzisaidia nchi za Afrika kujiondoa katika umasikini ili ziondokane na kuwa ombaomba wa misaada.
“Kwa yale niliyoyaona katika ziara yangu ya wiki moja kuanzia Senegal, Afrika Kusini na hapa Tanzania, ni dhahiri kuwa Afrika ina uwezo wa kujiondoa katika umasikini,” alisema Rais Obama.
Alisema mradi huo wa Power Africa unalenga mambo mawili makubwa. Kwanza, kuhakikisha kuwa idadi ya watu wanaopata umeme inaongezeka maradufu na pili kuziwezesha nchi za Afrika kujenga uwezo wa kuzalisha umeme wa kutosha.
“Kwa kuanzia, ili kutekeleza dhamira hiyo, tutahakikisha kuwa tunawapatia umeme watu milioni 20 katika nchi sita ambako mradi huu utatekelezwa,” alisema.
Rais Obama alisema wakati umefika sasa kwa Afrika kujigeuza kutoka bara la kuomba misaada na kuanza kuwa mtoaji wa misaada kwani uwezekano wa kufanya hivyo ni mkubwa.
Alisema kupitia mradi wa Power Africa kwa mfano, bara hilo lina nafasi kubwa ya kukuza uwekezaji na hivyo kuongeza uzalishaji na uuzaji wa bidhaa nje.
“Katika hili Marekani ipo pamoja nanyi. Hivi sasa tumekuwa na mbinu mpya ya kusaidia maendeleo kwa kuhakikisha kuwa tunakuwa washirika wa kuzisaidia nchi masikini ziweze kusimama zenyewe na kujihudumia,” alisema.
Alisema mradi huo utakuwa na faida kwa pande zote, kwani nchi za Kiafrika zitawawezesha wananchi wake kuongeza uzalishaji na hivyo kukuza vipato vyao na kwa upande mwingine, Marekani itafaidika kwa kampuni zake kuwekeza katika Bara la Afrika na hivyo kukuza ajira na mapato ya nchi hiyo kubwa duniani.
Kuhusu mradi huo; Profesa Muhongo alisema umekuja katika wakati mwafaka kwani Tanzania imeshajipanga kuongeza maradufu uzalishaji wa umeme kutoka kiwango cha sasa cha megawati 1,438.24 hadi kufikia megawati 2,780 mwaka 2015.
“Lengo letu ni kujenga uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 3,000,” alisema na kubainisha kuwa baada ya muda Watanzania wataanza kuona manufaa ya mipango hiyo ya Serikali.
Wakiwa katika mtambo huo wa Symbion, marais Obama na Kikwete pia walipewa maelezo kuhusu aina mpya ya mpira wa miguu ambao umejazwa gesi inayozalisha umeme.
Akitoa maelezo hayo, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Uncharted Play Inc ya Marekani inayotengeneza mipira hiyo, Jessica Matthews alisema mtu anaweza kuutumia umeme huo kuwashia taa na pia kuchajia simu ya mkononi.
Rais Obama aliisifia teknolojia hiyo mpya na kubainisha kuwa itawezesha watu wengi zaidi kupata umeme kwa gharama nafuu.

Kutoka Richmond hadi Symbion
Katika kuashiria jinsi dunia inavyobadilika haraka, mitambo ya Symbion yenye historia ndefu imegeuka kuwa mkombozi wa nishati ya umeme kwa Taifa la Tanzania baada ya kununua mitambo hiyo kutoka Kampuni ya Dowans mwaka 2011.
Dowans hadi sasa inavutana na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ikidai kiasi cha Dola 65 milioni ambazo iliamriwa zilipwe na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi ya Kibiashara.
Kampuni hiyo ilirithi mitambo hiyo kutoka kwa Kampuni ya Richmond, ambayo ilituhumiwa na Bunge kuwa na uwezo mdogo mwaka 2007.
Pia inadaiwa kupewa zabuni hiyo kinyume cha taratibu kiasi cha kusababisha Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa kujiuzulu pamoja na Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi na Waziri wa zamani wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Idrissa Msabaha.
Mkutano wa nishati
Katika hatua nyingine; Wizara ya Nishati na Madini leo inafanya kongamano la wazi na uzinduzi wa mpango wa kuleta matokeo makubwa sasa.
Profesa Muhongo amewaalika wadau wote wa sekta hiyo kwenye mkutano huo utakaofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City kuanzia saa 3.00 hadi saa 11.00 jioni.
Mada kuu itakuwa kujadili, kushauri na kutoa maoni juu ya miradi mikubwa ya sekta ya umeme itakayotekelezwa katika kipindi cha miaka mitatu.
MWANANCHI

No comments:

Post a Comment