Thursday, June 28, 2012

Watoto wa Sultan waliopinga mapinduzi wakidharauliwa watauvunja muungano




 Na Hafidh Kido

Abdulrahman Mohammed babu aliekuwa kiongozi wa chama cha kisiasa cha UMMA Party kabla ya mapinduzi ya Zanzibar wakati akizungumzia vuguvugu la mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 katika kitabu chake cha ‘Husuda ya Marekani dhidi ya mapinduzi ya Zanzibar. Siku 100 za kuundwa kwa Tanzania’ alisema usiku wa tarehe 11 Januari, mwaka 1964 katika hali ngumu ya maisha vijana wa mitaani watoto wa makabwela wasio na kazi waliamua kuingia mitaani na kufanya vurugu kupinga uongozi wa kisultani.

Katika kitabu hicho Babu alielezea ushiriki wa mapinduzi kwa vijana wa Unguja ambao hawakufurahishwa na utawala wa kiarabu kuendelea kushikilia uchumi wa visiwa hivyo mbali ya kupata uhuru mwaka 1963. 

Miezi michache iliyopita tumeshuhudia viongozi wa chama cha kiislam cha muamsho walivyofanya vurugu katika visiwa hivyo kwa madai ya kuitaka Zanzibar ijitenge na Tanzania bara ili kuepuka baadhi ya mambo waliyoyaita ukiukwaji wa maadili ya Mzanzibari na hali mbaya ya maisha inayosababishwa na kunyonywa katika mgawo usio halali katika keki ya taifa.

Lakini cha kushangaza siku chache baada ya vurugu zile zilizosababisha hasara kubwa kwa wamiliki wa sehemu za starehe, makanisa na watu kutoka Tanzania bara watu wasiojulikana walitoa waraka wa kupinga vurugu zile na kuziita ni za wapemba wasio na uchungu na visiwa hivyo kwani wanataka muungano uvunjike ili uongozi wa kisultani urudi Zanzibar.

Waraka huo uliotolewa na watu waliojiita waunguja umewashutumu watu wanaotoka kisiwa cha Pemba kuwa si wenyeji wa ukanda huu wa Afrika ya Mashariki na ni wamakonde kutoka sehemu za Pemba nchini Msumbiji, na ndiyo maana kipindi cha mapinduzi hawakuwa upande wa wanamapinduzi badala yake waliunga mkono utawala wa Sultan Jamshid.

Sehemu ya waraka huo inasema “Watu wa Unguja tunatoa ujumbe makhsusi kwa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania  Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, sisi watu wa Unguja tumechoka kuishi na Wapemba katika kisiwa chetu cha Unguja, kwani ni watu wasio na fadhila ya aina yoyote, hivyo tunakuomba Mh. Rais wa jamhuri fanya mazungumzo na Mh. Rais wa Zanzibar na ifikie hatua maalim Seif Sharif Hamadi apewe kisiwa chake cha Pemba na akatawale wapemba wenziwe.”

Taarifa hiyo ya kurasa moja iliendelea kueleza “Hapo siku za nyuma wapemba walidai kisiwa chao na nyinyi viongozi mkang’ang’ania kuwa hatuwezi kuvunja umoja sasa mnawaona hao tayari wameanzisha chama cha kisiasa cha ‘Muamsho’ kwa kisingizio cha dini.”

Utaona kuna hali ya kuchanganya mada hapa na haijulikani kuwa hii hoja ya kutaka muungano uvunjwe ina baraka za visiwa vyote viwili vya Unguja na Pemba ama la. Na ikiwa hoja hii inatoka kwa watu kutoka kisiwa kimoja tu cha Pemba inamaana zile tetesi za kutaka kumrudisha Sultani Jamshid ambae kwa sasa anaishi uhamishoni nchini Uingereza zina ukweli ndani yake.

Waraka huu unaodaiwa kutolewa na watu toka kisiwa cha Unguja kwa sababu haukutiwa saini na mtu yeyote inawezekana ni njia za serikali kuu kupoteza lengo la watu wa visiwani kupinga muungano ama inawezekana ni kweli hakuna maelewano na muafaka wa visiwa viwili hivi katika kupinga muungano.

Binafsi nilibahatika kukaa Unguja kwa miezi miwili nikifanya mazoezi ya habari TVZ mwaka 2007, nilichojifunza ni kuwa kuna mpasuko mkubwa baina ya watu wenye asili ya Unguja na Pemba. Hakuna mahusiano mazuri kama watu wengi wanavyodhani.

Waunguja wanajinasibu na hekima, utu na busara ya kutafakari mambo. Wapemba wanaonekana daima ni wapinzani na watu wenye chembechembe za uarabu kadhalika ni watu wenye hasira za haraka na huchukua maamuzi bila ya kutafakari. Hii ni tafsiri yangu baada ya kukaa Unguja kwa miezi hiyo michache, sijawahi kufika kisiwa cha Pemba lakini waliofika wananiambia kuna athari kubwa ya watu wenye asili ya uarabu kuliko waafrika.

Na ndiyo maana hata Rais wa kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ndugu Abeid Amani Karume inadaiwa alikuwa hana mapenzi na watu kutoka kisiwa cha Pemba. Alifikia kusema mpemba hatoshika uongozi wa juu katika visiwa vya Zanzibar, cheo cha mwisho kwa mpemba ni mwalimu mkuu wa shule.

Lakini cha ajabu mara hii viongozi wawili wa juu kabisa wanatoka kisiwa cha Pemba. Rais na Makamu wa kwanza wa Rais wote ni wapemba. Nadhani watu kutoka Pemba walitegemea makubwa kwa matokeo hayo lakini kinyume chake hakuna lolote lililobadilika zaidi ya wapemba kuendelea kukandamizwa.

Kudhihirisha chuki dhidi ya mapinduzi watu wenye asili ya kisiwa cha Pemba kwa muda mrefu wamekuwa wakipinga kitendo cha watu wa Unguja kupindua serikali ya Sultan Jamshid Bin Abdullah al-Said, chini ya waziri mkuu Mohammed Shamte.

Mwandishi wa kitabu cha ‘Ukweli ni huu kuusuta uwongo’ Amani Thani Fairooz, alichokiandika akiwa uhamishoni katika falme za kiarabu mwaka 1995; anaandika “Matunda makubwa waliyopata wananchi wa visiwani Unguja na Pemba kutokana na hayo yenyekuitwa ‘mapinduzi’, ni shida za kimaisha katika kila upande. Vyakula havinunuliki, nguo hazikamatiki mradi wananchi wamo katika kuhiliki kwa maisha yalivyo magumu . Vijana wamekuwa wazee kwa shida,” uk. 15.

Fairooz anaendele kuandika katika kitabu hicho kuhusu mapinduzi; “Mafisadi wachache kwa ajili ya maslahi ya nafsi zao hawakutahayari kuchanganyika na wageni waliokuwepo ndani ya nchi na walioletwa kutoka nchi jirani kwa makusudio khasa ya kuivamia Zanzibar na kuiondoa Serikali ya wananchi. Wananchi mafisadi hao walikubali kuongozwa na wageni, John Okello aliyetoka kwao Uganda, Injinia aliyetoka kwao Kenya na Mfaranyaki aliyetoka kwao Tanganyika, kuivamia nchi yao katika usiku wa manane wa kuamkia taarikh 12 Januari 1964.

“Wananchi, mafisadi kwa sababu ya maslahi ya nafsi zao hawakuhisi uchungu kuipoteza nchi yao, wala kuzipoteza roho za wazee wao, za ndugu zao na za marafiki zao….. ukatili, ushenzi na unyama uliofanywa katika visiwa hivi vilivyokuwa na ustaarabu wa kupigiwa mfano, hauwezi hata kuhadithika.”

Ukitazama maneno yaliyo katika kitabu cha Abdulrahman Babu miongoni mwa waasisi wa mapinduzi na mwenye asili ya Unguja, ukipambanisha na maneno yaliyo katika kitabu cha Amani Fairooz mwenye asili ya Pemba na mpinga mapinduzi utaona ni namna gani visiwa hivi viwili vilivyo na mitafaruku ya kikanda tangu zamani.

Kilichotokea kipindi cha utawala wa Kisultani ni watu wenye asili ya kiarabu, kihindi na kizungu kupewa kipaumbele katika masuala ya kimaendeleo lakini waafrika ama ‘Magozi’ kama walivyokuwa wakiitwa na watu wenye asili ya kiarabu walikuwa wakidharauliwa na kutengwa.

Wakwezi na wakulima lilikuwa ni jina la watu toka Unguja ambao ndiwo walionekana kuwa na uchungu sana kwa hali duni za kimaisha. Wakati wa vuguvugu visiwani humo watawala wa kiingereza walikuwa mbioni kuachia madaraka kwa wazalendo baada ya kufanya hivyo kwa nchi jirani za Afrika ya mashariki. lakini utaratibu uliotakiwa kutumika ilikuwa ni kupiga kura.

Kulikuwa na pande mbili zilizokuwa zikivutana kwa karibu vyama viwili vilivyoungana vya ZPPP (Zanzibar and Pemba People’s Party) na ZNP (Zanzibar Nationalist Party) maarufu kama Hizbul-Wattan, dhidi ya chama cha ASP (Afro Shirazi Party) chama kilichokuwa na watu wengi kutoka Unguja.

Muungano wa ZPPP/ZNP ulifanikiwa kushinda uchaguzi wa mwaka 1961, June kwa kupata viti 13 dhidi ya ASP waliopata viti 10. Ndipo ZPPP/ZNP walipounda serikali ya madaraka. Lakini tatizo likawa ni mgawanyiko wa wananchi juu ya nani akabidhiwe uhuru kutoka kwa waingereza.

Zanzibar haikuwa na utulivu kisiasa, wapemba walikuwa tayari kwa uhuru ila waunguja hawakuwa tayari. Sultan hakuwa na la kusema kwani kimsingi yeye angeendelea kutawala visiwa hivyo hata kama waingereza wangeondoka.

Baada ya mvutano wa kuunda katiba ya Zanzibar  ili wakabidhiwe uhuru wao, Machi na April 1962 huko Lancaster House, London baina ya upinzani na serikali ya madaraka lakini mazungumzo hayakufikia mwisho yakavunjika.

ASP ambao walikuwa ni upande wa upinzani walisusia mazungumzo yoyote ya kutangazwa tarehe ya uhuru mpaka ufanyike uchaguzi mwengine kwani kwa maelezo yao hawakuridhishwa na matokeo ya uchaguzi uliowaweka madarakani ZPPP/ZNP.

Baada ya mazungumzo ya muda mrefu vyama vyote vilikubaliana uchaguzi urudiwe, ndipo mwaka 1963, Julai ukaitishwa uchaguzi mwingine na muungano wa ZPPP/ZNP wakashinda tena viti 18 dhidi ya ASP iliyopata viti 13.  

 Serikali ya Uingereza ikawaita kwa mara nyingine wapinzani na viongozi wa serikali ya Zanzibar kuenda Uingereza kuzungumzia tarehe ya uhuru, mambo yalikwenda vizuri na ASP walikubali shingo upande muungano wa ZPPP/ZNP kupewa uhuru. Ndipo ikapangwa
10 December, 1963 kuwa tarehe ya uhuru wa Zanzibar chini ya waziri mkuu Mohammed Shamte na kiongozi wa nchi Sultani Jamshid al-Said.

Kilichowafanya watu toka Unguja kupinga uhuru huo ilikuwa ni kile kitendo cha Zanzibar kuendelea kutawaliwa na waarabu. Yaani walikuwa wakifuata mfumo wa kiingereza Sultan angekuwa mkuu wa nchi ambae atakuwa wa maisha akiendeleza ukoo wa kisultani, lakini Waziri mkuu atakuwa akichaguliwa kila baada ya muda fulani uliopangwa katika katiba ya Zanzibar. Kihalisi huo haukuwa uhuru bali kiini macho tu.

Ndipo ASP baada ya mwezi mmoja tu tangu Zanzibar kupata uhuru walifanya mapinduzi na kuungoa utawala wa kisultani nchini humo. Sasa ninaposikia mtu kutoka Zanzibar anapinga mapinduzi nakuwa simuelewi.

Hivyo naiasa serikali ya Tanzania chini ya Rais Kikwete, kuacha kudharau hizi vurugu za vikundi vya waislam kwani kirahisi tu vinaweza kuchota fikra za wazanzibari wote maana hata kipindi cha mapinduzi walioanza chokochoko ni vijana wa mitaani tu baadae kina Karume wakaingilia kati baada ya kuona mambo yamenoga. Huwezi kujua hata ndani ya Serikali ya mapinduzi Zanzibar kuna viongozi wakubwa wanataka muungano uvunjwe wanasubiri gari ikolee kasi ili wadandie.

Naomba kuwasilisha
lor ' c ;

No comments:

Post a Comment