Monday, July 13, 2015

Mganda aliyeua JWTZ alirudishwa kwao

Mganda aliyeua JWTZ arudishwa kwao
KAMPALA, Uganda
KIONGOZI wa kundi la waasi la Allied Democratic Forces (ADF) kutoka Uganda, Jamil Mukulu (51) amerudishwa kwao na kupokewa na  vyombo vya dola Ijumaa iliyopita akitokea Tanzania.
Mukulu alirejeshwa Uganda chini ya ulinzi mkali akapokewa na Jenerali wa Polisi (IGP) Kale Kayihura, mbele ya waandishi wa habari na kuwahakikishia kuwa haki itatendeka dhidi ya muasi huyo aliyezisumbua nchi za ukanda huu katika misitu ya Jamhuri ya watu wa Kongo (DRC).
“Maelfu ya familia za Uganda na DRC walipoteza ndugu zao kutokana na mtu huyu. Serikali ina deni kwao na sasa haki itatendeka,” alisema Kayihura ambaye kwa zaidi ya miaka 10 ameshiriki kumsaka Mukulu katika misitu ya Congo.
Aliongeza kuwa anaipongeza Serikali ya Tanzania kwa kumkamata mtu huyo hatari na kumfungulia mshtaka katika Mahakama zao kabla Uganda haijaomba arejeshwe ili wamfungulie mashtaka dhidi ya uhaini, ugaini na mauaji.
ADF chini ya Mukulu wanadaiwa kukishambulia kikosi cha kulinda amani cha JWTZ huko Congo na kuwaua askari wawili papo hapo. Jenerali Kayihura alisema, Mahakama ya Tanzania kwa kutambua kuwa Uganda kuna utawala wa sheria ilikubali ombo ya kurudishwa mshtakiwa huyo.
Baada ya mapigano ya muda mrefu Januari16, 2014, Jeshi la DRC lilianzisha Operesheni Sukola dhidi ya ADF na kuwatimua wanamgambo wake katika mapori walikokuwa wamejificha.
Aidha, mwanzoni mwa Aprili mwaka jana ngome kuu ya ADF iliyopo Madina ilisambaratishwa na kundi hilo kugawanyika, lakini kundi lililoongozwa na Mukulu lilifanikiwa kukimbia usiku wa manane.
Mukulu, ambayelengo lake kuu lilikuwa ni kumwondoa madarakani Rais Yoweri  Museveni na kumweka kiongozi wa Kiislamu, alitoroka na wapiganaji 30 wakiwamo maofisa wa juu 17 wa ADF pamoja na familia yake.
 
 
Hata hivyo historia ya muasi huyo inaeleza alikuwa Mkatoliki akifahamika kwa jina la David Amos Mazengo, kabla ya kubadili dini na kuwa Muislamu mwishoni mwa mwaka 1989.
Inaelezwa kuwa kamanda huyo wa ADF alipewa mafunzo na kundi la kigaidi la Al Qaeda huko Mashariki ya Kati ingawa Umoja wa Mataifa haujathibitisha iwapo ADF hupata misaada kutoka katika makundi ya kigaidi ya kimataifa.
Mwisho
 
 
 
Ugiriki yakubaliwa mkopo ukanda wa euro
BRUSSELS, Ubelgiji
VIONGOZI wa mataifa 19 yanayotumia sarafu ya Euro wamekubaliana kuisaidia Ugiriki kupata mkopo wa tatu ili ijikwamue na janga la kuporomoka uchumi.
Katika mkutano uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji jana Mwenyekiti wa Jumuiya ya Ulaya (EU), Donald Tusk alisemaviongozi wamekubaliana kwa pamoja kuisaidia Ugoriki.
Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Ugiriki, Alexis Tsipras baada ya mvutano mkali alisema taifa lake litapewa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Euri bilioni 35.
“Ugiriki haiwezi kuondoka kwenye ukanda wa Euro tena,” alisema mkuu wa kamisheni hiyo Jean-Claude Juncker akifuta minong’ono kuwa ikiwa mazungumzo hayatakwenda sawa Ugiriki itaondolewa kwene mataifa yanayotumia sarafu hiyo.
Tsipras alisema kwa kujiamini, “Kuondoka kwenye ukanda huu ilikuwa habari ya zamani tunaamini hivyo. Mkataba una masharti magumu lakini hatuna namna zaidi ya kukubali ili kujiokoa kiuchumi.”
Kwa upande wake kiongozi wa mawaziri wa fedha katika ukanda huo, Jeroen Dijsselbloem alisema kiasi cha fedha walichokopeshwa kinajumuisha Euro bil 50 zitakazoimarisha uwekezaji katika mali za nchi hiyo, ambapo bilioni 25 kati ya hizo itaimarisha huduma za kibenki.
Benki za Ugiriki zimefungwa kwa wiki mbili sasa ambapo miamala ya fedha katika mashine haitakiwi kuzidi Euro 60 kwa siku, hali hiyo imetajwa kuwa ngumu kuliko hali yoyote ya anguko la kiuchumi kuwahi kutokea hata kusababisha biashara nyingi kufungwa.
Hata hivyo uamuzi wa kuidhinisha mkopo huo si wa mwisho kwani vikao katika mabunge ya nchi wanachama lazima viamue kuidhinisha na kukubaliana kwa pamoja kuisaidia Ugiriki kwa mara ya tatu sasa.
“Bado safari ni ndefu ya kuamua juu ya makubaliano haya mazito,” alisema Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel jana asubuhi baada ya kutoka katika kikao.
Kwa upande wake Rais Francois Hollande wa Ufaransa alisema, “Maamuzi haya yamedumisha utu na mshikamano baina yetu nchi wanachama. Tumeonyesha kuwa Ulaya ina uwezo wa kumaliza matatizo ya ukanda wa sarafu ya Euro yaliyodumu kwa miaka saba sasa.”
Inaelezwa kuwa viongozi hao wamekaa katika meza ya mazungumzo mjini Brussels kwa zaidi ya saa 17 usiku mzima kuhakikisha mwafaka unapatikana kuisaidia Ugiriki iliyokumbwa na mdororo wa uchumi katika miaka ya hivi karibuni.
Majadiliano hayo yalianza Jumamosi kwa mkutano wa mawaziri wa fedha. Wakuu wa nchi walikutana Jumapili mchana na walijadiliana hadi Jumatatu alfajiri.
Mapendekezo yaliyowasilishwa na Tsipras yalihusisha utekelezaji wa hatua kali za kubana matumizi zikiwemo makato ya pensheni ya uzeeni, mageuzi ya masoko na ubinafsishaji mali za umma.
Mwisho
Somalia yaipeleka Kenya Mahakama ya Kimataifa
MOGADISHU, Somalia
SERIKALI ya Somalia jana imefungua kesi dhidi ya majirani zao Kenya katika Mahakama ya kimataifa (ICJ) kutokana na mgogoro wa mpaka baina ya nchi hizo.
Kwa mujibu wa taarifa za kuamini kutoka ndani ya serikali hiyo zinaeleza kuwa Somalia inailamu Kenya kwa kumiliki sehemu ya bahari iliyo ndani ya mipaka yake kwa njia isiyo halali.
“Mgogoro huu umekuwepo kwa miaka sita sasa, ni wa muda mrefu lakini mazungumzo ya ndani inaonekana yameshindikana ndio maana Somalia wameamua kulipeleka mahakamani,” alisema mtoa taarifa huyo aliyetaka hifadhi ya jina lake.
Somalia inaipeleka Kenya katika mahakama ya kimataifa huko The Hague Uholanzi kwa madai imekataa usuluhishi nje ya Mahakama.
Mgogoro huo umekuwa mkubwa baada ya kuwepo fununu za kupatikana utajiri wa mafuta na gesi katika sehemu hiyo ya bahari.
Mwisho
 

No comments:

Post a Comment