Wednesday, October 10, 2012

Ripoti za kifo cha mwanahabari zazidi kumiminika... Tume ya Haki za binaadamu na utawala bora nao watoa yao...

 Mwenyekiti wa tume ya haki za binaadamu na utawala bora nchini jaji kiongozi mstaafu Amiri R. Manento akionyesha muhtasari wa ripoti ya mauaji ya Mwangosi kwa wanahabari leo asubuhi.



 Huyu mama anatoka idara ya habari Maelezo, namkubali sana katika suala zima la upigaji picha.

                        Mwenyekiti akisisitiza jambo wakati akijibu maswali magumu ya wanahabari.

                                      Wanahabari wakiwa kazini katika mkutano huo leo asubuhi.


Na Hafidh Kido

Ripoti ya tume ya haki za binaadamu na utawala bora nchini imebaini kulikuwepo na uvunjifu wa amani katika tukio zima lililosababisha kifo cha mwanahabari Daudi Mwangosi mjini Iringa miezi michache iliyopita.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo asubuhi wakati wa kutoa muhtasari wa matokeo ya uchunguzi wa tukio hilo lililotokea Septemba 2, mwaka huu katika kijiji cha Nyololo mjini Iringa mwenyekiti wa tume hiyo jaji kiongozi mstaafu Amiri Manento, alisema uchunguzi wao ulibaini kuwepo kwa uvujifu wa haki za binaadamu na mikataba ya kimataifa na kikanda inayohusu amani.

“Tume imejiridhisha kuwa tukio lililopelekea kifo cha Daudi Mwangosi limegubikwa na uvunjwaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora. Kwa mujibu wa katiba ya nchi yetu eneo la sheria za makosa ya jinai, azimio la kimataifa la haki za binaadamu, mkataba wa kimataifa kuhusu haki za kiraia na kisiasa na mkataba wa  kimataifa kuhusu haki za kiraia na kisiasa  pamoja na mkataba wa mataifa ya Afrika kuhusu haki za binadamu na watu.

“Kutokana na mikataba yote hiyo tume imeona kuwa jeshi la polisi katika tukio lile limevunja haki zifuatazo: haki ya kuishi, haki ya kutoteswa na kupigwa, haki ya usawa mbele ya sheria na haki ya kukusanyika na kutoa maoni,” ilisema sehemu ya ripoti hiyo ambayo imeshakabidhiwa kwa serikali kwa mujibu wa mwenyekiti wa tume hiyo.

Aidha kwa mujibu wa jaji Manento, mkutano wa kufungua matawi mawili ya chama cha chadema mjini Iringa ilipata ruhusa ya kamanda wa polisi wa wilaya ya Mufindi ambae ndie alikuwa ‘officer in-charge’ wa polisi wa eneo husika kama sheria inavyotaka lakini siku iliyofuata RPC wa Iringa alikataza mikutano hiyo kinyume na taratibu.

“Uchunguzi umebaini kuwa kamanda wa polisi mkoa wa iringa Michael Kamuhanda katika utekelezaji wa majukumu yake alikiuka sheria ya vyama vya siasa (Cap 258 RE.2002) kifungu cha 11(a) na (b) na sheria ya polisi sura (322) kwa kuingilia kazi za OCD wa Mufindi ambae ndie ‘officer in-charge’. Kwa maana hiyo amri iliyotolewa kuzuia mikutano hiyo haikuwa halali kwakuwa ilitolewa na mtu ambae hakuwa na mamlaka kisheria kutoa amri hiyo,” alisema jaji Manento.

Alipozungumzia hatua ya msajili wa vyama vya siasa nchini John Tendwa kuwaandikia barua viongozi wa vyama vya siasa kusitisha shughuli zao kwasababu ya sensa alisema suala hilo ni kinyume na sheria za takwimu kusimamisha shughuli za kijamii wakati wa sensa.

“Maelezo yaliyotolewa ndani ya barua hizo yanakinzana na sheria ya takwimu Namba 1 ya mwaka 2002 inayotoa fursa kwa wananchi kuendelea na kazi zao wakati wa sensa pia ni kinyume na sheria ya vyama vya siasa kufanya shughuli zake bila kuingiliwa,” aliongeza.

Katika hatua nyingine mwenyekiti wa tume hiyo amezungumzia ripoti nyingine zilizotangulia na kusema kila mtu anayo haki kufanya uchunguzi wa tukio hilo na kuhusu matokeo kila mtu ana namna yake ya kurekebisha jamii.

“Sisi tupo kisheria na hakuna mtu wa kutuingilia, mara nyingine changamoto tunazokutana nazo ni kutokana na ukosefu wa fedha hivyo isionekane tunabagua matukio ya kuyafanyia utafiti. Sisi ripoti yetu tumeipeleka serikalini hao wengine wataipeleka wapi?”, alihoji.

Hii ni ripoti ya tatu iliyotolewa kuhusiana na kifo cha Daudi Mwangosi katika kipindi cha wiki moja. Siku ya jumanne Octoba 8 ripoti mbili zilizokinzana za baraza la habari Tanzania (MCT) na wizara ya mambo ya ndani na ulinzi; ambapo MCT ripoti yao ilionyesha jeshi la polisi lilihusika moja kwa moja na kifo cha mwandishi huyo pamoja na chuki za muda mrefu baina ya jeshi la polisi na wanahabari wa mkoa wa Iringa.

Wakati ripoti ya wizara iliyopewa jina la ripoti ya Dk Nchimbi, imetoa majibu tofauti kwa kueleza kuwa jeshi la polisi halikuhusika na mauaji hayo kabisa.

HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
10/10/2012      




No comments:

Post a Comment