Friday, September 21, 2012

MREJESHO: Matatizo ya Maji Kata ya GOBA


Thursday, September 20, 2012

Pamoja na manispaa ya Kinondoni kutoa shilingi milioni moja na nusu tarehe 14 Septemba 2012 kwa ajili ya kufunga mita na kuanza kusukuma maji ya mradi wa Goba, tarehe 19 Septemba 2012 wakati wa Mkutano wa Baraza la Madiwani nimemtaka Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kuwawajibisha watendaji waliozembea na kusababisha matatizo hayo kudumu kwa muda mrefu.

Izingatiwe kuwa kiasi hicho ni nyongeza baada ya awali kutolewa milioni tatu na Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo la Ubungo (CDCF) kwa ajili ya kuwezesha huduma ya maji kupitia mradi huo kurejea.

Ikumbukwe kuwa mwezi Agosti 2011 maji yalikatwa kwenye kata ya Goba kutokana na DAWASCO kuidai kamati ya mradi wa maji shilingi milioni 18 na katika kufuatilia deni hilo nilipata taarifa za Kamati ya Maji kuwasilisha malalamiko DAWASCO ya kutokukubaliana na kiwango hicho cha deni na pia kwa Manispaa ya Kinondoni kuhusu matatizo ya kiutendaji na kifedha katika mradi huo wa maji ikiwemo ya upotevu wa fedha.

Tarehe 5 Septemba 2011 niliwaunganisha wananchi kwa pamoja tukaandamana kwenda ofisi ya DAWASCO makao makuu ambapo tulikutana na mtendaji mkuu wa kampuni husika na kufanya mazungumzo ambayo yalisaidia baadhi ya hatua za msingi kuchukuliwa ikiwemo DAWASCO kurejesha huduma ya maji katika bomba kuu baada ya sehemu ya deni kulipwa na makubaliano kufikiwa kuhusu malipo ya kiwango kilichobaki.

Pia tarehe 24 Oktoba 2011 niliandika barua kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kutoa mwito wa hatua za dharura kuchukuliwa ili kuhakikisha uhakiki unafanyika wakati huo huo wananchi wengine wanaendelea kupata huduma ya maji; lakini udhaifu wa kiutendaji umefanya hatua ziwe za kusuasua.

Hata hivyo, pamoja na huduma ya maji kurejeshwa katika bomba kuu haikuweza kusambazwa kwenye mabomba ya wananchi pamoja na vioski vya kutolea huduma kwa sababu ya udhaifu wa utendaji katika ngazi ya kata na katika kamati ya maji hivyo tarehe 26 Januari 2012 niliwaunganisha wananchi kufika Manispaa ya Kinondoni kwa ajili ya hatua za haraka za Mkurugenzi wa Manispaa.

Kufuatia hatua hiyo Mkurugenzi wa Manispaa Fortunatus Fwema alifanya ziara katika kata ya Goba tarehe 31 Januari 2012 na kuagiza kwamba ndani ya tano maji yatoke katika kata hiyo na kuagiza Mhandisi wa maji na timu yake waweke kambi katika kata ya Goba mpaka maji yatoke kwa gharama za halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

Hata hivyo, muda huo ulimalizika bila maji kupatikana na kikosi kazi kilikabidhiwa jukumu tarehe 28 Februari 2012 kushughulikia kile kilichoelezwa kuwa ni kuanza uchunguzi wa Bomba la Maji kuanzia Tanki Bovu hadi kwenye tanki la Matosa ili kubaini wizi, upotevu wa maji na uharibifu wa miundombinu.

Katika kipindi cha kati ya Februari mpaka Agosti 2012 nimefuatilia Manispaa kwa njia mbalimbali na wakati wote maelezo yamekuwa kazi hiyo inachukua muda mrefu kwa sababu ya urekebishaji wa miundombinu ambapo Manispaa ya Kinondoni ilikubali kutoa mita 15 pamoja na stendi za bomba mpya kwa ajili ya kufunga katika bomba kubwa kwenye njia zinazoelekea kwa wananchi ili kudhibiti wizi na upotevu wa maji pamoja na kufanya marekebisho katika mabomba na gate-valves zilizohujumiwa.

Ikumbukwe kuwa matatizo ya maji kata ya Goba yanafahamika kwa mamlaka zote husika kuanzia Wizara ya Maji, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Manispaa ya Kinondoni na vyombo vya dola kuanzia mwaka 2007 mpaka mwaka 2012 lakini hatua kamili hazijachukuliwa kwa wakati.

Wananchi wa Goba wamepoteza uvumilivu kwa kuwa hatua hazichukuliwi kwa haraka na kutokana na hali hiyo mbunge kama mwakilishi wa wananchi nimeumua kuungana nao katika kutaka uwajibikaji wa watendaji wote waliozembea na kusababisha matatizo hayo kudumu kwa muda mrefu.

Nimefikia hatua hiyo kwa sababu njia zote za kawaida kupitia vikao na mawasiliano ya kiofisi zinaelekea kukwamishwa na uzembe, hujuma na urasimu na udhaifu wa kiutendaji katika ngazi mbalimbali.

Katika kushughulikia masuala la maji kwenye kata ya Goba, narudia kusisitiza hatua zifuatazo kuendelea kuchukuliwa kwa haraka na mamlaka zifuatazo:

Mosi; Mamlaka za Manispaa ya Kinondoni zikiongozwa na Meya na Mkurugenzi zinapaswa kufuatilia kwa haraka kuhakikisha maji yanarejeshwa Goba. Hatua hii iende sambamba na kupanua wigo wa maji Goba kwa kutekeleza kwa haraka upatikanaji wa maji kutoka pia mradi wa maji toka Madale Kisauke. 

Manispaa izingatie matatizo yaliyopo kwenye miradi ya maji inayoendeshwa na manispaa pamoja na kamati za wananchi au vyama vya watumia maji katika maeneo mbalimbali. Hivyo, pamoja na kuchukua hatua kuhusu mradi wa maji wa Goba, Manispaa ichukue hatua juu ya miradi iliyokwamba ukiwemo wa Mbezi Msumi na Makabe. Pia, Manispaa ya Kinondoni inapaswa kufanya mabadiliko kwenye idara ya maji kwa kuwa ina udhaifu mkubwa wa kiutendaji.

Pili; Wizara ya Maji, Mamlaka ya maji safi na maji taka (DAWASA) na Kampuni ya maji safi na maji taka (DAWASCO) zizingatie kwamba maeneo ya pembezoni ya Dar es salaam ambayo awali yalikuwa vijiji sasa ni mitaa yenye wakazi wengi. Hivyo, maeneo kama kata ya Goba na mengine ya pembezoni yanapaswa kuunganishwa moja kwa moja na mtandao wa maji chini ya mamlaka husika kwa mujibu wa sheria iliyounda DAWASA badala ya mfumo uliopo ambalo haulingani na mahitaji.

Tatu; vyombo vya ulinzi na usalama vinapaswa kushughulikia vyanzo vya migogoro badala ya kusubiri mpaka matatizo yanapoibuka kwa kushughulikia kwa wakati malalamiko yanayotolewa. Mathalani, Jeshi la Polisi (Ofisi ya DCI) na TAKUKURU wanapaswa kutoa kauli kuhusu hatua zilizochukuliwa juu ya tuhuma za ufisadi na ukiukwaji wa sheria katika mradi wa maji Goba ambazo zimetolewa na wananchi kwa mamlaka husika kuanzia mwa 2007.

Mamlaka husika zizingatie kuwa tarehe 27 Februari 2011 na 6 Machi 2011 nilifanya mikutano na wananchi katika kata ya Goba ambapo risala ya wananchi pamoja na ripoti ya ukaguzi wa mradi wa mradi wa maji Goba ya mwaka 2007 zilizosomwa ambazo zilieleza bayana matatizo yaliyokuwepo kwenye kamati ya maji pamoja na mradi kwa ujumla ikiwemo yaliyohusu upotevu wa fedha ambayo vyombo vya dola vilipatiwa taarifa lakini hatua hazikuchukuliwa kwa wakati. 

Kwa nyakati mbalimbali nimeziandikia barua rasmi mamlaka husika kuhusu masuala haya na mengine  na kutokana na kutochukua hatua kwa wakati mwezi Agosti 2012 kabla ya kumalizika kwa mkutano wa Bunge nilikutana na Waziri Mkuu Mizengo Pinda na kumweleza haja ya kuingilia kati ili ufumbuzi upatikane mapema.

John Mnyika (Mb)
19/09/2012


No comments:

Post a Comment