Wednesday, November 7, 2012

Kikwete atembea jumla ya kilometa 2,770 kufanya ziara mkoa wa kilimanjaro,ambapo alizindua miradi 19 ya maendeleo.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amerejea Dar es Salaam mchana wa jana, Jumanne, baada ya kumaliza ziara ya siku tisa katika mikoa minne ambako amekagua, kuanzisha ama kuzindua miradi 19 ya maendeleo na kutembea kiasi cha kilomita 2,770. 

Rais Kikwete amewasili Dar es Salaam akitokea Dodoma ambako amefanya ziara ya kikazi ya siku mbili baada ya kumaliza ziara katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara na Singida. Katika Mkoa wa Kilimanjaro ambako Rais Kikwete alianzia ziara yake Oktoba 28, mwaka huu, miongoni mwa mambo mengine alikagua nyumba za wahanga wa maporomoko ya mwaka 2006 kwenye kijiji cha Goha na akafungua Kiwanda cha Kusindika Tangawizi kilichoko Mamba Miamba, Wilaya ya Same, na akafungua Shule ya Sekondari ya Kata ya Asha Rose Mingiro iliyoko mjini Mwanga. Miradi mingine aliyoifungua Rais 

Kikwete katika Mkoa wa Kilimanjaro ni uzinduzi wa barabara za Rombo Mkuu-Tarakea na Kwasadallah-Masama na akafungua Ofisi ya Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (NAO) mjini Moshi. Katika Mkoa wa Arusha, Rais Kikwete alizindua Hospitali ya Wilaya ya Arusha ya Olturumet, akazindua Mradi Mkubwa wa Uboreshaji wa Miji kwa kufungua barabara za Jiji la Arusha, akazindua Jiji la Arusha, akafungua rasmi Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela na akatembelea Kiwanda cha Nguo cha A-Z. Kabla ya kuondoka Mkoani Arusha, Rais Kikwete alifungua Shule ya Msingi ya Sokoine na kuzindua ukarabati mkubwa wa Barabara ya Minjingu-Arusha. Mkoani Manyara, Rais Kikwete alifungua rasmi Barabara ya Singida-Minjingu-Arusha, akazindua mradi mkubwa wa maji wa Mji wa Babati na akaweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Babati-Bonga. 

Mkoani Singida, Rais Kikwete alizindua mradi mkubwa wa maji wa Mwankoko kwa ajili ya Mji wa Singida, akaweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Manyoni-itigi-Chaya na akafungua Barabara ya Issuna-Manyoni. Imetolewa na: Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu. 

Imetolewa jana na Ikulu Dar es Salaam
. 6 Novemba, 2012


1 comment: