Thursday, July 4, 2013

Rais wa mpito aapishwa Misri



Jaji mkuu wa mahakama ya juu zaidi ya kikatiba ameapishwa nchini Misri kuwa rais wa muda baada ya jeshi kumng'oa mamlakani rais aliyechaguliwa na raia kwa njia ya kidemokrasia na kushinda kwa wingi wa kura, Mohammed Morsi.
Viongozi duniani wamepokea kwa tahadhari matukio yanayojiri huko Misri. Waziri wa mashauri ya kigeni wa Ujerumani, Guido Westerwelle, amewaambia waandishi kwamba anaangalia kwa umakini hatua iliyochukuliwa na jeshi la Misri.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Uingereza , William Hague, amesema Uingereza haiungi mkono uvamizi huo wa kijeshi lakini haina budi kuitambua hatua hiyo na kusogea mbele. Hata hivyo alikataa kulishutumu jeshi kwa kumpindua Morsi akisema ni uvamizi ulioungwa mkono na watu wengi.
Mfalme Abdalla wa Saudia ametuma ujumbe wa hongera kwa kaimu rais wa Misri akisema kwamba uteuzi wake unajiri katika wakati muhimu.
Mkuu wa jeshi Generali Abdul Fattah al-Sisi alitoa tangaza hilo kupitia televisheini Jumatano jioni, katika kile Morsi, alisema ni mapinduzi ya kijeshi.
Generali Sisi alisema kuwa Morsi,ambaye ni rais wa kwanza kuchaguliwa amekosa kutimiza mahitaji ya watu.
Ishara ya mapenzi iliyochorwa angani kwa kutumia ndege za kijeshi kuwataka wananchi kupatana
Hatua hiyo inakuja baada ya siku nyingi ya maandamano, dhidi ya rais Morsi wa chama cha Musolim Brotherhood.
Waandamanaji walimtuhumu yeye na chama chake kwa kusukuma ajenda ya kiisilamu kwa taifa hilo na kukosa kusuluhisha matatizo ya kiuchumi yanayokumba taifa hilo.
Chama cha Muslim Brotherhood kimesema kuwa bwana Morsi pamoja na washauri wake wako chini ya kifungo cha nyumbani na hawana mawasiliano ya nje.
Hapo awali mkuu wa majeshi alisema kuwa katiba ya nchi hiyo imeahirishwa na kwamba jaji mkuu wa taifa hilo atachukuwa mamlaka ya rais.
Maelfu ya waandamanaji wanaompinga bwana Morsi mjini Cairo walisherehekea kwa shangwe na vifijo kufuatia taarifa hiyo ya jeshi lakini wale wanaomuunga bwana Morsi wanasemekana kubaki kimya huku wakisubiri matukio yatakayofwata.
Rais Obama amesema kuwa ana wasiwasi mkubwa kuhusiana na matukio yaliyopo nchini Misri huku katibu mkuu wa umoja wa mataifa Banki Moon akitaka kuwe na utulivu.
BBC SWAHILI

No comments:

Post a Comment