Saturday, June 30, 2012

Dr Asha Rose Migiro aagwa rasmi na kupewa shavu jingine la mjumbe maalum wa masuala ya UKIMWI barani Afrika.


Na Mwandishi Maalum

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amemteua Naibu Katibu Mkuu anayemaliza muda wake, Dkt, Asha-Rose Migiro kuwa  mjumbe wake maalum katika masuala yaukimwi na ugonjwa wa ukimwi Barani Afrika. 

Ban Ki Moon ametangaza uteuzi huo wakati wa hafla maalum aliyoiandaa mahsusi kwaajili ya kumuaga  Naibu Katibu Mkuu wake ambaye anahitimisha  utumishi wa  miaka mitano na nusu   katika nafasi yake.


Hafla hiyo imefanyika   siku ya alhamisi katika viunga vya Umoja wa Mataifa, na kuhudhuriwa na wageni waalikwa  mbalimbali wakiwamo mabalozi na wakuu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa.

“Ninatangaza rasmi kwamba ninamteua Dk.  Asha- Rose Migiro kuwa  mjumbe wangu maalum katika masuala ya ukimwi na ugonjwa wa Ukimwi Barani  Afrika," alisema Ban Ki Moon huku akishangiliwa kwa nguvu na wageni waalikwa.


Akiongea kwa hisia, Ban Ki Moon, ameeleza kwamba ingawa Migiro alikuwa naibu wake, lakini amekuwa mwalimu kwake kwani amejifunza mengi kwa kipindi alichokaa nae na daima ataendelea kuenzi mchango wake mkubwa.

“ Kama ni kuvaa viatu vyake, naweza kusema ningechekesha sana,  kwa ufupi siwezi kuvaa viatu vya Migiro, amekuwa msaada mkubwa sana kwangu, ameniwakilisha vema kila mahali nilipomtuma hata katika mazingira magumu na ya hatari,  kote ameniwakilisha vema sana, kama  mwalimu wangu, ni kama profesa wangu anastahili alama ya juu sana” akasema  Ban Ki Moon na kushangiliwa.

Akamuelezea  Migiro kama kiongozi si tu mwadilifu, lakini mwanadiplomasia  aliyebobea aliyefanya kazi kubwa ngumu na nzito kwa moyo mkunjufu, uhodari, umakini na uadilifu wa hali ya juu sana.

“ Siyo rahisi kuelezea yale aliyoyafanya nyuma ya pazia, namna gani alivyochapa kazi kwa nguvu, yapo mengi makubwa ambayo Migiro ameyafanya na  kuyakamilisha kwa uadilifu wa hali ya juu. Migiro ni mwanadiplomasia aliyebobea lakini ni mtu wa vitendo, vitendo ambavyo lazima utaona matunda yake” akabainisha Ban Ki Moon.

Akaongeza “Migiro amefanya kazi na viongozi wagumu,  akiwamo aliyekuwa  Rais wa Libya Muammar  Quadaff aliyethubutu hata kumrushia katiba ya Umoja wa Mataifa amezikuna nyonyo za watu wengi wakiwamo watu wanyonge na wenye matatizo mbalimbali. Migiro  unaondoka, lakini Umoja wa  Mataifa hautasahau mchango wako. Hapa ni nyumbani kwako, na nitaendelea kuomba msaada wako na ushirikiano wako, bado nitaendelea kukuhitaji” akasisitiza Ban Ki Moon.

nae Dk Migiro alimshukuru kiongozi huyo wa umoja wa mataifa na kuita uteuzi wake ni wa heshima na suala la UKIMWI lipo moyoni mwake atalitumikia kwa uwezo wake wote.

"Masuala ya  ukimwi na ugonjwa wa ukimwi, ni eneo ambalo limo ndani ya moyo wake na kwamba nashukuru kuona kwamba Katibu Mkuu ameniamini kwamba naweza kumsaidia, naahidi nitalitekeleza  jukumu  hilo kwa heshima  kubwa".

Hafla hiyo pia imehudhuriwa  na familia ya Naibu Katibu Mkuu ikijumuisha  mume wake, Profesa  Cleophas Migiro,  mdogo wa  Naibu Katibu Mkuu, Bi. Amina  Mtengeti na mtoto wa  mwisho wa Migiro Chansa Jasmin.

Asha-Rose Migiro anakuwa mwanamke wa pili kushika wadhifa huo na mwanamke mwafrika wa kwanza. Lakini pia ni naibu katibu mkuu ambaye amehudumu katika wadhifa huo kwa miaka mitano na nusu.

No comments:

Post a Comment