Saturday, June 15, 2013

Mechi za kufuzu kombe la Dunia kwa nchi za Afrika.



Ivory Coast na Misri ni miongoni mwa mataifa ya Afrika ambayo huenda yakafuzu kwa awamu ya mwisho ya kufuzu kwa fainali ya kombe la dunia ya mwaka wa 2014.

Endapo timu hizo mbili zitashinda mechi zao za wikendi hii, basi zitachukua nafasi ya kwanza katika makundi yao.

Ethiopia na Tunisia vile vile zinahitaji ushindi ili kuwa katika nafasi nzuri ya kufuzu.

Kwa mujibu wa hesabu endapo timu hizo zitatoka sare, na wapinzani wao wa karibu kutoka sare au kushindwa basi vile vile watakuwa wamejikatia tikiti ya raundi ijayo.

Sare ya aina yoyote hata hivyo huend ikadidimiza nafasi ya Ethiopia.
Miamba matatani

Misri, ambao ni mabingwa mara saba wa Afrika wamefuzu mara mbili tu kwa kombe la dunia, waliilaza Zimbabwe kwa magoli 4-2 katika mechi ya kundi G.

Mohamed Salah alifunga magoli matatu wakati wa mechi hiyo na wikendi hii wanacheza na Mozambique ambayo ililazwa magoli sita na Guinea.

Kushiriki katika fainali za kombe la dunia kwa mara ya kwanza kwa miaka ishirini na minne iliyopita, imekuwa ndoto ya kocha Bob Bradley raia wa Marekani na atakuwa na kibarua kigumu kuteua kikosi chake cha kwanza kitakachojumuisha wachezaji wakongwe kama vile Mohamed Aboutrika na chipukizi kama vile Salah.

Misri inacheza mechi hiyo huku ikiwa na ufahamu kuwa Mozambique inakabiliwa na matatizo baada ya kumfuta kocha wake Mjerumani Gert Engels, siku tatu zilizopita.

Mozambique walilazwa magoli sita kwa moja na Guinea Jumapili iliyopita na hivyo kuzima matumaini yao ya kufuzu kwa kombe la dunia.

Kufikia sasa Mozambique imezoa alama mbili pekee alama kumi nyuma ya vinara wa kundi hilo Misri.

Misri inahitaji alama moja tu ili kufuzu kwa raundi ya mwisho kwa kuwa tayari wamezoa alama 12, tano mbele ya Guinea.

Sare katika uwanja wao wa nyumbani dhidi ya Burkina Faso itaiwezesha Congo Brazzaville kufufua matumaini yake ya kufuzu.

Zambia na Algeria ni nchi zingine ambazo pia zinapigiwa upato kusonga mbele na ni sharti washinda mechi ya wikendi hii na pia katika mechi yao ya mwisho.

Miongoni mwa timu zinazokabiliwa na kibarua kigumu makundi yote kumi ni Burkina Faso ambayo ni sharti ishinde mechi yake dhidi ya Ethiopia mjini Adis Ababa.

Ikiwa Ghana itashindwa na Lesotho, basi itakuwa imesitisha safari yake ya kuelekea Brazil ikiwa Zambia itailaza Sudan.

Congo, ambayo itamtegemea nyota wake Christopher Samba anayecheza soka ya kulipwa nchini England na Klabu ya Queen Park Rangers, iliyoshushwa daraja, wanajikuta katika hali ngumu.

Congo imefunga mara mbili tu katika mechi nne, licha ya kuwa msimamo wa kundi E, inaonyesha wana magoli matano.

Hii ni kwa sababu walipewa magoli matatu baada ya Burkinafaso kuadhibiwa baada ya kumshirikisha mchezaji ambaye hakupaswa kucheza wakati wa mechi yao ambayo walitoka sare ya kutofungana bao lolote.

Viongozi wa kundi C, Ivory Coast wanacheza na Tanzania mjini Dar na nyota wake anayeichezea Arsenal Gervinho anatarajiwa kucheza baada ya kukosi mechi yao dhidi ya Gambia ambayo walishinda kwa magoli matatu kwa yai.

Ethiopia, ni nchi ya nne katika kundi A nyuma ya Afrika Kusini, Botswana na Jamuhuri ya Afrika ya Kati.

Ethiopia imeshinda mechi zake tatu na kutoka sare moja na hivyo imo alama mbili mbele ya Bafana Bafana ya Afrika Kusini.

Baada ya kutoka sare na Sierra Leona ya kufungana magoli mawili kwa mawili mjini Freetown, Tunisia wikendi hii inatoana jasho na Equitorial Guinea ambayo kwa sasa inashikilia nafasi ya kumi na moja barani Afrika kwa mujibu wa orodha ya timu bora iliyotolewa na shirikisho la mchezo wa soka duniani FIFA.

Tunisia imeshinda mechi moja kati ya nne ilizocheza.

Algeria nayo iliilaza Benin 3-1 na imepangiwa kuchuana na Rwanda.

Ikiwa Mali itatoka sare au kushindwa mechi yake dhidi ya Benin basi Tunisia itakuwa imefuzu kwa raundi ijayo ikiwa itaishinda Rwanda.

Bofya Matokeo ya mechi mbali mbali zilizochezwa siku ya Jumamosi
BBC SWAHILI

No comments:

Post a Comment