Thursday, June 28, 2012

Waandishi wasikubali kulazimishwa kuandika kisichosomeka



Na Hafidh kido
Mwalimu wangu wa somo la “issues in mass communication” Mohammed Matovu, aliwahi kutuuliza darasani ni nani adui mkubwa wa vyombo vha habari, ni serikali ama mashirika ya matangazo (Advertising companies). Kila mmoja alikuwa na jibu lake, lakini jibu langu lilikuwa ni mashirika ya matangazo ndie adui mkubwa wa vyombo vya habari, na mwalimu wangu akanipongeza kwa jibu zuri.
Sitofafanua jibu langu kwani leo sijakusudia kuogelea katika bahari hiyo ambayo wajuzi wa taaluma hii wanajua namna kina chake kilivyo kirefu.
Nina miezi kadhaa tangu nimalize shahada yangu ya mawasiliano ya umma nchini Kampala, Uganda. Bado nina zile chembechembe za kiuanafunzi, napenda sana kulumbana na hasa nikiona kitu ambacho kinagusa taaluma yangu ya uandishi. 
Miezi kama mitatu iliyopita nilisoma katika gazeti kuhusu taarifa za kushughulikiwa wahariri wawili wa shirika la utangazaji Zanzibar, Zanzibar Broadcasting Cooperation (ZBC), kwa kosa la kumbagua Rais Shein kwa kumwandika kwa uchache kuliko inavyotoa taarifa zinazomuhusu makamu wa kwanza wa Rais Seif Sharrif Hamad.
Wahariri hao wawili Juma Mohammed Salum na Ramadhan Ali walihamishwa kutoka ZBC makao makuu ambayo zamani ikitambulika kama Televisheni ya Zanzibar (TVZ) iliyopo Karume House, karibu na Hospitali ya mnazi mmoja Unguja. Na kuhamishiwa idara ya habari (MAELEZO) ya Zanzibar, ambayo ni ofisi ya chini ukilinganisha na ZBC.
Huku ni kukosa uzalendo na kupungukiwa akili, mtu ambae alikuwa anahariri habari za shirika la utangazaji katika nchi (Zanzibar), leo hii unampeleka eneo ambalo atakuwa anasimamia upokeaji na usambazaji wa taarifa za habari, tena zisizohaririwa, kwasababu tu anatuhumiwa kuhujumu matukio ya kihabari ya Rais. Maana kazi ya kuhariri inahitaji uwezo wa hali ya juu, na ninaamini mpaka wizara inawateua ni wazi uwezo wao ni wa hali ya juu.
Alipoulizwa na waandishi wa habari mjini Zanzibar katibu mkuu wa wizara ya habari, utamaduni, utalii na michezo ya serikali ya Umoja wa kitaifa Zanzibar Ali Saleh Mwinyikai, kuhusiana na sakata hilo alisema kosa kubwa la wahariri hao Juma Mohammed Salum (mhariri mkuu) na msaidizi wake Ramadhan Ali, ni kuvuruga ama kutofuata maelekezo ya namna ya kuripoti habari za viongozi.
Yaani kitendo cha kuandika sana habari za makamu wa pili wa Rais Zanzibar na kuandika kwa uchache matukio ya Rais Dk Ali Mohammed Shein, ndilo kosa hasa lililowafanya wahariri hawa kufukuzwa katika nafasi zao na kuwekwa watu wengine wanaojua kumpamba Rais.
Taarifa hizo si tu zinanifanya nianze kubadili fikra na kuanza kuamini kuwa adui mkubwa wa vyombo vya habari ni serikali iliyo madarakani, lakini zinamdhalilisha Rais Shein kwa kumuweka katika kundi la watu wanaopenda kuonekana katika vyombo vya habari hata akiwa analisha kuku wake wa kufuga pale Ikulu. Kwani wahariri hawa wamepewa karipio kali na serikali ya mapinduzi Zanzibar kwa kosa la kutomuandika sana muheshimiwa, na badala yake kumuandika msaidizi wake ambae ni mpinzani asiefaa kuonekana kwenye luninga.
Katika taaluma ya habari suala hilo tunaliita ‘conflict of interest or ethical dilema’ yaani ni kugongana kwa maslai ama kuweka rehani maadili ya kitaaluma.
Haiyumkiniki  kumfundisha mtu kazi usiyoiweza. Kwasababu sitaki kuamini kinachozungumzwa, kwani mwandishi yeyote wa habari hupenda vitu viwili katika vingi.
Kwanza mtu ambae habari inamuhusu awe maarufu; kitu ambacho naamini Dk Shein anacho ni Rais wa nchi ni maarufu kila mmoja anataka kusikia ama  kuona kutoka kwake. Kitu cha pili tukio liwe si la kawaida, la kuogofya, kuhuzunisha, kutia moyo kupita kiasi ama linahusu maslahi ya taifa, kitu ambacho sidhani ikiwa Dk Shein atahusika katika tukio moja kati ya hayo wahariri wale wangeache kutoa habari zake.    
Maana ya kusema hayo ni kuwa, mpaka Rais anakosa kuonekana katika vyombo vya habari ni kuwa hatengenezi tukio ama wazungu wanaita (he does not make news). Seif kwa kuwa alipambana kuipata nafasi hiyo kwa miaka mingi ni wazi wananchi wa Zanzibar na dunia wanataka kuona utekelezaji wake kama miongoni mwa viongozi wa juu katika nchi ambayo ilimtesa na kumnyanyasa mpaka kufikia hapo.
Hii inanikumbusha tukio la mwaka jana pale mkurugenzi wa Tanzania Broadcasting Cooperation (TBC) ndugu Tido Mhando, alipokutwa na masaibu kama hayo ya kutimuliwa katika nafasi yake kwasababu tu wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, alikuwa akitoa sana taarifa zinazohusu mikutano ya CHADEMA kuliko CCM.
Inatia kinyaa sana kuona serikali yetu inafanya vitu vya hovyo kwa watu wenye uwezo wa kipekee katika taaluma mbalimbali kwa kutaka kuwaridhisha wanasiasa.
Naamini kwa uwezo wake wa hali ya juu katika taaluma ya habari Tido Mhando, asingeweza kuwapa ‘coverage’ kubwa CHADEMA na kuwaacha CCM, ikiwa CCM ‘wana-make news’ ni wazi chama hicho kikongwe hakikuwa na sera yoyote mpya katika uchaguzi ule. Kitu ambacho kiliwafanya waonekane kwa uchache sana katika chombo hicho cha taifa.
Sote tunakumbuka mwanzoni mwa mwaka 2006 mara baada ya Rais Kikwete kuingia madarakani kila chombo cha habari wakati wa jioni lazima kianze na habari inayomuhusu Rais. Hata kama habari hiyo haikuwa na maana yoyote ni lazima itawekwa ya kwanza.
Mpaka ikafika mahali watu wakawa wanakejeli vyombo vya habari kila ifkapo saa mbili usiku wakati wa taarifa ya habari ya siku nzima. Habari ikianza tu utasikia watu wakikejeli ‘Rais kikwete….’ Yaani ni lazima mtangaji atataja jina la Rais Kikwete ndipo aendelee na habari nyingine.
Lakini baada ya Tido Mhando kukabidhiwa TBC kitu cha kwanza kufanya ni kuliondoa shirika hilo katika uangalizi wa Serikali yaani liwe shirika linaloingia katika upinzani wa kibiashara. Kwani hapo awali lilikuwa likipata ruzuku ya asilimia mia moja kutoka serikalini hivyo kukifanya kituo hicho kuwa tegemezi na kufuata kila ambacho serikali inataka.
Baada ya hapo tukashuhudia TBC ikianza kuja juu, vifaa vya kazi vya kisasa vikaingia, watangazaji wa shirika hilo wakaanza kuneemeka, aina ya habari za awali za kutukuza tu bila kufanya uchunguzi wa kina zikaanza kufutika na mwanga kuonekana na watu kurudisha imani.
Hakuna mtu ambae hajaridhishwa na kazi nzuri iliyofanywa na Tido Mhando wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Kila mtu alitamani ifike saa mbili aangalie TBC kuona nini kinaendelea, taswira halisi ya nchi yetu ilionekana na wapinzani walipata pa kuzungumzia.
Kiuhalisia TBC ilikuwa sahihi kufanya hivyo kwani shirika hilo la habari lilikuwa likijitegemea, na hata kama lingekuwa halijitegemei lakini chombo hicho kipo chini ya serikali hivyo kuacha kuandika mambo ya CCM sidhani kama ni kosa la kumfanya mtu kutimuliwa kazi. Kwani wakati wa kampeni CCM haikuwa na serikali, vyama vyote vilikuwa chini ya serikali. 
Hivyo kitendo cha kumfukuza Mhando, kimeidhalilisha serikali na chama tawala cha CCM kwa kuonekana wanapenda kuonyeshwa kwenye vyombo vya habari hata kama hawana cha kuiambia jamii. Mwanahabari habembelezwi wala kuombwa kuonyesha tukio, bali yeye mwenyewe atafanya kila juhudi kuweza kulipata tukio hilo ili kulitumia katika chombo chake.
Kitu ambacho kinanitia kinyaa kuhusu suala la Serikali ya Zanzibar na kuwatimua wahariri kwasababu tu hawampi ‘coverage’ kubwa Rais Shein, ni kuwa hata huyo ambae anapewa ‘coverage’ ni kiongozi wa serikali kuna ubaya gani?
Inawezekana hili agizo hata halitoki ikulu ya Zanzibar lakini kuna baadhi ya watu hupenda kujikombakomba kwa viongozi wa juu ili waonekane wanafanya kazi. Hakuna anaejua labda Rais mambo yamemtinga na hushiriki sana shughuli za nje ya nchi, shughuli zinazohusu kuzindua miradi, kutembelea wananchi na kutatua baadhi ya kero za kimaendeleo mambo hayo amemuachia makamu wake wa kwanza ambae ni Seif.
Sasa Seif Sharrif akionekana kwenye luninga vijana wa kisasa tunaita ‘akiuza sura’ sana kuliko bosi wake kuna ubaya gani?
Nadhani hili linapasa kuangaliwa kwa jicho la samaki, yaani liangaliwe kwa pande zote kitaaluma na kiutendaji. Yaani wanahabari wachunguze hili na kutoa tamko, kadhalika watendaji wa serikali nao walichunguze na kulitolea tamko hii ni aibu kwa wizara ya habari kubembeleza habari.
Waandishi tusiwe mabubu katika mambo yanayowahusu wenzetu, kudhalilishwa kwa wahariri Zanzibar kunaigusa taaluma hii kila pembe ya nchi. Hivyo hatuna budi kuzungumza na wanahabari wa Zanzibar ili kufanya uchunguzi wa kilichotokea.
Naamini heshima yetu itarudi, naomba kuwasilisha

No comments:

Post a Comment