Wednesday, November 28, 2012

makala ya niache nisome imetoka gazetini leo....


Na Hafidh kido

Tofauti na matarajio ya wengi kuwa mkuu mpya wa wilaya ya Handeni Muhingo Rweyemamu angeanza uongozi wake kwa kutazamia mambo makubwa kama kukuza uchumi ama usafi wa mji lakini nguvu zake zote amezilekeza katika kampeni ya ‘niache nisome’.

Raia Mwema iliamua kufanya ziara wilayani humo ili kuangalia mapambano hayo na mwandishi wetu hakufanya papara ya kukutana na kiongozi yeyote bali aliingia mitaani na kusikiliza maoni ya wakazi juu ya utendaji wa mkuu mpya wa wilaya yao inayotajika kuwa nyuma kimaendeleo katika wilaya za mkoa wa Tanga.

Ilichobaini Raia Mwema ni kuwa ndugu Muhingo hataki mchezo katika suala la mtoto wa kike, na wakazi wa Handeni hasa wale wanaopenda utamaduni huo wa kuoa vitoto vya shule inawawia vigumu sana kumpa ushirikiano. Katika vijiwe vya waendesha bodaboda, wauza kahawa, sokoni na vijiwe vya wacheza bao sehemu zote hizo wanazungumza kampeni ya niache nisome.

“Huyu mkuu wa wilaya ni mkali kweli, yaani hataki mchezo watoto wetu wenyewe anatupangia muda wa kuwaozesha. Hajui kama maisha ni magumu na hatuwezi kuwasomesha mabinti zetu au yeye aje atusaidie kulipa ada,” hayo ni baadhi ya mzungumzo ambapo mwandishi wetu alikwenda kushiriki kunywa kahawa bila ya kujitambulisha.

Niache nisome ni nini.

Hii ni kampeni iliyoanzishwa na ndugu Muhingo ili kumwokoa mwanafunzi wa kike kwa kumpa ujasiri wa kuwa na sauti ya kishujaa kumjibu mzazi ana mtu anaemtaka kimapenzi kwa kumwambia ‘niache nisome’. Lengo ni kumfanya ajitetee mwenyewe ili afikie malengo aliyojiwekea.

“Mbali ya taaluma ya uandishi wa habari lakini niliwahi kuwa mwalimu wakati fulani, nilipoteuliwa kuwa mkuu wa wilaya hii na Rais Kikwete nilikuta chama cha waandishi wa habari wanawake TAMWA wakifanya utafiti juu ya hali ya elimu wilayani humu na wakagundua watoto wengi wa kike wanashindwa kumaliza masomo yao kutokana na mimba na ndoa za mapema,” anaanza kueleza Muhingo.

Wakati mwandishi wetu akifanya mazungumzo haya hafla simu ya mkuu wa wilaya ikaita, alikuwa ni mzazi akitoa taarifa juu ya mwalimu mkuu anaetembea na wanafunzi. Baada ya kukata simu akapokea ujumbe mfupi kuna mwanafunzi mwengine anaolewa katika kata ya Kabuku.

Muhingo, akamgeukia mwandishi na kumwambia, “Nadhani habari yako inazidi kunoga maana umejionea hali halisi namna tatizo hili lilivyokuwa kubwa na watu wa Handeni tayari wameshakuwa tayari kutoa ushirikiano.”

Akaendelea na maelezo “Nilipoteuliwa katikati ya mwaka huu kitu cha kwanza nilipitia taarifa za wakuu wenzangu waliopita, sifa kuu ya wilaya hii ni maendeleo duni hasa katika nyanja ya elimu.

“Nikakuta mwaka 2011 wanafunzi wapatao 900 waliacha shule kutokana na sababu mbalimbali nyingi zikiwemo kuolewa na ujauzito. Niliumia sana, kitu cha kwanza baada ya kuingia ofisini nilijifanya mtu wa kawaida nikaanza kukaa vijiwe vya kahawa, nikaenda kukaa katika foleni za hospitali kusikiliza matatizo ya wananchi na hata sokoni nilipitapita mpaka walipoanza kunijua nikaamua kuacha lakini nilishapata taarifa nyingi sana kuhusiana na wilaya hii,” Muhingo.

Malengo ya kampeni

Niache nisome, ni kampeni aliyoinzasha akishirikiana na mkewe ambae anasoma shahada ya uzamivu katika mambo ya jamii kwenye chuo kimoja nchini China. Ambapo waliwashirikisha wanafunzi kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam, wakafanya utafiti na kukusanya taarifa za kutosha juu ya tatizo hilo.

Utafiti wao ulibaini kuwa wazazi nao huumia wanapoona binti yao amepata ujauzito akiwa shule, lakini kwa kiasi kikubwa binti hubaki peke yake pale anapozuiliwa kisheria kuendelea na masomo.

Awali kabla ya kukutana na mkuu wa wilaya Raia Mwema lilifika ofisi ya afisa maendeleo ya jamii wilayani humo ambae amehusika kwa kiasi kikubwa kusimamia kampeni hiyo ya niache nisome.
Ndugu Julius Mhando, afisa maendeleo ya jamii alianza kuelezea tatizo la utoro na mimba kwa watoto wa kike kutoka kwa wazazi ambao kwa kiasi kikubwa wamechangia tatizo hilo.

“Unajua miaka ishirini iliyopita  handeni kulikuwa na shule mbili tu za sekondari, hivyo utaona ni kwa kiasi gani kizazi cha kuanzia mwishoni mwa miaka ya thamanini hawakusoma. Na hawa ndiwo wazazi wa mabinti tunaoshughulika nao sasa.

“Wazazi hawajui umuhimu wa elimu, na Handeni asilimia 75 wanaishi katika umasikini uliotopea, hivyo zipo taarifa nyingi zinakuja ofisini kwetu wazazi wanawaficha watoto wao waliofaulu wasiende sekondari kwa kuwa hawana uwezo wa kuwasomesha. Unadhani mtu huyo binti yake akimaliza darasa la saba akija mtu anataka kuoa atakataa, au binti awe kidato cha pili ama tatu na anasoma katika mazingira magumu mzazi atakataa vipi posa ya binti huyo ikiwa binafsi hawezi kumsomesha wala kumuhudumia na isitoshe mwenyewe hajui umuhimu wa elimu kwani hakusoma,” alieleza kwa uchungu Mhando.

Aidha Mhando alifafanua kuwa sababu kubwa za mabinti kupata ujauzito wakiwa shule ni kutojitambua wala kutojithamini kama msichana, tama isiyolingana na uwezo wao pamoja na baadhi ya mabinti kujipa majukumu ya wazazi kwa kuwalea wadogo zao kwani wazazi wana hali mbaya kimaisha.

“Takwimu za idara yangu ya maendeleo ya jamii kwa wilaya hii ya Handeni inasema kwa mwaka 2012 mpaka kufikia mwezi huu wa kumi wanafunzi wa shule ya msingi walioacha shule kwasababu mbalimbali nyingi ikiwemo ujauzito na kuolewa ni kama ifuatavyo; darasa la nne 3%, darasa la tano 6%, darasa la sita 39%, wakati darasa la saba ni 52%,” alifafanua.

Kwa upande wa idara ya elimu wilayani humo ofisi ya afisa elimu ya sekondari imempokea mkuu wa wilaya mpya kama mkombozi na msaidizi mwema kwa tatizo hilo la utoro shuleni hasa kwa watoto wa kike.

Afisa taaluma kwa shule za sekondari wilayani humo Basil Mrutu, alizungumza kwa niaba ya afisa elimu na kueleza kuwa tatizo kubwa wanalokumbana nalo kwa upande wa sekondari ni idadi kubwa ya wanafunzi wanaofaulu kutoka shule za msingi kushindwa kuripoti kwa kidato cha kwanza.

“Kwa sasa wilaya kwa sekondari kidato cha kwanza mpaka cha nne ina wanafunzi wapatao 13688, kwa mwaka huu ufaulu kutoka darasa la saba ilikuwa ni asilimia 73, lakini kutoka januari mpaka octoba wanafunzi 241 hawajaripoti wasichana 139 na wavulana 102, sababu kubwa ikiwa ni hali duni ya maisha.

“Kwa upande wa mamba mwaka huu tu tuna taarifa za mamba zipatazo 23. tunamshukuru sana mkuu wa wilaya tangu aanze kampeni hii miezi miwili iliyopita tatizo linaonekana kupungua lakini itachukua mud asana kuisha kabisa maana wakazi wa Handeni wanaona ni kama utamaduni wao kuozesha watoto wakiwa na umri mdogo nadhani ni kutokana na kushindwa kuwahudumia kimaisha,” alieleza Mrutu.

Kwa upande wake Mrutu nae aliungana mkono na afisa maendeleo ya jamii wilayani humo kuhusu tatizo la wazazi kutosoma kutokana na uhaba wa shule miaka ya nyuma.

“Ni kweli wilaya hii ilikuwa nyuma sana kielimu kwasababu ilikuwa na idadi ndogo sana ya shule za msingi na sekondari, mathalan kabla ya mwaka 2005 wilaya ilikuwa na shule mbili tu za sekondari lakini hivi tunavyozungumza wilaya ina sule 30 za serikali na binafsi,” alizungumza kwa sauti ya ushindi Mrutu.

Alipozungumzia tatizo la ujauzito Mrutu alisema “Mara nyingi wanafunzi wanaopata ujauzito wakiwa shule ukichunguza maendeleo yao ni mabaya hata kitaaluma,nah ii inasababishwa na malezi mabaya waliyoyapata kutoka ngazi ya familia.

“Utakuta mtu aliempa mimba ni jirani ama ndugu wa karibu hivyo hata wazazi huwakingia kifua na kutaka tatizo limalizwe kifamilia mara nyingi tulikuwa tunaishia kuwafukuza shule halafu basi. Lakini tunashukuru mkuu wa wilaya wa sasa hataki mchezo anampeleka polisi kila kijana aliehusika na ujauzito wa mwanafunzi.

“Kampeni hii lazima uingwe mkono na wazazi wa Handeni kwani inakata minyororo ya ujinga, elimu ndiyo mzunguko pekee wa kuondoa umaskini, watoto wa kike wanatakiwa kupewa kipaumbele katika elimu kuliko wa kiume. Niache nisome, itamfanya motto wa kike ajitambue na kuhimili kupambana na mazingira hatarishi,” alisisitiza afisa taaluma huyo wa wilaya.

Raia Mwema halikuishia hapo lilikwenda kuonana na mkuu wa operesheni ya kukamata watu wanaohusishwa kuoa ama kuwapa ujauzito wanafunzi, huyu ni mkuu wa upepelezi wa jeshi la polisi wilaya ya Handeni ASP Juma Jumanne.

“Nimekuja handeni miezi michache iliyopita hazidi miwili kwa utafiti wangu mdogo nimegundua wilaya hii haina uhalifu mkubwa bali ni udokozi mdogomdogo, kazi kubwa ninayoifanya ni kushirikiana na mkuu mpya wa wilaya ndugu muhingo kuhakikisha watoto wa kike wanapata haki ya elimu bila bughudha,” alianza kumuelezea mwandishi.

ASP Jumanne alisema kuwa kampeni hii ya niache nisome haijawahi kufanyika katika historia ya wilaya ile, kwa maana katika taarifa ya ofisi yake ya upepelezi wala ofisini kwa bosi wake mkuu wa polisi wa wilaya OCD, hajaona kesi iliyoonyesha mtu au watu walikamatwa kwasababu ya kumpa mamba mwanafunzi ama kumuoa hali mambo hayo yalikuwa yakifanyika tena kwa kiwango cha juu.

“Tatizo ni kubwa sana kuliko unavyofikiri bwana mdogo, katika jeshi la polisi nimetembea wilaya nyingi sana lakini sijaona wilaya inayoongoza kwa mambo haya kama handeni. Haiwezekani kwa wiki tunapokea kesi sita mpaka saba (6-7) maana yake kwa siku wastani wa kesi moja ya ujauzito ama ndoa, huwezi kuamini tangu nianze kusimamia kesi hizi mpaka sasa kuna kesi 60 hapa kituoni zinazongoja kuenda mahakamani.

“Na mahakamani kuna kesi 20 zinazongoja hukumu, hivyo kufanya kesi 80, ndani ya miezi mitatu. Mbali ya zile ambazo hatujazikamata, unadhani tatizo hili ni kubwa kiasi gani,” alihoji ASP Jumanne.

Hata hivyo jeshi la polisi limelalamika changamoto wanazokutana nazo katika zoezi hilo kiasi kulifanya kuwa gumu kuanzia utekelezaji mpaka kusimama mahakamani.

Mathalan, wameeleza kuwa kitengo cha upelelezi kina askari 13 tu wilaya nzima, ni idadi ndogo kuliko wilaya yoyote nchini, kadhalika wilaya nzima ina gari moja tu la polisi ukiachia gari ya OCD, na vifaa vingine vya kiintelijensia.

“Wilaya ina uhaba wa askari wa upelelezi, vifaa ikiwemo silaha na  gari tena hasa mafuta ya gari. Maana ingawa gari tunayo moja wilaya nzima lakini ukosefu wa mafuta ya kutosha nalo ni tatizo kubwa maana kampeni hii inahitaji tuwepo eneo la tukio mara tu tunapopigiwa simu. Sasa mathalan kwa siku tukipokea simu tano za mabinti wanaoolewa ukichanganya na uhalifu mwingine wa kila siku mafuta tutapata wapi,” alihoji ASP Jumanne.

Changamoto nyingine wanayokumbana nayo katika operesheni hiyo ya kukamata watu wanaowapa ujauzito watoto wa shule ni sheria inayoonyesha kuwakingia kifua ‘mabazazi’ hao. Maana kwa mujibu wa sheria ya nchi kifungu cha 133 na 134, vinasema wai kuwa motto ni mwenye miaka 16, hivyo mtu yeyote mwenye umri unaozidi miaka hiyo akiolewa ama kushiriki mapenzi kwa ridhaa yake basi hakuna kesi hata akipata mamba.

Lakini wakati huohuo kwa kidato cha pili, tatu na nne wapo mabinti ambao wana umri wa mika 19 mpaka 20, maana yake wakipata ujauzito watu waliowapa hawatakiwi kupelekwa mahakamani maana sheria ya nchi inasema huyo si motto na ikiwa hakushurutishwa bali ameridhia tendo hilo hakuna kesi ya kujibu.

Majibu ya mkuu wa wilaya

Baada ya mwandishi wetu kuzunuka kote huko na kupata kilichojiri aliamua kurudi ofisini kwa mkuu wa wilaya na kumpa mrejesho wa watendaji wake wanavyopambana katika kumsaidia kuhakikisha mabinti wanapata haki yao ya elimu.

Kuhusiana na haba wa mabweni kwa wasichana Muhingo alisema uhaba wa mabweni si tatizo, maana kunaweza kukawepo mabweni na wanafunzi wakaambiwa wakae bure, lakini hakuna maji wala chakula na hili ndilo linalowafanya wakahangaika.

Hivyo ofisi yake kwa kushirikiana na baadhi ya mashirika ya kijamii wameamua kuhakikisha wanachimba visima katika kila shule ili kuwa na uhakika wa maji. Baada ya hapo wilaya itaanzisha utaratibu wa kuwa na mashamba ya shule, ambapo kwa kuanzia wamepata matrekta saba (7), ambayo watayasambaza katika shule zitakazokuwa tayari kutenga ekari za kutosha kuweza kulima.

“Hili la kurudisha kilimo mashuleni ni wazo ambalo wanafunzi wenyewe wamelipokea vizuri, maana tayari tumeshazungumza na wakuu wa shule na wapo waliokubali kutenga ekari za kutosha kuweza kulima mahindi na mbogamboga mazao yatakayotumika kwa chakula cha shule. Pia wanafunzi watakaokuwa tayari watafundishwa kuendesha matrekta na wengi wameonekana kulifurahia hili.

“Haya matrekta saba tutayasambaza katika tarafa zote saba kila tarafa trekta moja, na huko yatatembea katika mashule na kulima kwa ada ndogo ya mafuta ya kuendeshea trekta na kumlipa dereva ama msimamizi, kimsingi tunataka kuwajengea uwezo wa kujitegemea wanafunzi wote wa kike na wa kume,” Muhingo.

Kuhusu sheria kusema motto anaishia miaka 16, Muhingo aliitaka serikali kurekebisha hiyo sheria maana inawapa mwanya watu wabaya kuwaharibu wanafunzi. Na akasisitiza mtoto ni mtoto tu madhali anasoma, akishamaliza ama akifika chuo kikuu hapo watajuana wenyewe.

“Hali ni mbaya sana Handeni katika vita hii, najua huko mitaani wananichukia lakini wengi wa wanaonichukia ni wale wabaya lakini nikwambie ukweli wengi wameshaanza kukubali kutoa ushirikiano. Awali masheikh tuliwakuta wanaozesha tukasema na wao tukiwafunga haitosaidia bali niliwaita baadhi yao na wenyeviti wa vijiji nimezungumza nao na sasa wananipa ushirikiano wa kutosha.

“Kwa upande wa jeshi la polisi kuwa na uhaba wa vitendea kazi ni kweli, nililiona hilo na tayari nimeshazungumza na IGP Said Mwema, ila sitaki kuwaambia mpaka huo msaada utakapokuja. Maana kiukweli Handeni ilisahauliwa, hata idara ya maendeleo ya jamii hawana gari hata moja safari yao ya kwanza kuenda vijijini walitumia gari yangu ni hatari kweli,” alieleza.

Kampeni hii ya ‘niache nisome’ imevutia watu wengi hata mkuu wa mkoa wa Tanga Chiku Galawa, ameipenda na kuamua Handeni iwe ni wilaya mfano (pilot area) ili kampeni ikionyesha mafanikio iwe ni ya Mkoa na ikiwezekana nchi nchima.

Kwa kuthibitisha hilo Mkuu huyo wa mkoa atashiriki wiki ya elimu itakayofanyika wilayani humo hivi karibuni ambapo itakuwa ndiyo ya kwanza kufanyika tangu wilaya hiyo ianzishwe.


Hafidh kido
Handeni Tanga
  





No comments:

Post a Comment