Sunday, February 17, 2013

Kauli ya IGP Said Mwema kuhusu mauaji ya Padre Zanzibar..


Ndugu Wanahabari,
Nimelazimika nizungumze nanyi kuhusu tukio la kuuwawa kwa Padre Evaristi Mushi wa Kanisa Katoliki Zanzibar lililotokea leo asubuhi tarehe 17 Februari, 2013 eneo la Mtoni mkoa wa Mjini Magharibi, ambapo watu wasiofahamika walimpiga risasi Padre huyo alipokuwa anaenda kusalisha ibada katika kanisa la Betras. Baada ya tukio hilo kutokea alikimbizwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja, ambapo baadae alifariki dunia. Tukio hili ni baya na la kusikitisha.
 2 Kufuatia kutokea kwa tukio hilo na kujirudiarudia kwa vitendo vya kuwashambulia na kuwadhuru viongozi wa dini na uchomaji wa nyumba za ibada, Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama tumeanza uchunguzi wa kina wa kuwatafuta wanaohusika na matukio hayo.
 3Hivyo, nimetuma timu ya wataalam waliobobea kwenye masuala ya upelelezi na oparesheni kutoka Makao Makuu ya Polisi, kwenda kushirikiana na timu ya wataalam iliyoko Zanzibar. Hadi sasa watu watatu wananshikiliwa kwa mahojiano.
 Jeshi la Polisi limeimarisha doria maeneo yote hapa nchini na tunafuatilia mienendo na kuakamata watu wote wanaochochea, kufadhili, kuhamasisha na kushiriki katika vitendo vya uhalifu, vurugu na fujo.
 Tukiwa katika kipindi hiki, nawaomba wananchi wote hapa nchini kuwa watulivu wakati suala hili linaposhughulikiwa kuhakikisha kwamba wahalifu hao wanakamatwa na sheria inachukua mkondo wake.
 Naomba nitumie fursa hii pia, kuwasiliana na wananchi wenzangu wenye taarifa zitakazosaidia wahalifu hao kukamatwa kutupa ushirikiano kupitia namba zetu maalum za simu zifuatazo 0754785557 au 0782417247 na namba za makamanda wa mikoa na vikosi, ili kuhakikisha kwamba amani, usalama na utulivu vinadumishwa hapa nchini.
    Nawashukuru wananchi wote ambao wamekuwa wakitupa ushirikiano. 

AHSANTENI SANA

No comments:

Post a Comment