Sunday, January 5, 2014

Mapendekezo ya Mgawanyo Mpya wa Manispaa za Jiji la Dar es Salaam

 

Nimepokea mwaliko wa kikao maalumu cha kikao cha fedha na uongozi wa tarehe 3/01/2014 kikao kufanyika tarehe 06/01/2013 saa nane mchana kujadili mapendekezo ya kuongeza maeneo mapya ya utawala katika Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na ajenda zingine.

Nimeonelea tija kuwasilisha mapendekezo yangu kwa maandishi kwa umma na baadae katika kikao tajwa. Kwa hatua hii, ni fursa kwa kila mwananchi kutoa maoni yake juu ya haya;

Kwa ukuaji wa kasi wa Dar es Salaam ambao ndiyo mji mkubwa nchini Tanzania, jiji kitovu cha biashara na viwanda ambalo kadiri ya takwimu linakadiriwa kuwa na idadi ya watu milioni nne na nusu. Jiji hili limeshika nafasi ya tatu katika miji inayokuwa kwa kasi barani Afrika na miongoni mwa miji kumi inayokuwa kwa kasi duniani.

Ifahamike pia, Jiji la Dar es Salaam ndilo linashikilia asilimia themanini na tatu (83%) ya mapato ya serikali kitaifa na takribani asilimia sabini (70%) ya kodi zote zinazokusanywa nchini Tanzania.

Yafuatayo ndiyo mapendekezo yangu ya wasilisho la nyaraka ya mapendekezo yaliyoletwa katika ofisi yangu toka Manispaa ya Kinondoni;

Mosi, Pendekezo la kutumia “Manispaa” badala ya “Wilaya”:
Kadiri ya wasilisho, imetumika pendekezo la “wilaya”. Ningeshauri na kupendekeza kutokana na uhalisia na ukuaji wa kasi kutumika kwa “Manispaa” badala ya wilaya.

Pili, Pendekezo bora la mgawanyo wa Manispaa:
Katika wasilisho lenye uwepo wa mapendekezo saba. Ninaungana na kuafiki utumiaji wa pendekezo la pili lililowasilishwa la kuwa na Manispaa tano (5) ambazo ni;
i.                    Manispaa ya Ilala
ii.                 Manispaa ya Temeke
iii.               Manispaa ya Kinondoni
iv.                Manispaa ya Kigamboni
v.                  Manispaa ya Ubungo

Sababu muhimu:
1.        Ukubwa kijiografia: Kwa kuongeza wilaya mbili mpya yaani Manispaa ya Kigamboni na Manispaa ya Ubungo hii itasaidia wilaya hizi kuweza kuhimili ukubwa wa eneo wa kijiografia ambalo kwa sasa inaelemea wilaya hizi za sasa yaani Manispaa ya Kinondoni na Manispaa ya Temeke.
2.      Ukuaji wa kasi wa jiji: Katika ukuaji wa kasi unaoendelea jiji la Dar es Salaam maeneo yaliyopo katika wilaya hasa ya Kinondoni na Temeke ndiyo ambayo yanaongoza pia katika ukuaji huo wa kasi wa kimakazi na shughuli za kiuchumi kama viwanda na uwekezaji. Hivyo kwa kuwa na Manispaa mpya mbili(Manispaa ya Ubungo na Manispaa ya Kigamboni) zitasaidia kwa kiasi kikubwa kuweza kusimamia vyema mipango miji, kuujenga vyema mji na kusimamia kihuduma.
3.       Uwepo wa mipango ya kuimarisha ukuaji wa jiji kupitia miji ya pembezoni “satellite cities”: tayari serikali imeweka dhamira ya kuimarisha ukuaji wa jiji kupitia satellite cities. Hivyo uwepo wa wilaya mbili yaani Kigamboni (Satellite city Kigamboni) na Ubungo (“Luguruni Satellite City” ndani ya Kata ya Kwembe na Kata ya Kibamba) zitamudu kusimamia vyema ujenzi imara wa satellite cities na pia kuwezesha wilaya zitakazoachwa kama wilaya ya Kinondoni kuwa na ahueni ya kuelemewa na kazi hivyo nazo kusimamia vyema mipango ya ujenzi wa satellite cities zilizomo ktk maeneo hayo


Tatu, Ugawaji wa kata ndani ya Manispaa mpya na kusimamia kata zilizopo:
Katika mapendekezo yaliyowasilishwa, kumekuwa na mgawanyo mpya unaonyang’anya kata ambazo tayari zilikwisha kuwapo katika baadhi ya maeneo mathalani ndani ya Manispaa ya Kinondoni. Mfano wa maeneo kama Kisopwa, Mloganzila. Maeneo tajwa yamekuwa yakihamishwa toka Manispaa ya Kinondoni na kupelekwa Mkoa wa Pwani. Hivyo kukizana hata na dhamira ya kujaribu kuchukua baadhi ya kata na maeneo ambayo yapo katika miji inayokaribia jiji la Dar es Salaam katika dhamira ya kupanua jiji.

Pia, kwa nyakati tofauti tumeshuhudia viongozi wa kitaifa wakitaja mara kwa mara katika hotuba zao na matamko yako maeneo yaliyopo ndani ya Manispaa ya Kinondoni kama eneo la Mloganzila kuyataja kuwa katika Mkoa wa Pwani. Jambo hili si sahihi. Jambo hili limekuwa likiacha maswali mengi kwa wananchi. Ifahamike tu, wananchi hawa wanatambulika chini ya mifumo rasmi tuliyojiwekea inayowatambua kama wakazi wa Manispaa ya Kinondoni.

Kuna umuhimu mkubwa sana wa kuhakikisha ufafanuzi mpana unawekwa na kusimamia uwepo wa maeneo haya yaendelee kuwapo katika wilaya za Dar es Salaam.

Sambamba, kuna hitaji la haraka na muhimu katika mchakato huu kuhakikisha migogoro ya ardhi ndani maeneo ya Kisopwa na Mloganzila yapatiwe ufumbuzi wa kudumu. Pia kuhakikisha maeneo hayo yanabaki katika kata ya Kwembe kwenye Manispaa inayopendekezwa ya Ubungo.

Nne, Kujifunza toka miji na nchi zingine:
Kuna umuhimu mkubwa wa kupanua wigo wa miji na nchi ambazo tunaweza kuchota uzoefu katika zoezi la kugawa wilaya mpya na kupanua jiji la Dar es Salaam. Mifano minne kadiri ya wasilisho pekee haitoshi. Napendekeza na kushauri kuongeza miji iliyopo katika nchi ifuatayo, miji ambayo inashabihiana na sifa za jiji la Dar es Salaam la ukuaji wa kasi, mifumo wa kiutawala, hali za kiuchumi na kimaendeleo ;
i.                    Lagos-Nigeria
ii.                 Johannesburg-South Africa
iii.               London-Uingereza
iv.                New Delhi-India
v.                  Shangai, China

Katika kusoma na kuchukua uzoefu toka katika miji iliyowasilishwa katika pendekezo na hii mingine, tusiishie kuangalia mifumo ya ugawaji, ukuzwaji na usimamizi bali pia twende hatua ya kuangalia muundo wa utendaji wa miji hii ambayo yatasaidia sana katika kuboresha muundo wa kiutendaji wa jiji la Dar es Salaam.

Tano, Mapendekezo katika Muundo wa Kiutendaji wa Jiji la Dar es Salaam:
Nakubaliana na hitaji la kuwepo kwa Jiji la Dar es Salaam kama chombo kikuu juu ya Manispaa zote tano zinazopendekezwa zitakazokuwapo Dar es Salaam.

Pia, nakubaliana na kuunga mkono hitaji la Meya wa Jiji la Dar es Salaam kuchaguliwa na wananchi. Hii itatoa fursa katika utendaji na uwajibikaji imara ambayo unaweza kupimwa na wananchi.

Hivi ndivyo majiji ambayo yamepiga kasi ya kimaendeleo kama London (Uingereza) yanajiendesha. Pia hata majirani zetu kama Kenya; nao wametambua mfumo huu na kuuchukua katika Katiba yao mpya.

Pendekezo muhimu; kuna haja ya Jiji la Dar es Salaam likawa juu ya manispaa zote tano zinazopendekezwa na hivyo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa isiwe na mamlaka na nguvu kulinganisha na Jiji la Dar es Salaam.

Kuna umuhimu mkubwa sana wa kuhakikisha pia Jiji la Dar es Salaam linapatiwa mamlaka na madaraka ambayo hayaingiliwi na kuzuiwa na wilaya nyingine zozote zilizopo chini yake.

Sita, kuunganisha mapendekezo ya Muundo wa Mkoa wa Dar es Salaam na mchakato wa Katiba Mpya ya Tanganyika:
Kwa kutambua nchi ipo katika mchakato wa kuandika katiba mpya ya Tanzania. Mchakato ambao utatoa fursa ya uandishi wa katiba mpya ya Tanganyika kuna umuhimu mkubwa wa kuanza kuandaa kisheria hoja za kuwapo ndani ya katiba ya Tanganyika zenye kusimamia Muundo wa Jiji la Dar es Salaam. Huu ukawa ni mfumo wa mfano “modal” katika ngazi za jiji zenye kuhitaji kuwapo katika mfumo wa kikatiba. Hii ikiwamo na suala la Meya wa Jiji kubwa kuchaguliwa na wananchi na mengineyo muhimu.

Kuna umuhimu pia wa kuwepo wa hoja ya kikatiba katika upanuzi na ukuaji wa Manispaa na ngazi nyingine za miji ndani ya Katiba. Hivyo, Katiba ya Tanganyika inahitaji kuwa nguzo muhimu.

Hitimisho:
Naomba wananchi wa Jimbo la Ubungo na wananchi wa Jiji la Dar es Salaam kwa ujumla kutoa maoni yenu ili hatimaye tupate mfumo bora wa kiutawala kwa maslahi na ukuaji wa Jiji letu.

Wenu katika utumishi,

John J. Mnyika
Mbunge wa Jimbo la Ubungo

06 Januari, 2013

Hatimae Rais wa Sudan Kaskazini Omar Bashir, akubali kukutana na Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir..



Rais wa Sudan Omar al-Bashir anatarajiwa kuwasili mjini Juba kwa mazungumzo na Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir kuhusu mapigano yanayotokota nchini humo.
Vita vimekuwa vikiendelea nchini humo kwa zaidi ya wiki tatu huku pande zinazozozana zikikutana nchini Ethiopia kujaribu kukubaliana juu ya kusitisha vita.
Mgogoro huo ni kati ya jeshi la serikali ya Rais Kiir na waasi wanaomuunga mkono aliyekuwa makamu wake Riek Machar.
Takriban watu 1,000 wameuawa tangu mapigano kuanza tarehe 15 Disemba
Vita vilianza baada ya Rais wa Sudan Kusini kumtuhumu bwana Machar kwa jaribio la mapinduzi, madai aliyoyakanusha.
Takriban watu 200,000 wameachwa bila makao,kutokana na vita hivyo vya wenyewe kwa wenyewe vinavyosemekana kutokana na ukabila.
Aidha Bwana Kiir anatoka kabila la Dinka naye hasimu wake bwana Machar akitoka katika kabila la Nuer.
Vyombo vya habari Sudan Kusini viliripoti kuwa Rais Bashir atakwenda Juba Jumatatu kujadiliana na Rais Kiir kuhusu mzozo huo ingawa hakuna taarifa zaidi zilizotolewa.
Awali msemaji wa wizara ya mambo ya nje mjini Khartoum alisisitiza kuwa Sudan ingependa kuona kipindi salama cha kutafuta mwafaka wa amani Sudan Kusini.
Hadi Ijumaa wiki mwishoni mwa wiki, mazungumzo ya amani mjini Addis Ababa,Ethiopia, yamekuwa yakiendeshwa na wapatanishi. Lakini sasa pande zinazozozana zinatarajiwa kuanza mazungumzo ya ana kwa ana.
Chanzo: BBC SWAHILI

Ajali ya meli Zanzibar....



WATU KADHA WANAHOFIWA KUFA MAJI BOTI YA KILIMANJARO II IKITOKEA PEMBA KUJA UNGUJA

Meli ya Kilimanjaro II iliyokumbwa na dharuba katika mkondo wa Nungwi ikitokea Pemba kuja Unguja inahofiwa abiria waliokuwa mbele wamedondoka baharini kati yao saba kati yao hawajulikani waliko.

Meli hiyo ilikumbwa na mawimbi makali katika mkondo huo mapema leo ikiwa na abiria mia nne na 29 wakiwemo watoto 60 na mabaharia wanane.

Akizungumza na Zanzibar Islamic news Blog kamishna wa polisi Zanzibar Hamdan Makame amesema baadhi ya abiria waliokumwemo ndani ya meli hiyo wamelalamika wenzao hawawaoni.

Aidha amesema wamepokea taarifa ambazo hazijathibitishwa zinazosema watu wanne wameokolewa na wamelazwa katika kituo cha afya Nungwi.

Hata hivyo baadhi ya abiria waliokuwemo ndani ya boti hiyo wamesema mawimbi hayo yamevunja viti vya mbele vya abiria huku baadhi yao wamedondoka baharini.

Waziri wa Miundombinu na Mwasiliano Rashid Seif Suleiman amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kundi la wazamiaji tayari wamekwenda katika eneo la ajali hiyo.

Amwekiri kuwa ni kweli amepokea maelezo kuwa watu saba waliokuwa wakisafiri na chombo hicho wamezama na hawajaonekana.

Waziri Seif amesema kamati ya ulinzi na usalama imekutana mchana huu na kujadili tukio hilo kabla ya kuelekea eneo la tukio kushirikiana na wataalam wengine kuwatafuta watu hao.

Niabu Mkurugenzi wa Upelelezi Makosa ya Jinai Zanzibar DCI Yussuf Ilembo amesema boti hiyo iliondoka majira ya asubuhi na ilipofika mkondo wa Nungwi ilipigwa wimbi kali na mashine kuzima.

DCI Ilembo amesema abiria waliokuwa wamekaa juu ya boti hiyo waliteleza na kudumbukia baharini wakiwemo watoto, tayari mpango wa kwenda katika eneo la tukio kuwatafuta kwa kushirikiana na wananchi utekelezaji wake umeanza.

Hata hivyo amesema uhakiki wa majina ya wahanga bado unaendelea ili kupata majina yao na umri wao kwa vile kuna meli mbili zilisafiri kwa wakati mmoja.

Kwa upande wake Mkurugenz wa Usafiri wa Baharini (ZMA) Mhandisi Abdi Maalim amesema mabaharia walianza kazi ya kuwatafuta watu wanaosadikiwa kuzama majira ya alasiri leo kwa kushirikiana na mabaharia wa kujitolea.

Afisa mmoja wa kampuni ya Azam Marine amesema chanzo cha tukio hilo ni dhoruba ilioambatana na upepo mkali uliotokea baharini na kuleta taharuki kwa wasafiri.

Wakati chombo kimezimika watu walikata maboya ya uokozi na mtafaruku wa abiria kutaka kujinusuru ulikuwa mkubwa ,chombo hakikuzama ,kimeendelea na safari na kifika katika bandari ya Malindi.

Ajali hiyo ni ya kwanza kutokea mwaka huu ambapo hadi leo alasiri watu walionekana kukaa katika vikundi vikundi na wengine kkufika kwa ajili ya kupokea ndugu zao bila ya kuwaona licha ya meli hiyo kushusha abiria

Wakati huo huo uongozi wa boti hiyo umesema unafanya tathimini ili kujua idadi ya abiria waliodondoka baharini wakati ilipokumbwa na mawimbi.

Nalo Jeshi la polisi Zanzibar kwa kushirikiana na Jeshi la polisi Makao makuu Dar es salaam wametuma helkopta katika eneo la tukio ili kubaini watu ambao wanadaiwa kuzama katika eneo hilo.

Meli hiyo iliwasili bandari ya Malindi majia ya saa 5.00 mchana na iliondoka kisiwani Pemba saa 2.00 asubuhi.

CHANZO:ZANZIBARISLAMICNEWS

Wednesday, January 1, 2014

Wasifu wa marehemu Dk Mgimwa


HISTORIA fupi ya Waziri wa Fedha wa Tanzania, Dr. William Mgimwa aliyefariki dunia nchini Afrika Kusini alipokuwa amelazwa kwa matibabu.

Kuzaliwa: Januari 20, 1950 Kalenga Iringa.

Elimu:
1966 - 1967 Shule ya Msingi Tosa

1961 -1965 Shule ya Msingi Wasa

1970-1971 Seminari ya Mafinga

1968 - 1969 Tosamaganga Sekondari

1975 - 1984 Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) - Postgraduate in Finance

1989 - 1991 IDM Mzumbe (MBA - Finance)


Ajira
1981 - 2000 - NBC Ltd (Mhasibu, Mhadhiri, Mkurugenzi, Mkurugenzi Mkuu)

2000 - 2010 - Chuo cha Benki Kuu ya Tanzania Mwanza (Mkuu wa Chuo)

2010 - 2013 - Mbunge, Kalenga (CCM)
Kufariki: Januari 1, 2014