Wednesday, January 9, 2013

Michuano ya kombe la Mapinduzi, haya ndiyo niliyoyaonna.

 Wachezaji wa miembeni wakijisaidia haja ndogo kwenye ukuta. Uwanja hauna vyoo wala vyumba vya kubadilishia nguo.



Na Hafidh Kido

Michuano ya kombe la mapinduzi inayofanyika kila mwaka kuadhimisha sherehe za mapinduzi matakatifu yaliyomng’oa mkoloni wa kiarabu katika visiwa hivyo mwaka 1964 inakwenda mwishoni baada ya kubakia timu nne katika nane zilizoshiriki michuano hiyo.

Timu zilizoshiriki michuano hii ni nane ambazo kundi A lilikuwa na Simba, Tusker (Kenya), Jamhuri ya Pemba na Bandari. Kundi B lilikuwa na timu za Coastal Union, Mtibwa Sugar, Azam FC na Miembeni.

Timu zilizoingia hatua ya nusu fainali ni Tusker na Simba kwa kundi A, wakati kundi B ni Azam FC na Miembeni.

Nusu fainali ya kwanza itachezwa jumatano (leo) saa mbili na nusu usiku katika uwanja wa Amaan kati ya Simba na Azam FC, wakati nusu fainali ya pili itachezwa kesho alhamisi usiku katika uwanja huohuo kati ya Tusker na Miembeni. Wakati fainali iategemewa kuchezwa siku ya kilele cha sherehe za mapinduzi tarehe 12 January mwaka huu.

Simba kuondoa kikosi cha kwanza katika michuano

Timu ya Simba kutoka Tanzania bara ambayo imefuzu kuingia hatua ya nusu fainali katika michuano hii imeduwaza mashabiki wake wa Zanzibar baada ya kutangaza kuondoa kikosi cha kwanza cha timu hiyo ili kuweka kambi nchini Oman kujiandaa na mzunguko wa pili wa ligi kuu bara.

Wekundu wa mtaa wa msimbazi kariakoo Dar es Salaam wanafanya hivyo ili kujibu mapigo ya watani wao Young Africans nayo ya Kariakoo mtaa wa twiga baada ya timu hiyo kuwek kambi nchini Uturuki kwa wiki mbili sasa.

Kocha mkuu wa Simba Mfaransa Patrick Liewing aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa kuwa ameamua kufanya hivyo kwani anahitaji kukaa na kikosi cha kwanza cha timu hiyo ili kuweza kuwajua vema hasa ikizingatiwa mzungu huyo bado hajawaona Simba wakiwa uwanjani, kwani ameshuhudia mechi tatu za kombe la mapinduzi lakini asilimia kubwa ilikuwa ni vijana wa timu B.

Kwa uamuzi huo maana yake Simba watalazimika kuwaachia wachezaji wa timu B kuendelea na hatua ya nusu fainali ambapo mechi ya kwanza watakutana na Coastal Union kutoka mjini Tanga.

Mtibwa Sugar kuwekwa kambi moja na Coastal Union

Waswahili wanasema akumulikae mchana usiku atakuunguza, waandaaji wa michuano hii wamefanya kitendo cha ajabu sana katika taratibu za soka kwa kuwaweka wapinzani wawili kwenye hoteli moja.

Coastal Union na Mtibwa Sugar ni timu zilizo katika kundi moja yaani kundi B, lakini cha ajabu wote wamewekwa katika hoteli moja. Ni ajabu sana kwa waandaaji kufanya kitendo hicho kwani wanajua wazi katika michuano yoyote timu zinakuwa na usiri mkubwa hasa katika mbinu za kukabiliana na mpinzani wawapo uwanjani.

Wachezaji kukaa eneo moja kunaweza kuibua vitendo vya hujuma ama kuleta urafiki usio na msingi kwa timu zao.

Sasa sijui ulikuwa ni uhaba wa hoteli, kukosa fedha ama dharau tu kwa timu hizi kutoka Morogoro na Tanga. Raia Mwema ilijaribu kuzungumza na waandaaji juu ya suala hili lakini majibu yao ilikuwa ni ya mkato. Hakuna alietoa jibu la uhakika kuwa kwanini timu za kundi moja ziwekwe kwenye kambi moja, mpira ni vita, kuna mbinu nyingi za ndani ya uwanja na mbinu nyingi zaidi za nje ya uwanja. Lazima ZFA waandaaji wa michuano hii wajirekebishe.

 Uwanja wa Mao Tse Dong

Zanzibar ina uhaba wa viwanja, Unguja na Pemba ina viwanja viwili tu vinavyoweza kuchezesha mechi za kimataifa. Uwanja wa Gombani ulio Pemba na uwanja wa Amaan Unguja.

Lakini cha kushangaza wameamua kuutumia uwanja wa Mao Tse Dong ambao hadhi yake hauwezi hata kuchezesha ligi kuu ya Tanzania Bara. Upo katika hali mbaya sana, hakuna majukwaa na hata eneo la uwanja ‘pitch’ imezuiwa kwa kiasi kidogo sana. Laiti mashabiki watakuwa na hasira ni rahisi kuweza kuwavamia na kuwadhuru.

Aidha hakuna vyumba vya kubadilishia nguo wala vifaa vya usalama kama mitungi ya kuzimia moto na milango ya dharura ikiwa kutatokea vurugu. Ni uwanja ambao hauwezi kuuelezea kwa maneno matupu kuwa haufai hata kidogo kwa michuano hii ambayo inashirikisha mpaka timu kutoka nchi jirani kama Kenya ama Uganda.

Uwanja hauna vyoo kiasi wachezaji wakitaka kujisaidia ni tatizo kubwa kwani Raia Mwema ilishuhudia wachezaji wa timu ya Miembeni wakijisaidia haja ndogo pembeni ya kuta za uwanja huo bila aibu. Hata mashabiki wa kike wanaokuja kuangalia mpira wanakuwa na wakati mgumu kupata huduma ya vyoo.

Hii ni changamoto kwa chama cha soka cha Zanzibar ZFA kujipanga na kuomba msaada wa kujengewa viwanja vya soka. Maana Zanzibar ina wachezaji wenye vipaji vikubwa vya soka.

Na hata timu ya Zanzibar Heroes ilijizolea mashabiki wengi katika michuano ya Challenge mwaka jana. Hivyo ni vema kuwapa mashabiki wa soka Zanzibar kile wanachostahili. Hakuna anaejua lakini Zanzibar ni mji wa kitalii wanaweza kupata bahati ya kupendekezwa kusimamia michuano ya Afrika ama Challenge kwa Afrika Mashariki na kati.


                                         Uwanja hauna majukwaa.... Mao Tse Dong Zanzibar.

HAFIDH KIDO
kidojembe@gmail.com
0713 593894/ 0752 593894
9/1/2013
Unguja, Zanzibar


No comments:

Post a Comment