Tuesday, July 9, 2013

TRL kusafirisha mizigo ya tani mil 3 kwa mwaka ifikapo 2015.

 Mkurugenzi mtendaji bwa TRL, Mhandisi Kipallo Aman Kisamfu (katikati) akizungumza na wanahabari katika ukumbi wa idara ya habari MAELEZO leo asubuhi.

Bi Zamaradi Kawawa (aliyesimama) ambaye ni naibu Mkurugenzi wa idara ya habari MAELEZO akiwafafanulia wanahabari juu ya baadhi ya majibu yaliyokanganya kutoka TRL.


Mkurugenzi mtendaji wa TRL, mhandisi Kipallo Aman Kisamfu amesema wanataka kuhakikisha ifikapo mwaka 2015 shirika hilo liwe na uwezo wa kusafirisha tani milioni 3 za mizigo kwa mwaka.
Akizungumza katika ukumbi wa idara ya habari MAELEZO jijini Dar es Salaam leo asubuhi Kisamfu amesema Serikali imeamua kuuweka usafiri wa reli katika vipaumbele vya taifa vilivyowekwa katika mpango wa taifa wa miaka mitano unaoanzia 2011-2016.
“Mpango huu wa taifa umeongezewa nguvu kupitia mpango mwingine wa miaka mitatu ambao ni mfumo mpya wa kusimamia utekelezaji, ufuatiliaji na tathmini ya miradi ya maendeleo. Mpango huu umeanza kutekelezwa kwa kutumia uzoefu wa ‘Performance Management and Delivery Unit’ (PEMANDU) kutoka Malaysia.
“Katika mpango wa PEMANDU ambao unaendana na program ya matokeo makubwa ya haraka (Big Results now ‘BRN’), TRL imepanga kusafirisha mizigo kiasi cha tani milioni 3 kwa mwaka ifikapo mwaka 2015. Kiasi hiki ni kikubwa ambacho hakijawahi kusafirishwa na reli ya kati tangu ilipojengwa miaka mia moja iliyopita,” alisema KIsamfu.
Aidha katika bajeti ya Serikali mwaka wa fedha 2013/14 TRL imetengewa Sh Bil 137.6 ili kukamilisha miradi iliyokwishaanza kupitia bajeti ya mwaka jana. Miradi itakayokamilika kupitia bajeti ya mwaka wa fedha 2013/14 ni pamoja nah ii ifuatayo: Kutengeneza upya vichwa vya treni 8, kununua vuchwa vipya 13, kununua mabehewa mapya ya abiria 22, kununua mabehewa mapya ya mizigo 274, kununua mabehewa ya kubebea kokoto 25, kununua mabehewa ya breki  34, kununua mashine moja ya kushindilia kokoto kwenye reli, na kupata kreni moja yenye uwezo wa tani 100 ya kunyanyulia mabehewa na vichwa vya treni zinapotokea ajali.
Hata hivyo kwa mujibu wamkurugenzi mtendaji huyo wa TRL mradi wa miaka mitatu wa kuiinua TRL unahitaji kiasi cha Sh trilioni 1.1 ili kununua vichwa vipya vya treni 58, mabehewa ya mizigo 1960, mabehewa ya abiria 44 lengo likiwa ni kupata uwezo wa kubeba mizigo ya tani milioni 3 kwa mwaka ifikapo mwaka 2015.
 
HAFIDH KIDO
9 Julai, 2013
DAR ES SALAAM, TANZANIA

No comments:

Post a Comment