Friday, June 14, 2013

MAKOCHA STARS, IVORY COAST ANA KWA ANA


 Wakati timu ya Ivory Coast imewasili nchini jana usiku (Juni 13 mwaka huu) kwa ndege maalum, kocha wa timu hiyo Sabri Lamouchi na mwenzake wa Taifa Stars, Kim Poulsen watakutana na waandishi wa habari kuzungumzia mechi yao.

 Mkutano huo utafanyika kesho (Juni 15 mwaka huu) saa 4 kamili asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Mkutano huo pia utajumuisha makocha wa timu zote mbili. Ivory Coast inafanya mazoezi yake ya kwanza leo (Juni 14 mwaka huu) saa 9 alasiri kwenye viwanja vya Gymkhana.

Timu zote kesho (Juni 15 mwaka huu) zitafanya mazoezi ya mwisho kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Ivory Coast watafanya mazoezi saa 9 kabla ya kuwapisha Stars saa 10 kamili. Maandalizi yanaendelea vizuri ikiwemo kuwasili kwa maofisa wote wa mechi itakayochezwa Jumapili saa 9 kamili alasiri.

Wakati huo huo, mauzo ya tiketi kwa ajili ya mechi hiyo yameanza leo mchana (Juni 14 mwaka huu) katika vituo vya Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, City Sports Lounge iliyoko Mtaa wa Samora na Azikiwe, Dar Live Mbagala, BMM Salon iliyoko Sinza Madukani na Uwanja wa Taifa.

Mauzo yataendelea kesho katika vituo hivyo, wakati siku ya mchezo yatafanyika Uwanja wa Taifa. Viingilio katika mechi hiyo ya mchujo ya Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika katika kundi C ni sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000 VIP C, sh. 20,000 VIP B na VIP A sh. 30,000. Pia kuna kadi maalumu 100 kwa viti vya Wageni Maalumu (VVIP) zinazopatikana kwa sh. 50,000 katika ofisi za TFF.

TFF YATOA NOTISI YA MKUTANO MKUU

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ametoa notisi kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalumu wa Shirikisho utakaofanyika Julai 13 mwaka huu kwenye ukumbi wa NSSF Waterfront jijini Dar es Salaam ukiwa na ajenda moja ya marekebisho ya Katiba.

Notisi hiyo imetolewa juzi (Juni 12 mwaka huu). Rais ameitisha Mkutano huo kwa mujibu wa Ibara ya 25(1) ya Katiba ya TFF baada ya kupata maagizo kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kwa barua yake ya Aprili 29 mwaka huu.

Ajenda rasmi na taarifa nyingine zitatumwa kwa wajumbe siku 15 kabla ya Mkutano huo kwa mujibu wa Ibara ya 25(4) ya Katiba ya TFF. Wanachama wa TFF ambao ni vyama vya mikoa, vyama shiriki na klabu za Ligi Kuu wanatakiwa kutuma majina ya wajumbe halali.

TFF inapenda kuwakumbusha wanachama wake kutuma majina ya wajumbe halali ili kufanikisha maandalizi ya Mkutano huo. Ni vizuri kuhakikisha kuwa jina linalotumwa ni la mjumbe halali wa Mkutano Mkuu kwa mujibu wa Katiba ya TFF.

RAMBIRAMBI MSIBA WA ABDALLAH MSAMBA

Shrikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha mchezaji wa zamani wa timu za Pan Africans, Simba na Taifa Stars, Abdallah Msamba kilichotokea juzi usiku (Juni 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Msiba huo ni mkubwa kwa wadau wa mpira wa miguu kwani kwa nyakati tofauti Msamba akiwa mchezaji, na baadaye kocha wa timu kadhaa alitoa mchango mkubwa kwa timu mbalimbali alizochezea na kufundisha ikiwemo Villa Squad, hivyo mchango wake tutaukumbuka daima.

TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Msamba, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Kinondoni (KIFA) na klabu ya Villa Squad na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Maziko ya mchezaji huyo yamefanyika leo (Juni 14 mwaka huu) katika makaburi ya Ndugumbi mkoani Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mamia ya waombolezaji wakiwemo wachezaji wa zamani na viongozi mpira wa miguu nchini. Mungu aiweke roho ya marehemu Msamba mahali pema peponi. Amina



Boniface Wambura

Ofisa Habari

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
June 14, 2013

No comments:

Post a Comment