Sunday, October 14, 2012

tumkumbuke mwalimu kama mwanafalsafa na mwandishi wa vitabu....


Ndugu zangu,
Si vema leo mwanamapinduzi na mjamaa mwenzangu anatimiza mika 13 tangu kutangazwa kifo chake halafu ninyamaze bila kusema chochote. Sidhani ni ustaarabu.
Sijajiandaa kuandika makala katika gazeti lolote mwaka huu kama nilivyozoea kufanya hivyo miaka sita iliyopita kila mwaka. Si kwasababu ya kuizoea siku yenyewe wala si sababu ya uvivu, bali nadhani inatosha tuliyoyaandika kuhusu Mwalimu Nyerere. Inafika wakati mada na mijadala inajirudia mpaka kupoteza ladha na lengo.
Nina ushauri, kwanini tusiache kumuandika Mwalimu kutokana na nafasi za kisiasa ama ukombozi wa bara la Afrika alizowahi kuzishika. Badala yake tuanze kuangalia sehemu ya pili ya maisha yake ambapo sehemu hiyo haina washabiki wengi; hata sijui sababu ni nini.
Nataka kumuangazia Mwalimu katika anga ya uandishi wa vitabu na uanafalsafa. Naam hayati Julius Kambarage Nyerere alikuwa mwanafasihi mzuri sana. Akiamua kuyaweka mawazo yake katika maandishi nafsi yako itafurahi. Nimebahatika kusoma kitabu chake kinachohusu UJAMAA.
Hakika nimepata maana pana na faida ya kutosha kuhusu ujamaa wa kiafrka ‘African Socialism’. Mwalimu katika kitabu hiki amechambua maana nzima ya itikadi ya ujamaa, amejibu maswali yaliyokuwa yakiulizwa katika jamii juu ya sera ya ujamaa na kujitegemea.
Watanzania wengi mwanzoni mwa miaka ya 60, baada ya uhuru walishindwa kumuelewa Mwalimu katika sera hii ya ujamaa na kujitegemea. Wengi walitafsiri moja kwa moja ‘ujamaa’ ni umoja, umajumui, kushirikiana. Na ‘Kujitegemea’ ni ubinafsi, kufanya mambo kwa kujiamulia mwenyewe bila kutaka ushauri ama msaada wa aina yoyote kutoka upande wa pili.
Hivyo wengi walikanganywa na maneno haya mawili, lakini katika kitabu kile Mwalimu alichambua vizuri na watu wakaelewa. Hivyo nawashauri watanzania na waafrika kusoma vitabu vilivyoandikwa na baba wa taifa hili. Uzuri vipo kwa lugha mbili, kizungu na Kiswahili.
Kwa upande wa falsafa, sitopata wapinzani wengi katika hili. Maana Mwalimu alikuwa na kipaji cha kuelezea jambo kwa kina na likaeleweka, hata liwe na utata namna gani.
Wakati wa mwanzo wa utawala wale kulikuwa na utata juu ya kuanzishwa vijiji vya ujamaa. Na lawama zikamshukia Waziri Mkuu wake Mzee Rashid Mfaume Kawawa. Mwalimu aliacha kwanza wananchi wamalize hasira zao, baadae alitafuta muda na kuanza kuelezea faida za vijiji vya ujamaa. Leo hii fada yake inaonekana, vijiji vingi ambavyo baadae viligeuka miji vimetokana na vile vijiji vya ujamaa.
Sina haja ya kuumiza kicha katika hili, yapo mambo mengi ambayo hata hayahitaji ufafanuzi wala msomaji kuwa na elimu ama umri mkubwa kuweza kutambua na kufahamu kuwa Mwalimu alikuwa mwanafalsafa wa kiafrika wa wakati wake.
Tazama matatizo ya muungano alivyoyajadili kiasi kila upande ukajiona namna walivyofanya makosa. Kifupi alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kuzungumza, na si kuzungumza tu bali kueleweka katika mazungumzo yake.
Hivyo, ushauri wangu kwa watanzania ndiyo huo, someni sana maandishi ya Mwalimu. Tafuteni vitabu vilivyochapisha hotuba zake musome namna alivyojua kucheza na akili za wasikilizaji wake, wazungu wanaita ‘inspirational speaker’
Naomba niishie hapa kwa leo…..
HAFIDH KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
14/10/2012

No comments:

Post a Comment