Thursday, June 20, 2013

Maduka ya wahindi yashambuliwa DRC.


Maduka yanayomilikiwa na wahindi yamevamiwa katika mashambulizi mjini Kinshasa DRC baada ya kukamatwa kwa wanafunzi wakongomani nchini India.

Mwandishi wa BBC mjini Kinshasa anasema kuwa raia mmoja mhindi alijeruhiwa katika ghasia hizo na anatibiwa hospitalini.

Waandamanaji walighadhabishwa na hatua ya kukamatwa kwa wanafunzi 21 mjini Jalandhar, Kaskazini mwa India.

Kuna visa vya kutofautiana kuhusu sababu za kukamatwa kwa wanafunzi hao na kumekuwa na madai kuwa polisi wamewadhulumu.

Lakini balozi wa India katika Jamuhuri ya kidemokrasia ya Congo, Ram Manohar, aliambia BBC, kuwa polisi hawakuwadulumu wanafunzi hao, lakini wakasema kuwa kulikuwa na vurugu wakati wa maandamano.

Aliongeza kuwa wanafunzi hao waliachiliwa Jumatano nyakati za mchana.

Naibu waziri wa mambo ya nje wa DR Congo, alitoa ombi kuwa wanafunzi hao waachiliwe mara moja.

Maafisa wa utawala pia walitaka wanafunzi hao watibiwe kufuatia madai kuwa waliteswa walipozuiliwa.

Mapema taarifa za vyombo vya habari zilisema kuwa wanafunzi hao walijaribu kujitoa uhai.

Mwandishi wa BBC, Emmanuel Derville mjini Delhi, anasema kuwa wengi wa wanafunzi hao, waliozuiliwa wanatoka Kinshasa, na wako nchini humo kusomea uhandisi na masomo ya biashara kwa miaka miwili iliyopita.

Kulingana na Polisi, wanafunzi hao walikamatwa baada ya kuzuka kwa mapigano kati ya makundi hasimu ya wakongomani baada ya kuzuka mapigano katika kituo cha basi
mjini Jalandhar Jumamosi mchana.

Naibu wa polisi mjini Jalandhar, alisema kuwa wanafunzi hao walimpokonya mkoba wake mwathiriwa mmoja.

Lakini wanafunzi hao walisema kuwa purukushani lilianza baada ya mwanafunzi mmoja nusura kugongwa na basi

Baadaye alichapwa kwa bakora katika kile kilichoonekana kama shambulizi la ubaguzi wa rangi.
BBC SWAHILI





No comments:

Post a Comment