Thursday, June 13, 2013

Jicho la watanzania na Bajeti leo....


Dar es Salaam na Dodoma. Macho na masikio ya Watanzania leo yataelekezwa kwa Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa wakati atakapoisoma hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali kuanzia saa 10.00 jioni bungeni, mjini Dodoma.

Sambamba na Mgimwa, pia mawaziri wa fedha za nchi za Kenya na Uganda nao katika muda huo watasoma bajeti za nchi zao.

Waziri mpya wa Fedha wa Kenya, Henry Rotich atasoma bajeti ya kwanza ya nchi hiyo ikiwa chini ya utawala mpya wa Rais Uhuru Kenyatta wakati ya Uganda itasomwa na Waziri wa Fedha, Maria Kiwanuka.

Mwelekeo wa Bajeti

Dk Mgimwa aliwaambia waandishi wa habari, Dodoma jana kuwa Serikali imetenga kiasi cha Sh18.2 trilioni kwa ajili ya mwaka ujao wa fedha wa 2013/14.

Alisema wameweka vipaumbele kadhaa ambavyo ni nishati vijijini, miundombinu, maji na upatikanaji wa pembejeo za kilimo.

Bajeti hiyo itatanguliwa na ile ya mwelekeo wa hali ya uchumi ambayo itasomwa asubuhi na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Dk Mgimwa alisema wananchi hasa wa vijijini watapata huduma ya maji hasa baada ya kuongezwa Bajeti ya Wizara ya Maji.

Awali, wabunge waligomea Bajeti ya Maji ya Sh398 bilioni kabla ya kuongezwa hadi kufikia Sh582.5 bilioni ikiwa ni ongezeko la Sh184 bilioni.

Waziri Mgimwa alisema pia kuwa suala la nishati ya umeme ni kipaumbele kingine cha Serikali na kwamba itaisambaza katika maeneo mbalimbali nchini na zaidi katika maeneo ya vijijini chini ya Wakala wa Nishati Vijijini (Rea).

Alisema kipaumbele kingine ni usambazaji wa pembejeo za kilimo vijijini ili kuwasaidia wakulima kulima mazao bora. Pia alisema katika mwaka huu wa fedha Benki ya Wakulima itaanzishwa ili kutoa mikopo yenye unafuu ya kilimo.

Aidha, Serikali ilikwishatangaza vipaumbele vingine ambavyo ni ujenzi wa Bandari za Tanga, Dar es Salaam, Mtwara na Bagamoyo, reli, elimu, Mfumo wa Teknolojia ya Mawasiliano (ICT), afya na ujasiriamali.

Katika bajeti iliyopita, vipaumbele vya Serikali vilikuwa kuimarisha miundombinu ya uchumi ikijumuisha umeme, barabara, reli, bandari na kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha.



Mwelekeo wa uchumi

Dk Mgimwa alisema uchumi wa nchi umekua kwa asilimia 6.9, wastani ambao ni mzuri na kuongeza kuwa kumekuwa na ongezeko la karibu Sh1.84 bilioni katika bajeti na kufikia Sh18.2 trilioni.



Udhibiti wa fedha za Serikali

Kuhusu kudhibiti ufujaji wa fedha, Dk Mgimwa alisema: “Tumeweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba watu wasiokuwa na uaminifu wanachukuliwa hatua kali tena kwa haraka.”

Alikiri kuwapo kwa upungufu katika kufikisha fedha za miradi kwa wakati na kwamba hilo linasababishwa na ufinyu wa bajeti na makusanyo.

Moja ya hatua zilizochukuliwa na Serikali kudhibiti Kitengo cha Ununuzi hasa wa magari ya Serikali na katika hotuba yake bungeni alisema: “Ununuzi wa magari ni eneo linalotumia fedha nyingi za umma na kutokana na hilo, Serikali imeona kuna umuhimu wa kuweka utaratibu bora utakaowezesha kupata thamani ya fedha katika ununuzi wa pamoja na matumizi ya magari yake.

Deni la Taifa

Kuhusu deni la taifa, Dk Mgimwa alisema halina shida kwani tofauti na nchi nyingine, nchi bado inakopesheka. Kwa mujibu wa hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni, deni hilo limefikia Sh21.028 trilioni bila dhamana ya Serikali kwa mashirika ya umma na binafsi hadi kufikia Desemba 2012, kati ya fedha hizo, asilimia 75.97 ni deni la nje.

Waziri Mgimwa alisema Serikali imeanza kulipa na kuanzia Julai 2012 hadi Aprili 2013, malipo ya madeni yamefikia Sh1,666.77 bilioni na kati ya hizo, deni la nje lililolipwa ni Sh213.57 bilioni, na Sh1,453.20 bilioni ni deni la ndani.

“Kimsingi, bado tuko vizuri, deni letu ni himilivu kabisa kwa vigezo vya kimataifa na wananchi wajue kuwa kila fedha tunazokopa tunawekeza katika miradi na kwenye sekta bora zaidi,” alisema Dk Mgimwa.

Marekebisho ya PAYE

Bila ya kufafanua, Waziri Mgimwa alisema kutakuwa na marekebisho ya viwango vya kodi katika maeneo mbalimbali.

Katika sherehe za Mei Mosi, mwaka huu zilizofanyika kitaifa mkoani Mbeya, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), lilipendekeza kima cha chini cha mshahara kiwe Sh740,000 kutokana na kupanda kwa gharama za maisha.

Katibu Mkuu wake, Nicolaus Mgaya alisema iliiomba Serikali ipandishe kima cha mshahara kufikia Sh315,000 kwa kima cha chini tangu mwaka 2010, lakini ombi hilo halijatekelezwa mpaka sasa.



Misamaha ya kodi

Waziri Mgimwa alisema asilimia 33 ya misamaha ya kodi itafutwa. Misamaha hiyo imeongezeka kutoka vitu vitano hadi 27, huku ikielezwa kuwa taifa linapoteza Sh1.8 trilioni kutokana na misamaha hiyo. Alisema katika bajeti ijayo, Serikali imeliangalia eneo hilo kwa umakini hasa kwa vitu ambavyo havina tija kwa taifa.

Mapema mwaka huu Dk alitoa mwelekeo wa Bajeti kwa mwaka 2013/14 na kusema, Serikali imepunguza utegemezi kwa asilimia tano, ikilinganishwa na mwaka jana.



Mapendekezo ya wadau

Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba alisema hatarajii jipya katika bajeti ya leo akisema imekuwa ni kawaida kuweka vipaumbele zaidi katika utawala na mishahara badala ya miradi ya maendeleo.

Alisema masuala ya utawala yamekuwa yanaonekana kama ni ya dharura ambayo hayawezi kuachwa hivyo kufanya miradi ya maendeleo kusahaulika licha ya kutengewa fedha.

“Mfano rahisi ni miradi ya maji, waziri wakati anawasilisha bajeti yake bungeni alisema kuwa fedha zilizopatikana ni asilimia 60 ya bajeti nzima iliyopita sasa katika mazingira kama hayo unategemea nini kipya? ”alisema.

Profesa aliitaka Serikali iache kuchezea akili za Watanzania kwa kuongeza bei katika vitu ambavyo havitumiki nchini na kuacha kueleza mapato yanayotokana na mauzo ya vitu kama dhahabu.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Wafanyabiashara Wenye Viwanda (CTI), Felix Mosha alisema ongezeko lolote la kodi na ushuru wa forodha katika Bajeti ya Serikali 2013/2014 huenda likasababisha kushuka kwa uzalishaji katika sekta ya viwanda.

Pia alionya ongezeko la kodi litapunguza pato la taifa kutokana na walio wengi kujikuta wakishindwa kumudu gharama za uendeshaji.

Mosha alisema umakini unahitaji katika suala la misamaha ya kodi kwani ni mizuri, lakini usimamizi makini unahitajika kwa kuwa inatumika vibaya ya na ukweli.



Chama cha Walimu

Chama cha Walimu Tanzania (CWT), kimesema hakiamini kama Bajeti hiyo itawasaidia walimu kwa kuwa mapendekezo waliyokubaliana hayajafanyiwa kazi.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Rais wa CWT, Gratian Mkoba alisema hiyo bajeti itakayosomwa ni mambo ambayo yameshapitishwa kwenye Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi hivyo fedha zilizotengwa ni ndogo na mapendekezo yaliyotolewa na chama hicho hayakuingizwa.

Mkoba alisema bajeti hiyo haitawasaidia kwa kuwa mwaka uliopita kilitengwa kiasi kidogo cha fedha na kusababisha mambo mengi yaliyopendekezwa kuachwa.

Imeandikwa na Ibrahim Bakari, Habel Chidawali, Joseph Zablon na Pamela Chilongola.
MWANANCHI

No comments:

Post a Comment