Wednesday, October 3, 2012

Ugunduzi wa mafuta na gesi Tanzania iwe ni baraka kwa uchumi na si laana.



Na Hafidh Kido

Nchi nyingi za kiafrika zimekuwa zikiingia katika machafuko ya kisiasa mara baada ya kugundua utajiri wa mafuta na gesi asilia.

Sababu zinaweza kuwa ni usimamizi mbovu wa mikataba na mgawanyo wa rasilimali hiyo kwa wananchi kunakoibua chuki za wananchi wanapobaini kuibiwa rasilimali zao na wazungu ambao hawawanufaishi chochote zaidi ya kuendelea kuwadidimiza katika umaskini.

Kibaya zaidi hawa wanaojiita wafadhili hawaishi kuzinyooshea nchi za kiafrika kidole cha lawama kuwa hawana usimamizi bora wa rasilimali zao ilhali wao kwa namna moja ama nyingine hushirikiana na makampuni ya kibepari kuchota mafuta katika nchi maskini huku wakichonganisha makundi katika nchi hizo ili yatokee mapigano ambayo huwapa mwanya wa kuja tena kama wasuluhishi.

Mwanzoni mwa mwaka huu waziri mwenye dhamana ya nishati na madini nchini Prof. Sospeter Muhongo, alitangaza habari njema ya kupatikana mafuta na gesi kilomita 80 kutoka pwani ya Lindi katikati ya bahari.

Makampuni mawili ya Marekani na Norway (Statoil na Exxan Mobil) yaliyopewa kazi ya kutafuta mafuta kwa miaka mitatu walitoa habari njema kwa kueleza kuwa kuna gesi inayofikia zaidi ya futi za ujazo trilioni 20.
Prof. Muhongo, aliendelea kueleza kuwa takriban makampuni 19 yalikuwa yakitoa ushirikiano katika utafutaji huo, na kubainisha kuwa kisima kimoja kimeigharibu Serikali dola za Kimarekani milioni 100 mpaka 150 katika kufanya upembuzi yakinifu.

Hatua ya pili ambayo watanzania walikuwa wakiisubiri kwa hamu kutoka Serikalini ni namna rasilimali hiyo itakavyochimbwa na kuinufaisha nchi.

Ni kama Serikali imeligundua hilo na kutangaza rasmi kuwa leseni za uchimbaji hazitotolewa mpaka hapo Serikali itakapojipanga katika sera na sheria zitakazoelekeza namna gani wataingia mikataba na makampuni ya uchimbaji mafuta na gesi bila kupata hasara ama mikanganyiko kama wanayoipata katika madini mengine hasa Dhahabu, almasi na tanzanite.

Kituo cha sheria na haki za binaadamu nchini wakishirikiana na asasi nyingine za kiraia za SIKIKA na Hakielimu waliweka wazi msimamo wao kwa kuitaka Serikali kutosimamisha kwa muda bali wasitishe kabisa mchakato wa uchimbaji mafuta na gesi ili wajipange.

Mkurugenzi wa SIKIKA Irenei Kiria, alisema katika nchi nyingi duniani mafuta na gesi vimekuwa na msaada mkubwa katika kuinua uchumi lakini kwa Tanzania hali itakuwa tofauti ikiwa hatua stahiki hazitofuatwa.

Kilio kikubwa cha Kiria kiliegemea upande wa wataalamu wazalendo na namna ya ukusanyaji kodi, mirabaha kutoka kwa makampuni ya kigeni ambayo mara nyingi wao ndiwo wanaojihusisha na uchimbaji huo hasa ikizingatiwa shughuli hizo zinahitaji mitaji mikubwa na ujuzi wa hali ya juu.

“Tusifanye maamuzi yasiyo na tija, bado hatujajiandaa kwa wataalamu wa kutosha juu ya masuala ya mikataba na usambazaji mafuta na gesi. Serikali imesitisha suala hili kwa muda lakini sisi tunasema isimamishe kabisa mpaka hapo nchi itakapojitosheleza kimkakati juu ya rasilimali hizi.

“Kwa hivyo mchakato mzima wa utafutaji, uchimbaji na usambazaji gesi asilia na mafuta sambamba na mikataba, leseni, usimamizi, ukusanyaji kodi na mirabaha lazima isimamiwe vyema kwa uwazi na ushirikishwaji wa hali ya juu ili kila mwananchi ajiridhishe na kuona upatikanaji wa rasilimali hizi ni faida kwa nchi na maendeleo kwa ujumla,” alisema Kiria.

Aidha muungano wa taasisi hizo tatu ulisisitiza uundwaji wa sera na sheria zitakazolinda mchakato wa upatikanaji gesi na mafuta ili kuhakikisha nchi haiingii katika matatizo kama mifano inavyoonekana katika nchi nyingi za kiafrika ambapo upatikanaji wa mafuta umekuwa na laana badala ya baraka.

Kwa upande wake meneja wa utafiti na sera Hakielimu Godfrey Boniventure, alisema Tanzania mpaka sasa haijaandaa hata mzalendo mmoja kuweza kupata nafasi ya kutoa huduma katika uzalisahji na usambazaji mafuta na gesi. Hii ikijumlisha wataalamu wa uchimbaji, usambazaji na hata watu wa kawaida watakaotumika kama washauri juu ya rasilimali hizo adimu duniani.

“Hatutaki kusikia hadithi ya kasungura kadogo, huu ni wakati wetu watanzania tunatakiwa kuitumia nafasi hii kujinufaisha kiuchumi na kijamii. Serikali ipange mikakati na kuhakikisha tunapata sera na sheria muafaka kulinda rasilimali hizi,” alisisitiza Boniventure.

Hivi karibuni, Waziri Kivuli wa Fedha na Mipango ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe alikaririwa na vyombo vya habari akisema kitu hichohicho kuwa Serikali inapaswa kusitisha utoaji wa leseni za utafutaji na uchimbaji wa gesi na mafuta kwa miaka 10 ili ijipange na kuweza kumudu kusimamia yenyewe uvunaji wa rasilimali hiyo.

Nilipozungumza na Zitto kwa njia ya simu alinieleza kuwa Serikali lazima iwe makini sana katika suala la mafuta maana rasilimali hii ni ya watanzania tofauti na madini ambapo makampuni ya uchimbaji yanapopewa vibali madini yanakuwa ni yao.

“Watu hawajui kitu kimoja, mafuta ni mali ya taifa tofauti na madini mengine. Makampuni yanapokuja kuchimba mafuta ama gesi wanachopata kutoka kwetu ni tozo la shughuli ya uchimbaji ila kinachopatikana ni mali ya Serikali.

“Kwa mfano ikiwa kampuni itatumia gharama ya dola 20 kuchimba pipa moja, hicho ndicho kiasi wanachotakiwa walipwe labda na faida kidogo lakini mafuta yetu hawayagusi hata tone. TPDC na TRA wanachotakiwa kufanya ni kuhakikisha wanasimamia mikataba na kuwabana wawekezaji wababaishaji ambao mara nyingi hutumia ujanja kuiibia Serikali wakishirikiana na viongozi walafi, naamini sheri na sera zipo kinachokosekana ni utekelezaji tu” alisema Zitto.

Nilichojifunza kutoka katika kauli ama msimamo wa Zitto ni namna Serikali na vyombo vyake wanavyotakiwa kujiandaa kukabiliana na ubabaishaji wa makampuni ya kigeni ambayo muda si mrefu yataanza kutiririka kuomba nafasi ya kuchimba mafuta.

Ni muhimu sheria ya kusimamia mafuta na gesi itungwe  ili kuhakikisha mgawanyo wa mapato unafikia malengo kwa kuelekezwa katika shughuli za ujenzi wa barabara, hospitali, shule na mambo mengine muhimu ambayo yatainua uchumi ili kila mwananchi aone kuna mabadiliko chanya mara baada ya kugundulika rasilimali hii adimu duniani.

Zitto hakuishia hapo tu lakini aliitaka Serikali kujenga chuo mkoani Mtwara ambacho kitapika wataalamu wa uchumi na mikataba katika masuala ya gesi na mafuta.

“Si lazima tukawa na wataalamu wa uchimbaji mafuta tu, mimi maoni yangu jamii ya watanzania ikodolee macho sana katika masuala ya mikataba na mahesabu ya uzalishaji mafuta. Hapa ndipo nchi nyingi za kiafrika zinapoibiwa rasilimali zao, lazima tupate wataalamu wazalendo ambao watakuwa wameiva katika uchumi wa mafuta na mikataba, tuwe na watu ambao wanaweza kubishana na kung’amua ujanja wa makampuni haya ya kigeni. Kujua nchi itapata asilimia ngapi na mchimbaji anapata ngapi hapo ndipo tunapoibiwa, kadhalika gharama za kuchimba pipa moja na namna ya kuwalipa wachimbaji, hapo ndipo tunapoibiwa.

“Unajua nimejifunza mambo mengi sana katika makampuni haya ya kigeni, wanatuibia sana maana wana wataalamu wa hali ya juu katika masuala ya mikataba na uchumi, sisi bado tupo nyuma na hapo ndipo wanapotuibia.

“Vilevile tutumie nafasi hii kuwapa ajira vijana maana katika uchimbaji mafuta baharini kunatumika meli ambazo zinahitaji mabaharia. Kwa mfano kwa sasa kule Mtwara kuna meli nne za utafutaji mafuta na kila meli inaajiri wastani wa mabaharia 400 kwa mwezi 200 kila baada ya wiki mbili wanaingia kwa kupokezana. Lakini watanzania wapo wachache sana wengi ni raia wa kigeni na hata vyakula wanavyokula wakiwa melini vinatoka nchi jirani ya Kenya watanzania tumelala tu,” alisisitiza.

Nimeielewa mantiki ya kauli yake, ni kuwa si wataalamu waliosoma tu lakini hata ambao wana elimu ya chini wanaweza kupata ajira katika uchimbaji mafuta, mathalani mafundi mchundo wanaweza kupata ajira melini na kuchomea mabati ya meli, ama wapishi na hata wauza vyakula kwa wafanyakazi wa meli za uchimbaji mafuta.

Serikali inaweza kuweka sheria ya kuwabana wageni kutojihusisha na shughuli ndogondogo kama hizo. Kama watakuja wataalamu wa utafutaji na uchimbaji mafuta basi wasije na wafanyakazi bali wafanyakazi watoke hapahapa.

Na hivi ndivyo nchi za kiarabu zilivyofanikiwa katika uchumi wao, ni kwa njia hii hii ya kuwabana wageni wasifanye shughuli ambazo wazawa wanaweza kuzifanya tena kwa uwezo mkubwa kuliko wao.

Leo ukienda nchi yoyote ya kiarabu ama kirusi katika machimbo ya mafuta huwezi kupata kazi kirahisi, unaweza kukuta mtaalamu mkuu wa uchimbaji ni mzungu lakini wasaidizi wake wote ni waarabu. Maana yake baada ya miaka kadhaa ijayo hawatahitaji wataalamu kutoka nje bali watakuwa na wataalamu wao wazalendo walioiva, nchi inapata faida na wananchi wanapata ajira.

HAFIDH A. KIDO
DAR ES SALAAM, TANZANIA
0713 593894/ 0752 593894
03/10/2012




No comments:

Post a Comment