Tuesday, July 2, 2013

Wazungu wanasema: For Brazil, the party has only just begun.



Hakuna shaka taifa la Brazil linaanza kurudisha ufalme wa soka miguuni mwa wachezaji wao baada ya mwishoni mwa wiki iliyopita kutwaa taji la mashindano ya mabara yaliyofanyika nchini humo kwa kuwafunga Hispania 3-0.
Kwa muda mrefu Brazil imekuwa ikifanya vibaya katika michuano mikubwa ya soka hasa walipokuja Afrika kwa michuano ya kombe la dunia 2002 nchini Afrika Kusini, wachambuzi wa soka wakaanza kutabiri mwisho wa soka la Brazil na kutupa turufu ya kwa Ujerumani na Hispania.
Lakini kufanya vibaya kwa timu za Hispania kwenye kombe la mabingwa barani Ulaya dhidi ya timu za Ujerumani kuliamsha hisia kuwa Ujerumani inaweza kuchukua nafasi ya Brazil, lakini baada ya kombe la mabara kufikia hatua ya nusu fainali kila mtu akaanza kuamini Hispania imedhamiria, kilichotokea wakati wa fainali katika kiwanja cha Maracana jijini Reo De Jeneiro ni kilio kwa walioichukia Brazil.
Mabao mawili ya Frederico Chaves Guedes ‘Fred’ na moja la mshambuliaji aliyekuwa gumzo katika michuano hiyo Neymar Junior, yaliwamaliza nguvu wachezaji wa Hispania kiasi Sergio Ramos wa Hispania kushindwa kufunga penati katika kipindi cha pili.
Ambaye ameshuhudia fainali ile lazima ataafiki kuwa Brazil waliutawala mchezo kwa dakika zote tisini kama hiyo haitoshi walionekana kama wanacheza na wadogo zao tena kwenye mechi ya kirafiki, Hispania hawakuonyesha uhai kabisa waliangusha matarajio ya mashabiki wengi usiku ule.
Historia pia ilimkandamiza kocha wa Hispania Vicente Del Bosque kwani Brazil hawajawahi kupoteza hata mechi moja ya kiushindani katika ardhi yao tangu mwaka 1975 walipofungwa na Peru katika michuano ya Copa America.
Aidha tangu mwaka 1934 Hispania wamefanikiwa kuwafunga Brazil mechi mbili tu katika mechi tisa walizokutana ambapo mwaka 1934 walipokutana kwenye kombe la dunia nchini Italia, Brazil walilala kwa mabao 3-1 na mwaka 1990 katika mechi ya kimataifa Brazil walilala kwa mabao 3-0 kwa hiyo ni kama Brazil wamejibu mapigo ya mwaka 1990.
Katika hatua nyingine Brazil pia imeweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza kuwafunga Hispania katika mechi ya ushindani tangu mwaka 2010, ambapo Hispania imecheza mechi 29 bila kufungwa na taifa lolote mpaka jumapili iliyopita walipotulizwa na Brazil.
Wazungu wanasema: For Brazil, the party has only just begun. 
HAFIDH KIDO
kidojembe@gmail.com
July 3, 2013
DAR ES SALAAM, TANZANIA

No comments:

Post a Comment