Wednesday, September 19, 2012

Kampala yajikomboa kwa kupata usafiri wa kisasa..


 Jembe nikipita pembeni ya moja ya mabasi hayo ya kisasa yaliyomwagwa jijini Kampala. Yanavutia kweli.

 Hiki ni kituo cha daladala cha New Tax Park. Kipo katikati ya jiji la Kampala. Hiace hizi tunazipeleka wapi?

 Pikipiki ni usafiri maarufu jijini Kampala lakini una hatari moja, nayo ni ajali na nauli kubwa. Mabasi yamekuwa mkombozi wa wengi.

                               Moja ya Hiace zikiwa katikati ya jiji... Hazitakiwi tena hizi.


Kampala imeamua kujikomboa katika matatizo ya usafiri kwa kuamua kuingia mkataba wa miaka mitano na kampuni ya usafirishaji iitwayo Pioneer Easy Bus ambayo imeahidi kuingiza mabasi ya kisasa yapatayo 522.
Jembe nilijionea mabasi hayo na kuvutiwa kuandika chochote hasa ukizingatia jiji letu la Dar es Salaam muda si mrefu litaingia katika harakati ya kupokea mabasi ya kisasa zaidi kuwahi kutokea katika historia ya nchi yetu.
Lakini bado tatizo lipo, ni namna gani meya wa Kampala Lord Lukwago ataweza kuyaondoa magari madogo maarufu ‘hiace’ katika mji wa kampala ambayo yalikuwa yakitoa usafiri kwa muda mrefu.
Nikiwa Kampala mwanzoni mwa mwaka huu wakati huduma ya mabasi hayo ikianza, nilishuhudia vurugu na kutoelewana baina ya madereva wa mabasi hayo na madereva wa ‘hiace’ maana hakika mabasi yameletwa ili kuja kupunguza adha ya usafiri katika jiji hilo linalokuwa kwa kasi. Lakini na hawa waliokuwepo kwa muda mrefu tunawasaidia vipi?
‘Hiace’ nauli ni 1000 ya Uganda, na haya mabasi mapya nauli ni 800, 200 pungufu. Unadhani abiria atakubali kuenda kupinda mgongo katika ‘hiace’ tena kwa nauli ya juu wakati anaweza kukaa kwa raha katika basi zuri kwa nauli pungufu?
“Lunaana, Lunaana paka Zana.” Hiyo ni sauti ya kondakta wa basi kubwa akimaanisa ‘mia nane mpaka zana’ Zana ni eneo la kampala, yaani kutoka Nakasero Kampala mjini mpaka zana ni mia nane. Wakati ‘Hiace’ wanafanya elf moja.
Si hivyo tu hata maeneo ya karibu viongozi wa serikali za mitaa ama wilaya za Kampala waliweka ngumu kidogo kuukubali mradi huu wa mabasi mapya. Maana sehemu kama Wakiso, Entebbe na Mukono walikuwa na ubishi mkubwa kuyakubali mabasi hayo.
Unajua sababu? Watakosa pesa za kuiibia Kampala City Council. Maana huu mradi utasimamiwa na mtu binafsi, hivyo pesa zitakuwa zinapelekwa jiji moja kwa moja. Na wao walishazoea kuiibia Kampala City Council kwa kusajili ‘hiace’ hewa na baadhi ya vigogo kuingiza magari yao halafu hawalipi kodi. Hatari kubwa hii.
Ilibidi bunge la Uganda liingilie kati chini ya kamati ya usafiri na kuamua mradi huo uanze mara moja mwanzoni mwa mwaka huu. Na kwa kuanza kampuni hiyo ya Pioneer Easy Bus katika mwezi March iliingiza mabasi 60, halafu baadae ikaongeza mengine 40 na kufanya mabasi 100. Na mengine 422 yanakuja kukamilisha idadi ya mabasi 522. Si raha hii jamani?  
Kampuni hiyo imewekeza kiasi cha shilingi bilioni 23 za kiganda sawa dola za kimarekani milioni 10.
Mabasi hayo yatapita maeneo muhimu ambayo yalikuwa na tabu ya usafiri mjini Kampala ambayo ni Mukono, Luzira, Bweyogerere, Ntinda, Mulago, Namugongo, Nakawa, Nateete, Rubaga na Zana.
Mungu atawajaalia kuweza kumaliza tatizo la usafiri katika mji unaokuwa kwa kasi sana Afrika Mashariki na kati.
HAFIDH KIDO
KAMPALA, UGANDA
19/09/2012
+256790836878/ +255752593894

No comments:

Post a Comment