Friday, December 26, 2014

Ligi Kuu Tanzania Bara kuanza leo

Ligi kuu ya Tanzania bara, maarufu kama Ligi Kuu ya Vodacom inaanza rasmi mzunguko wa pili leo, Ijumaa baada ya kusitishwa tangu Novemba 7, 2014.
Hadi ligi hiyo ilipositisha mzunguko wa kwanza, tayari timu 14 zinazoshiriki ligi hiyo zilikuwa zimecheza michezo saba kila moja.
 
 
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Shirikisho la Kandanda nchini Tanzania, TFF, Simba ambayo ni miongoni mwa timu kongwe za ligi hiyo na ambayo katika mzunguko wa kwanza haikuwa na matokeo mazuri baada ya kwenda sare mara sita na kushinda mchezo mmoja na kujikusanyia pointi tisa ikishika nafasi ya saba katika msimamo wa ligi hiyo, leo inaikaribisha Kagera Sugar inayoshikilia nafasi ya tano katika pambano litakalofanyika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Michezo mingine itafanyika katika viwanja mbalimbali kuanzia Ijumaa, Jumamosi na Jumapili wiki hii.
 
 
Mpaka sasa Mtibwa Sugar ndiyo inayoongoza ligi hiyo ya Vodacom baada ya kujikusanyia pointi 15, ikifuatiwa na Young Africans(Yanga) kwa kuwa na pointi 13 sawa na Azam mabingwa watetezi.
Mbeya City iliyotikisa msimu uliopita na kupata mashabiki wengi nchini Tanzania, imejikuta ikizibeba timu zote baada ya michezo saba ikiwa na pointi tano tu ikitanguliwa na timu za Ndanda na Tanzania Prisons zenye pointi sita kila moja.
 
Hata hivyo mzunguko huu wa pili utakuwa na kivutio cha aina yake baada ya timu hizo kuruhusiwa kusajili katika dirisha dogo, ambapo Simba imeweza kusajili wachezaji wapya ndugu mahiri kutoka Uganda kina Sserunkuma.
Nao wapinzani wao wa jadi Yanga, imemtimua aliyekuwa kocha wake kutoka Brazil Marcio Maximo baada ya kufungwa mabao 2-0 na Simba katika mchezo wa Nani Mtani Jembe. Pia Yanga imesajili wachezaji mahiri akiwemo Amisi Tambwe ambaye katika mzunguko wa kwanza alichezea timu ya Simba lakini akaenguliwa katika usajili wa dirisha dogo.
Kinachosubiriwa na wapenzi na mashabiki wa timu hizo ni kwa kila timu kupata ushindi, kufikia ubingwa.

Mwaka 2014 ulikuwa mgumu kwa waandishi wa kimataifa


Kamati ya kimataifa ya kuwalinda waandishi wa habari, CPJ, imesema waandishi kiasi 60 waliuwawa kazini 2014 au kwa sababu ya kazi yao. Asilimia 44 ya waandishi walilengwa katika mauaji.
Kamati ya CPJ yenye makao yake makuu mjini New York nchini Marekani, imesema katika ripoti yake mpya iliyochapishwa leo kwamba idadi kubwa isiyo ya kawaida au takriban asilimia 20 ya waandishi waliouwawa walikuwa ni wa kimataifa, ingawa idadi kubwa ya waliotishwa iliendelea kuwajumuisha waandishi katika nchi zao za asili.
Miongoni mwa waandishi waliouwawa mwaka huu ni Anja Niedringhaus, mpiga picha wa shirika la habari la Associated Press aliyepigwa risasi alipokuwa akiripoti kuhusu uchaguzi wa Afghanistan.
Ripoti ya Kamati ya CPJ imesema idadi ya waandishi wa habari waliouwawa mwaka huu ilipungua kutoka 70 mwaka uliopita, lakini miaka mitatu iliyopita imekuwa mibaya zaidi tangu shirika hilo lilipoanza kuorodhesha matukio ya aina hiyo mnamo mwaka 1992.
Kriegsfotografin Anja Niedringhaus Archivbild 2005 Rom Anja Niedringhaus
Mzozo unaoendelea nchini Syria ambao sasa umeingia mwaka wa nne, umechangia kwa kiwango kikubwa. Ripoti hiyo imesema waandishi wapatao 17 waliuwawa mwaka huu, huku wengine wapatao 79 wakiwa wameuwawa tangu mapigano yalipoanza mwaka 2011.
Waandishi wa kigeni walilengwa
Syria imehusishwa na visa viwili vya kutisha vya mauaji ya waandishi wa habari mwaka huu, kuchinjwa kwa waandishi huria wa kimarekani James Foley na Steven Sotloff na kundi linalojiita Dola la Kiislamu. Wote wawili walikuwa wamepotea wakati wakiripoti kuhusu mzozo huo wa Syria.
Mzozo nchini Ukraine kati ya serikali mpya na wanamgambo wanaoungwa mkono na Urusi ulisababisha waandishi watano na wafanyakazi wawili wa vyombo vya habari kuuwawa wakati mahusiano kati ya Urusi na mataifa ya magharibi yalipoporomoka na kufikia kiwango cha chini kabisa tangu kumalizika kwa vita baridi. Mauaji hayo yalikuwa ya kwanza kurekodiwa na kamati ya CPJ nchini Ukraine tangu mwaka 2001.
Siku 50 za vita katika Ukanda wa Gaza kati ya Israel na Wapalestina wakati wa msimu wa kiangazi zilisababisha waandishi wapatao wanne na wafanyakazi wengine watatu wa vyombo vya habari kuuliwa, akiwemo mpiga picha wa shirika la habari la Associated Press, AP, Simone Camili na mkalimani Ali Shehda Abu Afash, waliouwawa na mlipuko wa mabaki ya bomu.
James Foley Journalist Reporter James Foley
Takwimu kuhusu vifo
Nchini Iraq, waandishi wasiopungua watano waliuwawa, watatu kati yao walipokuwa wakiripoti mapambano dhidi ya kundi la Dola la Kiislamu, wakati lilipokuwa likiyateka maeneo ya kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Ripoti ya CPJ inazungumzia mauaji ya kwanza ya waandishi wa habari katika kipindi cha miaka kadhaa katika baadhi ya nchi, zikiwemo Paraguay, ambako vifo vitatu viliripotiwa kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 2007 na Myanmar, ambako kuuliwa kwa mwandishi wa habari aliyekuwa akizuiliwa, ni kifo cha kwanza tangu mwaka 2007.
Kamati ya CPJ pia imeripoti mauaji ya kwanza ya mwandishi wa habari katika Jamhrui ya Afrika ya Kati, ambayo imegawanyika kutokana na machafuko kati ya Wakristo na Waislamu. Na hata kuripoti mapambano dhidi ya ugonjwa hatari wa Ebola kumesababisha vifo vya waandishi huku maiti za mwandishi na wafanya kazi wawili wa vyombo vya habari ikipatikana katika kijiji kimoja nchini Guinea, ambako walikuwa wamekwenda kuripoti kuhusu kampeni ya uhamasishaji wa umma.
Kamati ya Kimataifa ya kuwalinda waandishi wa habari CPJ, inasema inachunguza vifo vya waandishi wapatao 18 mwaka huu. Shirika hilo halihesabu vifo vinavyotokana na magonjwa au ajali ya magari au kuanguka kwa ndege mpaka ajali hizo ziwe zilisababishwa na hatua za uchokozi.

Wednesday, December 10, 2014

Ummy Mwalimu afanya ziara katika kiwanda cha Plastic cha OK jijini.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu, jana alifanya ziara ya ukaguzi wa mazingira katika kiwanda cha OK Plastic, kilichopo jijini Dar Es Salaam. Ziara hiyo ni muendelezo wa ziara za kuangalia hali ya mazingira kwenye viwanda mbalimbali hapa Nchini.


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalim akielekeza jambo wakati wa ziara ya kutembelea kiwanda cha OK Plastic kilichopo jijini Dar Es Salaam.


  Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu akimsikiliza Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais Bi Magdalena Mtenga wakati wa ziara hiyo.



 Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu akiangalia jinsi betri chakavu zinavyohifadhiwa kiwandani hapo.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (wa kwanza kushoto) akipata maelezo ya uendeshaji wa kiwanda cha OK Plastic kutoka kwa Menejimenti ya kiwanda hiko.

Wengine wanaofuatia ni Mkurugenzi Msaidizi-Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais bi Magdalena Mtenga, Bwana Anacleto Pereira Mkuu wa Idara ya sheria wa OK plastic, Fadl Ghaddar Mkurugenzi Mtendaji wa OK plastic na Martin Msamba Meneja wa kiwanda.



Ziara ya naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira

 Ofisa Uhusiano wa kampuni ya SBS, Geofrey Kanenge  (katikati) akitoa maelezo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (Mb) (wa pili kushoto)  kuhusu udhibiti wa utiririshaji wa maji taka yatokanayo na usafishaji wa mapipa yenye kemikali unavyofanywa na kampuni hiyo wakati wa ziara ya ukaguzi wa mazingira mkoani Mtwara.

 Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (katikati) akipata maelezo kuhusu ubanguaji wa korosho kutoka kwa Uongozi wa Kiwanda cha Micronix  kilichopo mkoani Mtwara wakati wa ziara aliyoifanya mkoani humo.

 Sehemu ya Wananchi wakimsikiliza Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kukagua hali ya Mazingira ya viwanda  aliyoifanya mkoani Mtwara.





Eneo la bwawa la asili la Mdenga lililofukiwa kinyume cha sheria na kampuni ya SBS inayojishughulisha na urejelezaji wa taka mkoani Mtwara na kusababisha uharibifu wa mazingira katika eneo hilo.


Tuesday, December 2, 2014

Aliyewakosoa Sasha na Malia ajiuzulu


WASHINGTON, Marekani
 
Mfanyakazi katika chama cha Republican nchini Marekani amejiuzulu baada ya kukosolewa kwa kuwatuhumu wanawe Rais wa Marekani Barack Obama , Sasha na Malia kwa kuwaambia kuwa wamekosa ustaarabu.
Elizabeth Lauten, afisaa mkuu wa mawasiliano wa mwanasiasa mkuu wa chama hicho, Stephen Fincher, alijiuzulu Jumatatu.
Bi Lauten, aliwakosoa watoto wa Obama Sasha na Malia kwenye ukurasa wake wa Facebook baada ya watoto hao kuonekana wakiwa wamevalia sketi fupi kwenye hafla ya jioni.
 
 
Baadaye Lauten alifuta maandiko yake ambayo baadaye aliyataja ya kuumiza moyo na kuudhi.
Bi Lauten pia alikuwa amewakosoa Sasha na Malia kwa kusema walionekana wasio na furaha walipokuwa wamesimama na baba yao katika hafla ya maankuli katika Ikulu ya White House.
Wakati watu wengi walihisi kwamba Sasha na Malia hawakua na furaha kuwa na baba yao katika hafla ile na hata kulizungumzia swala hilo kwenye mitandao ya kijamii,Bi Lauten aliamua kujitoa kimasomaso na kuwakosoa wasichana hao kupitia kwa Facebook.
 
 
Mwanamke huyo akiomba msamaha, alisema baada ya kufanya maombi na hata kuzungumza na wazazi wake na kisha kusoma maandiko yake kuwahusu Sasha na Malia, alihisi kweli aliwakera wasichana hao.
"ningependa kuomba radhi kwa wote niliowaudhi kwa matamshi yangu, na nina ahidi kujifunza na kubadilisha mwenendo wangu, '' alisema Lauten.
Chanzo: BBC Swahili.

Al Shabaab waua 36 Mandera,Kenya


NAIROBI, Kenya
Kundi la wanamgambo nchini Somalia Al Shabaab limekiri kuwaua watu 36 katika shambulio lililotokea kwenye machimbo ya kokoto karibu na mji wa Mandera kaskazini mwa Kenya.
Katika taarifa iliyotolewa kwenye mtandao wa kundi hilo, wanamgambo hao wamesisitiza kuwa ndio waliowaua wakenya hao kwa sababu ya majeshi ya Kenya kuendelea kuwa nchini Somalia.
Taarifa za mauaji hayo zilitolewa kwa mara ya kwanza na Shirika la Msalaba Mwekundu.
Inaarifiwa kuwa wafanyakazi hao walipigwa risasi wakiwa katika mahema ya. Walioshuhudia shambulizi walisema kwamba wapiganaji hao waliwatenga waisilamu na wakristo huku wakiwachinja baadhi, na kuwapiga risasi wlaiosalia.
Wakazi wa eneo hilo wamesema waathirika wote wa tukio hilo ni watu wasio Waislam ambao walikuwa wakifanya kazi katika machimbo hayo yaliyopo Kormey kilomita 15 kutoka mji wa Mandera Kaskazini mwa Kenya.
Tukio hili linafuatia tukio la wiki moja iliyopita ambapo watu wapatao 28 waliuawa katika shambulio la basi la abiria huko Mandera.
 
Kundi la wapiganaji wa Kiislam la Al Shabab wamekiri kuhusika na mauaji hayo.
Mkuu wa Polisi eneo hilo, amesema bado wanafuatilia tukio hilo.
Katika tukio lingine, mtu mmoja ameripotiwa kuuawa nchini Kenya kufuatia mlipuko katika klabu moja ya usiku katika mji wa Wajir kaskazini mwa Kenya.
 
Kwa mujibu wa Kamishna wa Polisi wa Wajir, Frederick Sishia, shambulio hilo limefanyika saa mbili usiku na kuua mtu mmoja na watu wengine wanne wamejeruhiwa.
Washambuliaji hao walitumia magruneti na silaha nyingine za kijeshi kufanya shambulio hilo.
Wiki iliyopita watu wengi waliuawa eneo la Mandera kaskazini mwa Kenya.
Kenya imejikuta ikilengwa na mashambulio ya kigaidi tangu majeshi yake yapelekwe nchini Somalia kukabiliana na wapiganaji wa Al Shabab. Mbali na miji ya kaskazini mwa Kenya kushambuliwa kila mara, miji mikubwa nchini humo ya Nairobi na Mombasa imekuwa ikilengwa na mashambulio ya kigaidi.
Chanzo: BBC Swahili

Jela miaka 50 kwa kuwaharibu watoto Kenya






NAIROBI, Kenya
Mahakama nchini Kenya imemhukumu kifungo cha miaka 50 jela raia mmarekani kwa kutengeza na kusambaza picha chafu za video za watoto wakifanya vitendo vya ngono.
Terry Ray Krieger alikiri makosa yake mbele ya mahakama mwezi jana. Pia alipatikana na kosa la kuwadhalilisha watoto wadogo huku akinasa vitendo hivyo kwa kanda ya video.
Alikamatwa na maafisa wa usalama Kenya baada ya kupata taarifa kutoka kwa shirika la kimataifa la polisi kwamba alikuwa anasambaza video hizo zilizokuwa zinaonyesha watoto wakifanyiwa vitendo vichafu kwenye mtandao.
Krieger amewahi kushtakiwa kwa makosa sawa na hayo na kufungwa jela nchini Marekani miaka 20 iliyopita.
Polisi wa Kenya walipokea taarifda kutoka kwa polisi nchini Marekanmi wakiwaamiwa kuwa kuna raia mmarekani nchini Kenya anayetengeza na kusambaza video chafu za watoto wadogo wakihishwa na vitendo vya ngono.
Aliomba mahakama kumuonea huruma kutokana na maradhi anayougua ya mifupa lakini mahakama ilisema kuwa maradhi yake sio haiwezi kuwa sababu ya kutowajibishwa kwa makosa yake.
Chanzo: BBC Swahili