Sunday, June 2, 2013

Rasimu ya katiba mpya kuzinduliwa mchana huu viwanja vya Karemjee.

Dar es Salaam. Mwelekeo wa Taifa la Tanzania utaanza kujulikana leo mchana Tume ya Mabadiliko ya Katiba itakapozindua rasimu ya Katiba Mpya kwenye tukio la kihistoria litakalofanyika kwenye Viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam.

Watanzania wanasubiri kwa hamu kuona kama rasimu hiyo itakuja na majibu ya maswali magumu, makubwa ya muundo wa Muungano, madaraka ya Rais, uteuzi wa mawaziri kutokana na wabunge, muundo wa wakuu wa mikoa/wilaya na muundo wa mihimili mingine miwili ya dola; Mahakama na Bunge.

Uzinduzi wa rasimu hiyo unafanyika baada ya Tume hiyo kufanyia kazi ya uchambuzi wa maoni ya wananchi. Maoni hayo yalitolewa na wananchi wapatao 1,015,564 kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na waliohudhuria mikutano ya moja kwa moja, waliotuma ujumbe mfupi wa simu (sms), barua pepe na kutumia mitandao ya kijamii.

Idadi ya makundi yaliyotoa maoni ni 170 zikiwamo asasi 22 za dini, kiraia 72, taasisi za Serikali 71, vyama vya siasa 19, viongozi na watu mashuhuri 43 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

Rasimu hiyo ndiyo itakayopelekwa kwenye Mabaraza ya Katiba na itajadiliwa miezi mitatu ili kuona kama mapendekezo ya Tume hiyo baada ya kuchambua maoni hayo ya wananchi yanafaa au yanahitaji marekebisho.

Huo ni mwendelezo wa mchakato wa mabadiliko ya Katiba ulioanza mwaka jana baada ya Rais Jakaya Kikwete kuteua wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuanza kukusanya maoni.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Dar es Salaam jana na Katibu wa Tume hiyo, Assaa Rashid uzinduzi huo utaonyeshwa moja kwa moja kupitia Televisheni ya Taifa (TBC) kuanzia saa nane mchana.

Taarifa hiyo iliwaomba wananchi kufuatilia uzinduzi huo kwa umakini ili waweze kujua kinachoendelea. Kuzinduliwa kwa rasimu hiyo kutaanzisha upya mjadala wa Katiba ambayo inatungwa kwa mara ya sita.

Katiba iliwahi kutengenezwa mwaka 1961 wakati Tanganyika ilipopata Uhuru, mwaka 1962 baada ya nchi kuwa Jamhuri, mwaka 1964 ilipoundwa Katiba ya Muda baada ya Tanganyika na Zanzibar kuungana na mwaka 1965 ilitungwa Katika Mpya iliyodumu hadi mwaka 1977 baada ya vyama vya Tanu na ASP kuungana na kuifanya nchi kuwa chini ya utawala wa chama kimoja cha siasa.

Kwa upande wa Zanzibar kumekuwapo Katiba Tatu. Kwanza ni ile ya Uhuru iliyotungwa mwaka 1963, Mwaka 1979 ikatungwa Katiba nyingine na ya mwisho ni ile ya mwaka 1984.

Muundo wa Muungano

Kwa muda mrefu, suala la muundo wa Serikali mbili katika Muungano limekuwa mwiba katika siasa za Tanzania Bara na Zanzibar.

Wakati wa kutoa maoni yao, wananchi na wadau wengi wametofautiana kuhusu ni aina gani ya Muungano unaokidhi mahitaji ya sasa ya Watanzania. Kundi ambalo limeonekana kuwa kubwa likitaka Muungano wa Serikali Tatu ikiwa na maana ya Serikali ya Tanganyika, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hata hivyo, kuna kundi lingine ambalo linapendelea muundo uliopo sasa wa Serikali mbili, ya Muungano na SMZ uendelee na lingine linataka Serikali moja. Rasimu itakayotolewa leo inatarajiwa kutoa mwelekeo wa muundo huo.

Mwaka 1984, suala la muundo wa Muungano liliwahi kumlazimu aliyekuwa Rais wa Zanzibar na Makamu wa Rais, Aboud Jumbe kujiuzulu kwa kile kilichoitwa kuchafuka kwa hali ya hewa ya kisiasa huko Zanzibar.

Pia mwaka 1993, Muungano huo ulitikiswa baada ya kuibuka kwa kundi la Wabunge wa CCM lililokuwa linaitwa G-55 waliotaka kuundwa kwa Serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano lakini hoja yao ilizimwa na Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Pia suala la mgawanyo wa rasilimali nalo limekuwa likisababisha matatizo makubwa katika Muungano.

Madaraka ya Rais

Mbali na suala la Muungano ambalo lilikuwa ni moto katika maoni hayo, suala la madaraka ya Rais nalo ni eneo ambalo limekuwa likilalamikiwa ambalo rasimu inatarajiwa kutoa mwelekeo kuhusu madaraka hayo hasa katika uteuzi wa mawaziri na idadi ya wizara kama ilivyo katika Katiba ya Kenya ya sasa.

Mawaziri kutokana na wabunge

Baadhi ya wananchi waliotoa maoni yao kuhusu mabadiliko ya Katiba wametaka mfumo wa sasa wa uteuzi wa mawaziri kutoka miongoni mwa wabunge ubadilishwe. Wanataka wateuliwe kwa kuzingatia sifa na weledi badala ya utashi wa kisiasa.

Mmoja wa watu maarufu waliowahi kutoa maoni wakitaka mawaziri wasitokane na wabunge ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa.

Bunge na Mahakama

Spika wa Bunge, Anne Makinda alipotoa maoni yake alipendekeza kwenye tume hiyo kwamba kuwe na mabunge mawili; la seneti na la kawaida.
Hoja hii nayo imekuwa ikizungumzwa na wadau mbalimbali hasa wakihoji chombo kinachodhibiti Bunge kwa sasa.

Pia wadau wengi hasa wanasheria wanaona kwamba mfumo wa sasa wa uteuzi, hasa wa majaji una kasoro na kwamba mhimili huo wa Dola uachwe ujiendeshe na kuteua viongozi wake kama ilivyo Bunge.

Nafasi za wakuu wa mikoa/wilaya

Moja ya hoja ambayo imejadiliwa pia katika mchakato huo wa Katiba Mpya ni nafasi ya wakuu wa mikoa na wilaya. Baadhi ya wananchi wanataka vyeo hivyo vya kisiasa viondolewe na madala yake wawepo magavana ambao watachaguliwa na wananchi katika mikoa husika.    
MWANANCHI

No comments:

Post a Comment