Tuesday, July 23, 2013

Timu za soka zinawatumia vipi wafadhili?


 
Rais wa Simba Aden Rage (kushoto) akipeana mkono na mwakilishi wa Azam huku mwanasheria wa Azam akishuhudia mara baada ya kusaini mkataba wa mil 331 wiki iliyopita.
Wiki iliyopita timu kongwe ya soka nchini Simba SC iliingia mkataba mnono wa mil 331 na Azam Media Group ili kuweza kuitumia Simba TV kurusha matukio mbalimbali ya timu hiyo wakati huohuo  watapata faida ya kutangaza biashara zao.
Siku zote waswahili husema penye fungu ndipo huenda nyongeza lakini watu husahau kuwa anayehangaika ndiye anayepata.
Wapinzani wakubwa wa Simba yaani Yanga nawo walipata kuingia kwenye mazungumzo na Azam Media Group ili kupata mkataba aina hiyo ila haijulikani mazungumzo yao yameishia vipi. Ila kikubwa ni dalili za wazi kuwa vilabu vya soka Tanzania  vinaanza kuendeshwa kwa faida.
Hili ni somo kwa timu nyingine zinazoshiriki ligi kuu ya Tanzania bara kutafuta wadhamini watakaowapa kipato kikubwa kitakachowawezesha kujenga majengo ama kuanzisha miradi  itakayowasaidia kupata fedha za kuendesha timu kwa mwaka mzima, bila kutegemea fedha za mlangoni ambazo hazina uhakika.
Fedha inayopatikana lazima itumike kutengeneza fedha, Simba na Yanga wamejaaliwa kupata busara hiyo ya kuwekeza kwenye soka kwa kuendeleza vyanzo vya mapato. Kingine ni kuwa na uongozi uliokamilika ambapo kunakuwa na ofisi zilizo hai zenye kushughulikia masuala ya fedha, miradi, usajili, kuuza taswira ya timu ndani na nje ya nchi na kamati maalum inayokutana na wafadhili kujadili thamani ya timu.
Hapa ndipo timu nyingine zinaposhindwa, mfadhili lazima aangaliwe kiwango anachonufaika kwa kutangaza biashara yake kwenye vifua ama migongo ya wachezaji, timu nayo inanufaika kwa kiwango hichohicho?
Huu si wakati wa kun’gan’gania wafadhili bali timu zinahitaji kupata wadhamini watakaoingia mikataba na timu ili iwepo ‘win win situation’ timu inufaike na mdhamini anufaike.
Kwa kipindi kirefu nembo ya Yanga ilitumika vibaya, wajanja waliuza bendera, fulana na vifaa vingine vyenye nembo ya Yanga. Mpaka miezi michache ilipopita baada ya watu wenye akili kukaa na kujadili uhalali wa watu kuitumia vibaya nembo ya timu, ndipo ikapitishwa hoja kuwa nembo lazima iiletee faida timu.
Yanga sasa wanazungumza kuhusu kujenga uwanja utakaoingiza watazamaji 40,000 hicho ni kitega uchumi kikubwa kitakachowaingizia mapato mengi kwa mwaka mzima.
Viongozi wa timu zinazoshiriki ligi kuu wafunguke macho katika hili, ligi ya Tanzania muda si mrefu itaingia kwenye orodha ya ligi zinazorushwa kwenye kituo maarufu cha luninga Supersport. Wadhamini lazima watambue gharama ya kutangaza biashara zao kwenye luninga inayorusha matangazo dunia nzima.
HAFIDH KIDO
23 JULAI, 2013

No comments:

Post a Comment