Wednesday, June 19, 2013

Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir awafuta kazi mawaziri wawili kwa ubadhirifu.

Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir, amewafuta kazi mawaziri wawili serikalini wanaohusishwa na sakata kubwa na mamilioni ya dola .

Bwana Kiir pia amewaondolea kinga dhidi yao wakiwa waziri wa fedha Kosti Manibe na mwenzake anayehusika na maswala ya baraza la mawaziri Deng Alor kushtakiwa na kuamuru kuanzishwa kwa uchunguzi dhidi yao

Wawili hao wangali kutoa kauli yoyote kuhusu tuhuma hizo.

Wadadisi wanasema kuwa ufisadi ni moja ya vikwazo vikubwa kwa utawala wa Kiir , Sudan Kusini tangu nchi hiyo kujitawala mwaka 2011, na kulifanya kuwa taifa changa zaidi duniani.

Mwezi juni, Bunge la Sudan Kusini lilipiga kura kuwasimamisha kazi kwa muda maafisa wakuu 75 wa serikali waliohusishwa na ufisadi.

Rais Salva Kiir alituma ujumbe kwa maafisa wa iliyokuwa serikali ya zamani ikiwataka warejeshe dola bilioni 4 pesa walizodaiwa kuiba.

Hata hivyo serikali ilitangaza kwenye mtandao wake rasmi kuwa bwana Manibe na bwana Alor, wataachishwa majukumu yao mara moja.

Rais Kiir aidha aliwaamuru kufika mbele ya kamati inayochunguza kashfa hiyo kujibu maswali kuhusu kuhusika kwao na sakata ya mamilioni ya dola pesa za serikali.

Pesa hizo zilidaiwa kutumika kununua kabati maalum za kuweka pesa ambazo haziwezi kuteketea , lakini haijulikani ikiwa kweli waliweza kuzipokea.

Sudan Kusini ina utajiri wa mafuta , lakini ni moja ya nchi barani Afrika ambazo zina miundo mbinu duni na taasisi duni za kiafya na elimu

Ilijipatia uhuru kutoka kwa Sudan mwaka 2011 mwezi Julai baada ya vita vya muda mrefu vya wenyewe kwa wenyewe. Chanzo: bbcswahili

No comments:

Post a Comment