Tuesday, October 9, 2012

Hii ni habari kwa ufupi kuhusu ripoti ya kifo cha Mwanahabari Daud Mwangosi. Nitaitafuta 'soft copy' ya ripoti nzima halafu niimwage hapa nanyi musome kwa kiswahili na kikoloni.



Na Hafidh Kido
Ripoti ya timu maalum iliyoundwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) na jukwaa la wahariri Tanzania (TEF) kuchunguza mauaji ya mwandishi wa habari Daudi Mwangosi alieuwawa Septemba 2 mwaka huu imegundua kuwa kulikuwepo na mahusiano mabaya baina ya polisi wa mkoa wa Iringa na waandishi wa habari.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo asubuhi wakati wa kuzindua matokeo ya ripoti hiyo katibu mkuu wa MCT Kajubi Mukajanga, alisema kuanzia mwishoni mwa mwaka jana mahusiano baina ya polisi na waandishi wa habari mkoani Iringa yalikuwa mabaya kiasi cha kuwafanya waandishi kupata mazingira magumu kufanya kazi na jeshi hilo.
“Uchunguzi wa awali wa hali ya mahusiano kati ya viongozi wa Mkoa wa Iringa wakiwamo Polisi na waandishi wa habari kabla ya mauaji ya Mwangosi ulibaini kwamba mahusiano hayakuwa mazuri na yanagubikwa na kutoaminiana kati ya pande hizo mbili tangu robo ya mwisho wa mwaka 2011,” alisema Kajubi.
Akifafanua njia walizotumia kufanya uchunguzi huo Kajubi alieleza kuwa “Timu yetu ilihusisha watu watatu John Misenyi kutoka MCT upande wa machapisho na utafiti, wa pili ni Haruna Shamte kutoka jukwaa la wahariri pamoja na Simon Berege ambae ni Mhadhiri chuo kikuu cha Tumaini.
“Mchakato wa kukusanya taarifa hizi ulihusisha mbinu za uandishi wa kiuchunguzi wa hali ya juu kwa kuhoji wananchi waliokuwepo katika eneo la tukio, jeshi la polisi, viongozi wa chadema, waandishi wa habari waliokuwepo eneo la tukio na majeruhi walioshiriki maandamano ya chadema,” Kajubi.   
Akitolea mfano wa matukio yaliyoashiria mahusiano mabaya baina ya polisi na wanahabari mkoani humo Kajubi alisema ripoti inaonyesha kuwa Novemba mwaka 2011, mwandishi Lauren Mkumbata wa ITV alipigwa vibaya huku vifaa vyake vya kazi vikiharibiwa kwa makusudi na aliyekuwa mkuu wa polisi Iringa OCD Mohamed Semunyu, wakati akiwa kazini.
Katika tukio jingine ripoti hiyo inaeleza kuwa katika ziara ya makamu wa Rais Mohammed Gharib Bilal mkoani humo February 2011, waandishi walilazimika kulala kwenye basi walilosafiria kutokana na viongozi wa mkoa na jeshi la polisi kupuuza kuwapatia hoteli ya kulala pamoja na huduma nyingine.
Aidha ripoti hiyo yenye kurasa thalathini imebainisha kuwa katika siku ya tukio la kuuwawa Mwangosi jeshi la polisi lilionekana kuwakwepa waandishi wengine waliotoka mikoa tofauti na Iringa ambao waliletwa na chadema katika mikutano ya vuguvugu la mabadiliko. Miongoni mwa waandishi hao ni waandishi kutoka Dar es Salaam na mikoa mingine lakini hakuna hata mmoja alieguswa, hivyo hiyo inadhihirisha ni namna gani jeshi la polisi lilikuwa likijua mipango yao.
“Suala la kukosewa na kutotambuliwa Mwangosi halipo kabisa kwasababu polisi waliwafukuza, kuwapiga, kuwajeruhi na hatimae kumuua mwandishi ambae walikuwa wakimjua vizuri kabisa. Marehemu Mwangosi alizingirwa na kupigwa na polisi wasiopungua saba na kuuwawa wakati polisi mmoja mwandamizi alijeruhiwa vibaya.
“Matokeo haya yanathibitishwa na maelezo pamoja na ushahidi uliokusanywa kwa kutumia picha za video na ushahidi mwingine muhimu wa taarifa za vyombo vya habari,” ilisema taarifa hiyo.
Wakati huohuo mjumbe wa umoja wa vilabu vya habari nchini (UTPC) Abubakar Karsan, alieleza masikitiko yake kutokana na tukio hilo na kudai kuwa sifa ya Tanzania imeharibika kwani haijawahi kutoke katika historia ya Tanzania mwandishi kuuwawa akiwa kazini.
“Kwa kuona hivyo tumeamua kumuenzi ndugu Mwangosi kwa kuifanya tarehe ya kifo chake September 2, kuwa ndiyo ya mkutano mkuu wa UTPC kila mwaka, kadhalika tutaanzisha tuzo ya uandishi uliotukuka tutakayoipa jina la Mwangosi na mwisho tutaanzisha mfuko wa kusaidia waandishi wanaopata matatizo wakiwa kazini na kuipa jina la Mwangosi fund,” Karsan.
Daudi Mwangosi ni mwandishi wa kituo cha Channel Ten cha jijini Dar es Salaam, aliuwawa katika mvutano baina ya jeshi la polisi na wafuasi wa Chadema kijijini Nyololo, Wilaya Ya Mufindi Mkoani Iringa mnamo Septemba 2 mwaka huu.
HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
09/10/2012


NB: Nimefundishwa katika uanahabari kutokubali kushindwa, leo nimefanya kituko cha mwaka baada ya kusahau kuenda mjini na Kamera. Hivyo nilichofanya baada ya kurudi nyumbani nikaandika hiyo habari halafu nikaipiga picha hiyo ripoti. Sina picha ya viongozi wa MCT walioisoma hiyo ripoti....

No comments:

Post a Comment