Wednesday, July 10, 2013

Serikali imeamua kufufua viwanda 17 vilivyorudi mikononi mwao baada ya kubinafsishwa.

 Nicodemus Mushi, Ofisa habari na mawasiliano Wizara ya viwanda na biashara akizungumza na waandishi wa habari leo asubuhi katika ukumbi wa idara ya habari MAELEZO jijini.

 Nicodemus Mushi akiwa na naibu mkurugenzi wa MAELEZO, Zamaradi Kawawa leo asubuhi.

Wanahabari wakifuatilia kwa makini maelezo ya ofisa habari na mawasiliano wa wizara ya viwanda na biashara.


Serikali imeamua kufufua viwanda vyote vilivyokufa wakati wa kipindi cha kubinafsisha viwanda vya Serikali wakati wa awamu ya tatu ya utawala wa Rais Benjamin Mkapa.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mendeleo ya viwanda na biashara nchini ofisa habari na mawasiliano wa wizara ya viwanda na biashara Tanzania, Nicodemus Mushi amesema wizara hiyo imedhamiria kuongeza ajira na kukuza pato la taifa kupitia viwanda vya ndani.
Mushi aliweka wazi kuwa Wizara imekusudia kuifanya sekta ya viwanda nchini kuendelea kuisaidia juhudi za Serikali katika kupambana na tatizo la ajira nchini kwa kuajiri idadi kubwa zaidi ya watu hasa vijana wenye ujuzi katika fani mbalimbali na kuzalisha bidhaa bora kwa kiwango kinachohitajika kwa soko la ndani na nje ya nchi.
“Viwanda vilivyobinafsishwa chini ya sekta ya viwanda na biashara ni 74 na kati ya hivyo ni viwanda 17 tu ndivyo havifanyi kazi. Juhudi za kufufua viwanda hivyo zinafanyika chini ya Consolidated Holding Corporation (CHC) iliyo chini ya wizara ya fedha, kwa kuzingatia utaratibu wa urekebishaji wa mashirika ya umma,” alieleza Mushi.
Aidha wizara hiyo imelenga kuboresha vivutio kwa ajili ya uwekezaji kwenye viwanda vinavyotumia malighafi mbalimbali zilizopo nchini vikiwemo viwanda vya nguo, ngozi, usindikaji matunda, mbogamboga na usanifu wa madini ya vito.
Katika hatua nyingine wataangalia wajasiriamali hasa wa vijijini ili kuwaeweka katika program ya muunganisho wa ujasiriamali vijijini kwa kutoa ushauri, mafunzo, mitaji na huduma za kiufundi kwa wajasiriamali.
“Tunawatazama wajasiriamali kama kundi maalum linalopewa kipaumbele, lengo letu ni kuhakikisha sekta hii inaendelea kuwakomboa watanzania kwa kuwapa ajira, kuwapa kipato na kuwaondolea umaskini. Ndiyo maana SIDO na chuo chetu cha elimu ya biashara wapo pamoja nao wakati wote likiwapa mafunzo, kukusanya katika vikundi na kuwapa mbinu za kupata mitaji na namna bora ya kufanya shughuli zao kwa tija,” alieleza Mushi.
HAFIDH KIDO
10 Julai, 2013
DAR ES SALAAM, TANZANIA

No comments:

Post a Comment